Waziri
wa Viwanda na Biashara Prof. Kitila Mkumbo (Mb) ametoa maelekezo kwa
ajili ya kuimarisha sekta ya viwanda na biashara ili sekta hizo
zichangie kwa kiwango kikubwa katika ukuaji wa uchumi na kutekeleza
malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025, Mpango wa Taifa wa
Maendeleo wa III wa miaka mitano 2021/22 – 2025/26, Ilani ya CCM ya
uchaguzi 2020 na Maelekezo ya Serikali ya Awamu ya Sita na Ushauri na
maoni maelekezo ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika
kukuza uchumi wa Viwanda nchini.
Profesa Mkumbo ametoa
maelekezo hayo alipokutana na menejimenti ya wizara na wakuu wa taasisi
zilizochini ya wizara hiyo kwa lengo la kutoa mwelekeo wa utekelezaji
wa majukumu ya Wizara katika kikao kilichofanyika tarehe 10/04/2021
katika ukumbi wa Chuo cha Biashara jijini Dodoma.
Akiongea
katika kikao hicho, Waziri alisema Dira ya Maendeleo ya Mwaka 2025
inalenga kuona Tanzania inahitimu na kuondokana kuwa nchi masikini
inayotegemea kilimo na uchumi wa uzalishaji duni na kufikia uchumi wa
kati ifikapo mwaka 2025 ambapo wananchi wengi wajihusihe na kilimo cha
kisasa kinachofunganishwa na viwanda na huduma. Hivyo alisisitiza kuwa
ili kufikia dira hii wizara hiyo ina nafasi na mchango mkubwa katika
kufanikisha azma hiyo.
“ Uchambuzi wa maudhui ya Dira ya Taifa ya
Maendeleo 2025 na Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa III wa miaka mitano
2021/22 – 2025/26 unaonesha wazi kabisa nafasi ya Sekta ya Viwanda na
Biashara…sisi kama Wizara tunatarajiwa kutoa mchango karibu kwa kila
eneo la matokeo tarajiwa.”
Alisema pia katika Mpango wa Taifa wa
Maendeleo wa III wa miaka mitano 2021/22 – 2025/26, malengo sita kati ya
malengo mahsusi 12 yanahusu sekta ya viwanda na biashara, kati ya
vipaumbele vitano vya mpango huo vitatu vinahusu wizara hiyo, katika
Sekta 30 za mpango huo Sekta 6 zinahusu Wizara na katika hatua 156
hatua 54 zinahusu Wizara ya Viwanda na Biashara.
“Taasisi
zote zilizochini ya Wizara ya Viwanda zinamchango mkubwa katika
utekelezaji wa majukumu ya Wizara ili kufikia malengo ya Dira ya Taifa
ya Maendeleo 2025 na Mpango wa taifa wa Maendeleo wa III wa miaka mitano
2021/22 – 2025/26, malengo ya Ilani ya Uchaguzi ya CCM 2020, Maelekezo
ya Serikali awamu ya sita. Hivyo nawasihi muendelee kufanya kazi kwa
mujibu wa Sheria Kanuni na taratibu zinazosimamia taasisi zenu katika
utoaji wa huduma bora kwa wananchi na si kuwa kikwazo”
Hata
hivyo, Profesa Mkumbo alisema hakusudii kutumia muda mwingi katika
kutunga Sera, Sheria na mikakati na kuwa yeye analenga katika
utekelezaji na kuona matokeo ya utekelezaji huo kwa kuchochea ukuaji wa
haraka wa Sekta ya Viwanda na Biashara.
Pia aliwataka wataalamu
wa Idara ya Sera na Mipango ya Wizara kusimamia uhuishaji wa nyaraka
mbalimbali za kisera na sheria ili ziende na wakati na kuakisi maudhui
ya Mpango wa tatu wa Maendeleo na maono ya Rais wa Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan.
Akitoa maelekezo mahususi
kwa upande wa sekta ya viwanda, Profesa Mkumbo alitaka kuwa bayana na
dhana na aina ya viwanda tunavyotaka kuviendeleza hapa nchini, kuwa na
kanzi data ya kisasa ya viwanda. Pia alielekeza katika kupima maendeleo
ya viwanda kwa kuzingatia kiwango cha uzalishaji na ajira, kuweka
mazingira namasharti rahisi katika kukuza na kuchochea viwanda vidogo
vidogo vinavyotumia teknolojia rahisi na ya kisasa na vilivyojikita
vijijini na mijini,
Profesa Mkumbo pia alisisitiza mkazo katika
kuwatambua, kuwawezesha na kuwahudumia wawekezaji katika viwanda vikubwa
na vyenye tija katika uchumi na kuhuisha Mkakati wa Viwanda nchini,
ikiwemo dhana ya EPZ na SEZ. Alisema pia kusimamia kwa karibu miradi ya
kielelezo iliyopo katika Mpango wa Maendeleo wa Tatu wa Taifa ambayo ni
mradi wa Chuma wa Mchuchuma na Liganga, Magadi Soda wa Engaruka, ujenzi
wa Kiwanda cha Sukari-Mkulazi na kanda Maalum za Uchumi na Maeneo Maalum
ya Uwekezaji
Profesa Mkumbo alisema pia kuimarisha utafiti na
matumizi yake katika maendeleo ya viwanda, ikiwemo kuwa na ushirikiano
wa karibu na taasisi za utafiti na elimu ya juu na kupanua na kuboresha
mahusiano na ushirikiano na taasisi za sekta binafsi.
“ Pia
kuimarisha ushirikiano na OR-TAMISEMI katika maendeleo ya viwanda vidogo
vidogo, tunataka kuona uwezekano wa kuwaongeza majukumu maafisa
biashara wa Halmashauri ili pia wasimamie viwanda vidogo vidogo katika
maeneo yao kwa kushirikiana na SIDO.”
Kwa upande wa sekta ya
biashara, Profesa Mkumbo aliweka msisitiza katika suala la kujenga imani
kwa wafanyabiashara kupitia, uwazi na mawasiliano chanya ya mara kwa
mara. “Tunataka tunapokutana na wafanyabiashara tufanye mazungumzo yenye
tija ya kubadilisha mikakati ya kukuza biashara na masoko, badala
mikutano hiyo kutumika tu kama jukwaa la kusikiliza malalamiko ya
wafanyabiashara.”
Alisema pia kuendelea kuzipitia kanuni za
mamlaka za udhibiti zinazoonekana kukwamisha biashara, kuchochea na
kuhamasisha tabia ya kujali wateja miongoni mwa watendaji wa Serikali
wanaohudumia sekta mbalimbali za biashara.
Profesa Mkumbo alisema
pia kuipitia na kufanya tathimini ya utekelezaji wa “Blue Print” kwa
lengo la kuona maeneo ambayo bado hayajatekelezwa na kusimamia
utekelezaji wake kikamilifu na kwa haraka, kushirikiana na OR-TAMISEMI,
kuchambua na kuchakata kwa umakini maoni ya wabunge na wadau wengine
kuhusu haja ya kuwa na Mfuko mmoja wa Mtaji kwa ajili ya wajasiriamali
na wafanya biashara wadogo.
Alisema pia kuratibu na kusimamia
uanzishwaji wa sera ya maendeleo ya sekta binafsi, ikiwemo biashara
ndogo zinahitaji upendeleo maalumu ili kukua na kuweka msisitizo wa
pekee katika kutafuta masoko ya bidhaa za Tanzania ndani ya nchi na nje
ya nchi na kuratibu na kusimamia uanzishwaji wa maeneo maalum ya
kibiashara hususani kwa maeneo ya mipakani. Pia, kuona namna ya
kuimarisha eneo maalumu la kibiashara la Kariakoo ambalo kihistoria
limekuwa likifanya vizuri na kuwalinda walaji.
Aidha, Profesa
Mkumbo amesisitiza haja ya watendaji wa wizara na wataasisi kubadilisha
mtizamo katika utendaji kazi na kuwa na “corporate thinking” na tabia ya
kujali wateja kwa kuzingatia kuwa wadau tunaowahudumia ni
wafanyabiashara.
Pia amewalekeleza wataalamu wa wizara hiyo
kuhakikisha wanatoa ushauri wa kitaalamu wenye ushahidi wa kisayansi na
ameahidi atatoa ushirikiano mkubwa kwa wafanyabiashara
Aidha,
Profesa Mkubwa alisikiliza maoni na changamoto mbalimbali zinazozikabili
taasisi hizo kutoka kwa Wakuu wa Taasisi kutoka TBS, WMA, BRELA,
TANTRADE, SIDO, NDC, EPZA, FCC, FCT, WRRB, TIRDO, CAMARTEC, TEMDO na CBE
na kuahidi kuzitatua.
No comments:
Post a Comment