HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, December 6, 2021

NYUMBA 133, SHULE ZAEZULIWA NA UPEPO

 


Na Yeremias Ngerangera, NAMTUMBO.
NYUMBA 133 zikiwa za bati 120 na nyumba za nyasi 13 za wananchi wa Kijiji cha Likuyuseka wilayani Namtumbo mkoani Ruvuma zimeezuliwa na upepo mkali ulioambatana na mvua kubwa iliyonyesha siku ya jumanne wiki hii na kuezua nyumba , pamoja na madarasa ya shule ya msingi Likuyusekamaganga.

Diwani wa kata ya Likuyuseka kassimu Gunda alisema mvua hiyo ilianza muda wa saa kumi jioni iliyotanguliwa na upepo mkali na kusababisha nyumba za wananchi kuezuliwa pamoja na madarasa ya shule ya msingi Likuyusekamaganga.

Agnetha mlowe mratibu elimu kata, kata ya Likuyuseka alisema yeye ni muhanga kutokana na nyumba aliyokuwa anaishi kuezuliwa na upepo huo na kulazimika kuhamia nyumba ya jirani kupata hifadhi.

Mwalimu mkuu wa shule ya msingi likuyusekamaganga Boniface Reammy Sichela alisema madarasa 3, ofisi ya walimu 1 na nyumba 1 ya shule zimeezuliwa na upepo huo huku akidai hakuna mwanafunzi au mwalimu yoyote aliyeathirika na tukio hilo kimwili kwa kuwa wakati tukio hilo linatokea wanafunzi tayari walisharudishwa nyumbani.

Mtendaji wa kata ya likuyuseka Fransis hunja alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kudai kuwa hakuna maafa yoyote yaliyotokea kwa wananchi kutokana na tukio hilo japo kuwa kuna wananchi 8 waliopata majeraha madogo madogo na kati ya hao sita walipelekwa zahanati ya likuyuseka na wakapatiwa matibabu na wawili walienda kituo cha afya Namtumbo na wakapatiwa matibabu.

Kwa mujibu wa Hunja alidai waathirika wote waliofikishwa zahanati ya Likuyuseka na kituo cha afya Namtumbo kupatiwa matibabu afya zao zinaendelea vizuri na wanaendelea na shughuli za kilimo kama kawaida.

Mvua kubwa na upepo mkali ulioezua nyumba na shule katika Kijiji cha Likuyuseka umewarudisha nyuma wananchi wa Kijiji hicho kutokana na baadhi ya wananchi kutokuwa na uwezo wa kugharimia kununua bati,misumari na fedha za kumlipa fundi ili kuezeka nyumba zao kama ilivyokuwa awali badala yake wamerudia kuezeka nyasi ili Maisha yaendelee.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad