HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, June 16, 2021

BRELA wabaini mapungufu utoaji wa leseni kwa wafanyabiashara

 


Na Amiri Kilagalila, Njombe


KUTOKANA  na mapungufu yanayojitokeza katika zoezi la utoaji wa leseni kwa wafanyabiashara,wakala wa usajili wa biashara na leseni (BRELA) umetoa elimu ya sheria ya leseni za biashara kwa maafisa biashara wa mikoa mitatu ya nyanda za juu kusini.

Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya semina ya siku ya tatu kwa maafisa hao inayoendelea mkoani Njombe,afisa kutoka kitengo cha leseni katika BRELA Rajab Chambenga amesema,mchanganyiko wa utoaji wa leseni baina ya BRELA na halmashauri umesababisha maeneo mengi ada kutozwa tofauti na ana ya biashara.

Hata hivyo duru zinaarifu kuwapo kwa baadhi ya wafanyabiashara nchini wanaofunga biashara zao bila mamlaka ya toaji leseni kujua hatua inayowalazimu wakala wa usajili wa biashara na leseni kuendeleza zoezi la ukaguzi na utoaji elimu.

Aidha Chambenga anakiri kuwapo kwa Baadhi ya wafanyabiashara nchini wanaofunga biashara zao bila taarifa kuwafikia jambo linalowapa wakati mgumu pindi wanapotaka kuhuisha biashara .

"Baada ya kufanya zoezi la ukaguzi katika mikoa tofauti tumegundua leseni za kundi 'A' ambazo huwa zinatolewa na BRELA na kundi 'B' ambazo huwa zinatolewa na halmashauri,kulikuwa na mkanganyiko ambapo baadhi ya leseni ilitakiwa zitoke BRELA ikawa inatolewa na halmashauri,na kutokana na hilo hata ada ambazo zilikuwa zikitozwa haziendani na ile biashara.Kutokana na changamoto hiyo tukaona ni vema kutoa mafunzo ya sheria za leseni za biashara kwa maafisa biashara ili kuepukana na hiyo changamoto"alisema Rajab Chambenga

Baadhi ya Maofisa Biashara kutoka halmashauri mikoa mitatu ya Njombe,Iringa na Ruvuma akiwemo Majaliwa Hamis Kassim na Msafiri Mtandi wanasema elimu wanayopatiwa Inawaongezea maarifa ya kwenda kuwaelimisha wafanyabiashara katika maeneo yao na kwamba baadhi yao wamekuwa wakishindwa kutambua umuhimu wa kumiliki leseni katika biashara zao.

"Kukutana kwetu na kupewa mafunzo ya pamoja tunaamini tutaenda kuboresha utoaji wa leseni kwa wafanyabiashara wetu na kikubwa tuelewe uchumi wa nchi unajengwa kwa sehemukubwa na wajasiriamali pamoja na wafanyabiashara na wafannyabaishara ili wafanye biashara vizuri wanahitaji kupatale leseni"alisema Msafiri Mtandi

Lusietha Mapunda ni afisa biashara wa halmashauri ya wilaya ya Ludewa Mkoani Njombe amesema baadhi ya wafanyabiashara wamekuwa wakaidi kujitokeza kuomba leseni hadi pale wanapopatwa na madhira.

"Niwaombe wafanyabiashara wajitokeze kuchukua leseni kwa maana kile ni kibali unapohitaji kufungua biashara,sisi tupo kwa ajili ya kuwalea na kuwashauri wafanyabiashara katika shughuli zao"alisema Lusietha Mapunda

Mkakati wa serikali ni kuhakikisha wafanyabiashara wanafanya shughuli zao kwa mujibu wa sheria pamoja na kupunguza bugudha baina ya wafanyabiashara na serikali yao.
Abbas Kotema afisa leseni mwandamizi kutoka BRELA akieleza majukumu ya BRELA na madhumuni ya semina kwa maafisa ikiwa ni pamoja na kuangali vifungu vya sheria na njia za kuboresha ili kuwasaidia wafanyabiashara.




Baadhi ya maafisa biashara wa mikoa mitatu ya nyanda za juu kuini wakiwa katika semina ya siku ya tatu wakijifunza sheria ya leseni za biashara ili kufanya kazi na wafanyabisahara katika maeneo yao kwa kufuata utaratibu na sheria.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad