HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, April 12, 2021

TAKUKURU MANYARA YAREJESHA SHAMBA LA URITHI

Na Mwandishi wetu, Babati

TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa TAKUKURU Mkoani Manyara, imerejesha shamba la mjane wa Profesa Joshua Doriye aliyetaka kudhulumiwa na viongozi wa Kijiji cha Getanuwas Wilayani Hanang’.

Mkuu wa TAKUKURU Mkoani Manyara, Holle Joseph Makungu akizungumza na waandishi wa habari mjini Babati amesema mjane huyo wa Profesa Doriye aliyekuwa Katibu Mkuu ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji kwa wakati huo, alitaka kudhulumiwa shamba hilo na Mwenyekiti wa kijiji hicho Adam Maulid Mwanga.

Makungu amesema Profesa Doriye katika uhai wake kama ilivyo kwa watanzania wengine alikuwa na haki ya kumiliki mali ikiwa ni haki ya kikatiba iliyoainishwa chini ya ibara ya 24 (1) (2) katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 ikisomeka pamoja na madhumuni ya kutungwa kwa sheria ya kuzuia na kupambana na rushwa namba 11/2007.

Amesema kati ya mali alizofanikiwa kumiliki wakati wa uhai wake ni pamoja na shamba lilillopo kijiji cha Getanuwas wilayani Hanang’ mkoani Manyara.

“Mwaka 2019 mjane wa marehemu huyo Profesa Doriye wakati akishuhulikia shughuli ya mirathi Mwenyekiti wa Serikali ya Kijiji cha Getanuwas Adam Maulid Mwangu kwa kushirikiana na watu wengine waliokuwa na nia ovu ya kutwaa shamba hilo alikataa kutambua umiliki wa ardhi wa marehemu Profesa Doriye katika kjiji hicho hivyo kukwamisha ufungaji wa shauri la mirathi namba 47/2019 uliokuwa ukiendelea mahakama ya mwanzo Kawe.

“Baada ya Mwenyekiti huyo kutotambua umiliki huo mjane aliwasilisha malalamiko yake TAKUKURU na tukaanzisha uchunguzi wa kina wa mjane huyo wa Profesa Doriye,” amesema Makungu.

Amesema uchunguzi wao umebaini kwamba marehemu Profesa Doriye alipewa shamba hilo na serikali ya kijiji cha Getanuwas tangu mwaka 1978 na umiliki wake haukuwahi kuangaliwa na mtu yeyote katika kipindi chochote na nyaraka zote kuhusu umiliki zipo na viongozi wa wakati huo wamethibitisha pasipo shaka umiliki wa shamba hilo kwa Profesa Doriye.

“Tulipomuhoji Mwenyekiti huyo wa kijiji wa sasa Adam Maulid Mwangu kupitia ushahidi wa nyaraka mbalimbali alionyesha kujutia kitendo alichomfanyia mjane, aliomba msamaha akieleza kwamba yeye hakuwahi kuziona nyaraka za umiliki wa shamba hilo na hivyo kukiri kumtambua mmiliki na kukiri kutomsumbua tena mjane na wanufaika wa shamba hilo,” amesema Makungu.

Amesema shamba hilo pamoja na nyaraka walikabidhi rasmi kwa mjane wa marehemu ili aweze kuendelea na utaratibu wa kufunga mirathi hiyo katika mahakama ya mwanzo Kawe.

“Tunawaonya baadhi ya wenyeviti wa vijiji wachache wa aina ya Adam Maulid Mwangu kuwa hawakuchaguliwa kwenda kutegua maamuzi halali yaliyoamuliwa na vikao halali vya serikali za vijiji zilizotangulia hasa katika eneo hili la ardhi, kufanya hivyo kama alivyofanya Mwangu kwa nia ya kujipatia ardhi ni matumizi mabaya ya madaraka na kinyume cha kifungu cha 31 sheria ya kuzuia na kupambana na rushwa namba 11/2017 na watakaobainika sharia itachukua mkondo wake,” amesema Makungu.  

Alitumia nafasi hiyo kuwafahamisha wana Manyara na watanzania kwa ujumla kwamba ukisoma madhumuni ya kutungwa kwa sheria ya kuzuia na kupamba na rushwa namba 11/2007 yameainishwa kwamba sheria hiyo imetungwa ili kuhakikisha kuwa wanaondokana na rushwa na dhuluma za aina zote na sheria hiyo imetungwa ili kuhakikisha kuwa kila mmoja anakuwa na haki ya kumiliki mali aliyoipata kwa njia halali na umiliki huo utalindwa kwa msingi wa sheria kama ilivyofanyika kwa mali ya marehemu Profesa Doriye.

“Hivyo tunaendelea kuchukua hatua kwa wale wachache ambao kwa tamaa zao wanagombea nafasi za kisiasa zikiwemo uenyekiti wa mtaa na vijiji kwa nia ovu ya kwenda kupora mali za wananchi zilizopatikana kwa njia halali,’’ amesema Makungu.
Mkuu wa TAKUKURU Mkoani Manyara, Holle Joseph Makungu akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake mjini Babati.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad