HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, December 2, 2021

Baada ya Ng'ombe 17 kufa Kiutata Monduli,wafugaji wamuomba Rais Samia kusikia kilio chao

 



Na John Walter-Monduli.

Serikali mkoani Arusha imechukua Sampuli 17 ya Ng'ombe waliokufa Kiutata katika kijiji cha Popo Migungani A eneo la Mto wa Mbu wilaya ya Monduli ili kujua chanzo cha vifo hivyo.

Daktari wa Mifugo mkoa wa Arusha Dr. Sabas Shange amethibitisha kufa kwa ngo'mbe hao 17 na kufanya uchunguzi wa awali kuona chanzo ni nini ambapo ameeleza kuwa wamefanya uchunguzi wa mazingira kwa kuangalia historia ya mifugo ilipoanzia mpaka tatizo lilipotokea na kuzichukua baadhi ya sampuli kwa ajili ya uchunguzi wa Kina. "Lakini tumejaribu kumpasua mmojawapo kujiridhisha" alisema Dr. Shange

Kufuatia hilo, Wafugaji katika maeneo hayo wamemuomba mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan na mwenyekiti wa wafugaji Taifa wapokee kilio chao na kuangalia kwa jicho la pili kwa kuwa wamepata hasara kubwa.

Mmoja kati ya wafugaji ambao mifugo yao imekufa ni Baraka Komite anasema ndani ya dakika kumi akiwa anachunga aliona Ng'ombe wa kwanza anaruka kisha kuanguka wakadhani kuwa ameumwa na Nyoka.

"Tulimkimbilia tukamkamata tuangalie nini kimetokea,lakini wakati tunamuangalia huyu, mwingine akaruka mara ghafla wakaanza kuanguka wengi"alisema Komite

Mfugaji huyo ameendelea kusema kuwa huenda ni binadamu wanaangamiza mifugo yao kwa sumu na kwamba hawatalivumilia jambo hilo huku akimuomba Rais Samia Suluhu Hassan kuwaangalia wafugaji kwani hiyo ni mara ya tatu kutokea kwa tukio kama hilo.

"Wiki mbili zilizopita kuna ng'ombe alikufa kwa ajili ya sumu na haijulikani nani amempa, hata sisi wafugaji pia ni wataalamu wa kujua mimea inayoua mifugo, kwa hiyo mnapotuambia kwamba kuna mimea imeua ng'ombe ni kitu ambayo haiwezi kuingia akilini maana ile mimea inaota kipindi cha Masika" alisisitiza Komite

Mwenyekiti wa Kijiji cha Popo John Sulle amesema muda wa saa saba na nusu mchana alipata taarifa kutoka kwa wananchi na alipofika alikuta ng'ombe saba wamelala chini wakaanza kuwapa maziwa na maji huku katika eneo hilo pua zikinusa harufu nzito kama ya sumu ambapo alitoa taarifa polisi na kwa viongozi wengine wa kijiji.

Naye mwenyekiti wa Kijiji cha Losirwa Yamati Laizer ameiomba serikali kufanya uchunguzi wa kina kwenye sampuli walizozichukua ili kujua sababu ni nini.Diwani wa kata ya Esilalei Mheshimiwa Lemia ameliomba jeshi la Polisi kufanya upelelezi wa kina juu ya tukio hilo.

Mkuu wa wilaya ya Monduli Frank Mwaisumbe ambaye alifika katika eneo hilo kuwafariji wahanga aliwapa pole na kuwataka kuendelea kuwa watulivu wakati wataalamu wanashughulikia vipimo katika maabara ili kubaini nini kilichoua mifugo hiyo.





No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad