Makamu
wa Rais, Samia Suluhu Hassan amesema kuwa katika kipindi cha miaka
mitano iliyopita Mkoa wa Tanga umepaokea jumla ya Sh bilioni 73 na
milioni 500 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya elimu.
Makamu
wa Rais amesema hayo Wilayani Korogwe Mkoani Tanga wakati akizungumza
na wananchi katika Mkutano wa hadhara mara baada ya kuweka jiwe la
msingi la Ujenzi wa Chuo cha VETA Korogwe ambapo amesema ahadi ya
Serikali ni kuendelea kuwasomesha watoto wa kitanzania kuanzia darasa
la kwanza hadi kidato cha nne bila malipo pamoja na kujenga shule za
sekondari, Vyuo vya Ufundi na Vyuo Vikuu vya kutosha.
Amesema
ameridhishwa na miradi ya Serikali inayotokelezwa katika mkoa wa Tanga
ikiwepo ujenzi wa VETA mpya katika halmashauri ya Korogwe na kutaka
ikamilike kwa wakati ili iweze kutoa elimu na ujuzi kwa vijana katika
Mkoa wa Tanga.
"Tanga inakua kwa viwanda vinavyojengwa na
vitahitaji wataalamu, hivyo VETA Korogwe ikikamilika ichukue vijana ili
tupate wataalamu watakaofanya kazi kwenye viwanda,"amesisitiza Makamu wa
Rais Mama Samia Suluhu Hassa .
Nae Waziri wa Elimu Sayansi na
Teknolojia Prof Joyce Ndalichako amesema Chuo cha Ufundi VETA Korogwe
ni moja kati ya Vyuo vya vya ufundi 25 vinavyojengwa katika halmashauri
mbalimbali nchini kupitia Mradi wa Kukuza Stadi za Ujuzi na Kazi
ambapo Serikali ilitenga Sh bilioni 40 kwa ajili ya ujenzi wa vyuo hivyo
na kwamba ujenzi wake unasimamiwa na Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya
Ufundi Stadi VETA.
Amesema sambamba na kujenga VETA hizo bado
zipo VETA nne ambazo zinajengwa kupitia Halmashauri ambazo ni Ruangwa,
Kasulu Kongwa na Nyasa na kufanya VETA zinazojengwa kufikia 29 na kwamba
zitakuwa zimekamilika kufikia Juni 2021 na kuanza kudahili.
"Baada
ya VETA hizi kukamilika, Mwezi Julai 2021 tunatarajia kudahili
wanafunzi ambapo tutaongeza udahili wa wanafunzi elfu 24 mia sita na
hamsini," Amesema Waziri Ndalichako.
Kwa upande wake Mkuu wa
Wilaya ya Korogwe, Kissa Gwakisa Kasongwa amesema wanaishukuru Serikali
kwa kuwapatia Chuo cha Ufundi VETA Korogwe kwa kuwa kitataoa fursa kwa
vijana wa Halmashauri ya Korogwe na Tanga kwa ujumla kupata ujuzi na
Maarifa.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa VETA Dk Pancras
Bujulu amesema ujenzi wa VETA Korogwe umefikia asilimia 65 ambapo
mpaka kukamilika utagharimu Sh bilioni 1 na milioni 600.
Ameongeza
kuwa mradi utakapokamilika mwezi Mei 2021 Chuo kitakuwa na uwezo wa
kudahili jumla ya wanafunzi 840 kati yao 240 ni wa kozi za muda mrefu
na 600 wa kozi za muda mfupi kati ya miezi mitatu na sita.
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi Dkt. Pancras Bujulu akitoa ufafanuzi kwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan kuhusu ujenzi wa VETA Korogwe mkoani Tanga.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akiweka jiwe la Msingi katika Chuo cha Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi Korogwe kilichopo Mkoani Tanga. Kushoto ni Waziri Wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako.Baadhi ya wakazi wa Halmashauri wa Wilaya ya Korogwe mkoani Tanga wakimsikiliza Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan (hayupo pichani)alipokuwa akizungumza nao Machi 15, 2021.
Waziri Wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako akizungumza na wananchi wa Halmashauri ya Wilaya ya Korogwe, (hawapo pichani) mkoani Tanga.
No comments:
Post a Comment