HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, October 28, 2021

Msajili Hazina akagua upanuzi kiwanda cha sukari Kilombero

 *Uzalishaji sasa kuongezeka kwa tani 144,000 zaidi

SERIKALI kwa kushirikiana na Kampuni ya Sukari ya Kilombero imeanza utekelezaji wa mradi wa upanuzi wa Kiwanda cha Sukari cha Kilombero kitakachokuwa na uwezo wa kuzalisha tani 144,000 za sukari kwa mwaka.

Mradi huo wenye gharama ya Shilingi bilioni 584 ulioanza kutekelezwa Mei mwaka huu unatarajiwa kukamilika Juni 2024 na kuwezesha kiwanda hicho  kufikisha tani 271,000 kwa mwaka. Kwa sasa kiwanda hicho kinazalisha tani 127,000 kwa mwaka.

Akizungumza kuhusu mradi huo alioutembelea hivi karibuni Kilombero mkoani Morogoro, Msajili wa Hazina, Mgonya Benedicto aliagiza kasi na ufanisi katika utekelezaji  wake ili kufanikisha juhudi za serikali za kuondoa uhaba wa sukari  nchini na pia kuongeza pato la serikali na wananchi wanaozunguka mradi huo.

Aliongeza kusema; ”  Nataka muongeze juhudi katika utendaji kazi, kuimarisha usimamizi wa mradi na na Serikali tunaahidi kutoa ushirikiano utakaohitajika katika kufanikisha mradi huu muhimu kwa uchumi wa Taifa.”

Serikali ina hisa ya asilimia 25 katika Kampuni ya Sukari ya Kilombero, hisa nyingine zinamilikiwa na Kampuni ya Illovo Sugar Africa .

Msajili wa Hazina, Mgonya aliishukuru Menejimenti kwa kuunga mkono juhudi za Serikali katika uwekezaji huo wa kihistoria unaolenga kuongeza uzalishaji wa sukari nchini na kupunguza pengo la la mahitaji ya sukari nchini.

Naye Meneja Mkuu  wa kampuni hiyo ya Sukari Kilombero anayeshughulikia Fedha, Fakihi Fadhili alisema mradi wa upanuzi wa kiwanda hicho utaongeza kiwango cha miwa kutoka kwa wakulima wadogo wa Bonde la Mto Kilombero kutoka tani 600,000 za hivi sasa mpaka kufikia tani 1,700,000.

Alisema kwa upanuzi huo, wakulima wataondokana na usumbufu wa soko la miwa na hivyo kuongeza mara tatu ya kipato cha wakulima hao kufikia Shilingi bilioni 300 ifikapo mwaka 2028.

Aidha idadi ya wakulima wadogo watakaojihusisha na uzalishaji wa miwa inatarajiwa itaongezeka kutoka 8,000 hadi 16,000 na kunufaisha wananchi 100,000 wa maeneo yanayozunguka bonde la Kilombero.

Kwa upande wa ajira, Fakihi alisema kutakuwa na ongezeko la ajira ya moja kwa moja ya zaidi ya  watu 2,000 na ongezeko maradufu ya kodi kutoka Sh bilioni 50 zinazolipwa sasa na kampuni hiyo.

Mradi huo pia umelenga kuzalisha umeme wa megawati 10 kwa ajili ya matumizi ya kiwanda na wa ziada kuingizwa katika gridi ya taifa.

Aidha, inatazamiwa kuwa mchango wa Kampuni ya Sukari ya Kilombero kwa uchumi wa nchi utaongezeka maradufu kutoka Sh bilioni 340 kwa mwaka hadi kufikia wastani wa Sh bilioni 750 kiwanda kipya kitakapoanza uzalishaji.

Meneja Mkuu wa Kiwanda cha Sukari cha Kilombero anayeshughulikia Fedha, Fakihi Fadhili akitoa ufafanuzi kwa Msajili wa Hazina, Mgonya Benedicto namna mitambo ya kuzalisha sukari kiwandani hapo inavyofanya kazi wakati wa ziara ya Msajili wa Hazina hivi karibuni mkoani Morogoro. Msajili alikwenda kiwandani hapo kujionea kuanza kwa utekelezaji wa mradi wa upanuzi wa kiwanda unaotarajiwa kupaisha uzalishaji wa sukari kutoka tani 127,000 hadi 271,000 ifikapo mwaka 2023.

Msajili wa Hazina, Mgonya Benedicto akikagua moja ya bidhaa za sukari inayozalishwa  na Kiwanda cha Sukari cha Kilombero kilichopo Morogoro kutoka kwa Meneja Mkuu anayeshughulikia Fedha, Fakihi Fadhili wakati wa ziara ya Msajili wa Hazina aliyetembelea kiwandani hapo hivi karibuni kujionea kuanza kwa utekelezaji wa mradi wa upanuzi wa kiwanda unaotarajiwa kupaisha uzalishaji wa sukari kutoka tani 127,000 hadi 271,000 ifikapo mwaka 2023.

Msajili wa Hazina, Mgonya Benedicto akipokea maelezo ya ubora wa sukari inayozalishwa na Kiwanda cha Sukari cha Kilombero kilichopo mkoani Morogoro kutoka kwa Meneja Mkuu anayeshughukia Fedha, Fakihi Fadhili wakati wa ziara ya Msajili wa Hazina aliyetembelea kiwandani hapo hivi karibuni kujionea kuanza kwa utekelezaji wa mradi wa upanuzi wa kiwanda unaotarajiwa kupaisha uzalishaji wa sukari kutoka tani 127,000 hadi 271,000 ifikapo mwaka 2023.

Msajili wa Hazina, Mgonya Benedicto akitoa maelekezo kwa Meneja Mkuu wa Kiwanda cha Sukari Kilombero anayeshughukia Fedha, Fakihi Fadhili kuhusu namna bora ya kuongeza ufanisi katika uzalishaji wa sukari katika kiwanda hicho wakati wa ziara yake ya hivi karibuni mkoani Morogoro. Msajili wa Hazina alitembelea kiwandani hapo kujionea kuanza kwa utekelezaji wa mradi wa upanuzi wa kiwanda unaotarajiwa kupaisha uzalishaji wa sukari kutoka tani 127,000 hadi 271,000 ifikapo mwaka 2023.

Meneja Mradi wa Upanuzi wa Kiwanda cha Sukari cha Kilombero, Dennis Mdoe akitoa maelezo kwa Msajili wa Hazina, Mgonya Benedicto kuhusu utekelezaji wa mradi wa upanuzi wa kiwanda hicho wakati wa ziara ya Msajili wa Hazina aliyetembelea kiwandani hapo hivi karibuni kujionea kuanza kwa utekelezaji wa mradi wa upanuzi wa kiwanda unaotarajiwa kupaisha uzalishaji wa sukari kutoka tani 127,000 hadi 271,000 ifikapo mwaka 2023.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad