HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, March 16, 2021

Dkt. Kalemani azindua rasmi kitaifa, REA III mzunguko wa Pili

Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani(katikati) akiweka jiwe la msingi kuashiria uzinduzi rasmi wa kitaifa, mradi wa usambazaji wa Umeme Vijijini, Awamu ya Tatu, Mzunguko wa Pili, uliofanyika, Machi 15, 2021 katika kijiji cha Ugaka wilayani Igunga mkoani Tabora.

Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani(katikati) akikata utepe kuashiria uzinduzi rasmi wa kitaifa, mradi wa usambazaji wa Umeme Vijijini, Awamu ya Tatu, Mzunguko wa Pili, uliofanyika, Machi 15, 2021 katika kijiji cha Ugaka wilayani Igunga mkoani Tabora.

Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani akizungumza na wanakijiji wa Ugaka wilayani Igunga mkoani Tabora (hawapo pichani) wakati wa ziara ya uzinduzi rasmi wa kitaifa, wa mradi wa usambazaji wa Umeme Vijijini, Awamu ya Tatu, Mzunguko wa Pili, uliofanyika, Machi 15, 2021

 

Naibu Waziri wa Nishati, Wakili Stephen Byabato ( kushoto) akibadilishana mawazo na Mbunge wa Manonga, Saif Gulamali ( kulia) wakati wa ziara ya uzinduzi rasmi wa kitaifa, wa mradi wa usambazaji wa Umeme Vijijini, Awamu ya Tatu, Mzunguko wa Pili, uliofanyika, Machi 15, 2021 katika kijiji cha Ugaka wilayani Igunga mkoani Tabora.

Waziri wa Nishati, Dkt.Medard Kalemani akikabidhi cheti kwa Mhandisi Alistidia Kashemeza akiwa ni miongoni mwa Meneja wa Kanda, Mkoa na Wilaya Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), na Wakala wa Nishati Vijijini (REA), waliofanya kazi vizuri ya kusimamia mradi wa usambazaji wa umeme vijiji katika mradi uliotangulia, wa pili kulia ni Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Nishati, mhandisi Leonard Masanja. 

Baadhi ya wanafunzi wa shule ya msingi katika Kijiji cha Ugaka wakiwa wamenyoosha juu jarida linalochapisha habari za Wakala wa Nishati Vijijini( REA) kufurahia uzinduzi rasmi wa kitaifa wa mradi wa usambazaji umeme vijijini , Awamu ya Tatu, Mzunguko wa Pili, uliofanyika, Machi 15, 2021, katika kijiji hicho wilayani Igunga mkoani Tabora

======    =======   ======   ========

 Na Zuena Msuya, Tabora

Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani amezindua rasmi kitaifa usambazaji wa Umeme Vijijini, Awamu ya Tatu, Mzunguko wa Pili utakaokamilisha usambazaji wa umeme katika Vijiji vyote 1974 vilivyosalia nchini.

Uzinduzi huo wa Kitaifa ulifanyika katika Kijiji cha Ugaka, Wilayani Igunga Mkoani Tabora, Machi 15, 2021.

Dkt.Kalamani alisema kuwa mradi huo utagharimu shilingi Trilioni 1.24 za kitanzania na utatekelezwa kwa kipindi cha miezi 18 kuanzia sasa katika mikoa yote nchini.

Pamoja na mambo mengine, Dkt.Kalemani alisema kuwa kila wilaya itakuwa inapewa mkandarasi wake kutekeleza mradi huo ili kukamilisha kazi hiyo kwa wakati, tofauti na ilivyokuwa katika miradi iliyotangulia ambapo mkandarasi alikuwa akipewa zaidi ya mkoa mmoja kufanya kazi hiyo jambo ambalo lilichangia kusuasua na kutokamilika kwa wakati kwa mradi.

Alisema kuwa kwamantiki hiyo,hakuna kuongeza muda wa ziada   kwa mkandarasi yeyote atayeshindwa ama kuchelewa kukamilisha mradi huo kwa muda uliopangwa,na atayeshindwa kukamilisha mradi huo kama mkataba unavyoelekeza atafutiwa mkataba wake na kufikishwa mahakamani kwa mujibu wa sharia.

“Kwa sasa hakuna kuongeza muda kwa mkandarasi yeyote atayechelewesha mradi, tutachukuwa hatua za kisheria kwa mujibu wa mkataba, ikiwemo kufuta mkataba wa mkandarasi na kumfikisha mahakamani, tumeamua kutoa mkandarasi mmoja kwa kila wilaya hiii yote ni kuhakikisha kazi hii inakamilika kwa wakati ndani ya miezi 18, tutakuwa tumemaliza kusambaza umeme katika vijiji vyote 1974 vilivyosalia nchi nzima", alisema Dkt.Kalemani

Aliendelea kuwasisitiza wananchi kulipia gharama ya shilingi 27,000 tu katika vijiji na mitaa, na kamwe wasikubali kurubuniwa maafisa wasio waaminifu pamoja na vishoka watakaotaka kuwatoza gharama kubwa zaidi.

Pia wananchi hao waendelee kutandaza nyaya katika nyumba zao ili kujiweka tayari kuunganishiwa Umeme.

Aidha aliwataka wakandarasi hao kujitambulisha kwa uongozi wa vijiji, wilaya na mkoa kabla ya kuanza kazi na kuwaeleza viongozi hao ratiba za kazi zao kwa eneo husika ili kuwa rahisi viongozi hao kufuatilia kwa karibu utekelezaji wa mradi huo.

Alisitiza kuwa wakandarasi hao wahakishe kuwa kazi zote zisizohitaji taaluma maalum zipewe kwa wakazi wa eneo husika na walio karibu na eneo hilo ili kunufaika na uwepo wa mradi huo.

Katika kuboresha huduma ya upatikanaji wa umeme muda wote katika wilaya ya Igunga, Dkt.Kalemani aliahidi kujenga kituo kidogo cha kupoza umeme katika wilaya hiyo ili kupunguza tatizo la umeme kutokuwa na nguvu linalosababishwa na Umeme huo kutoka umbali mrefu.

Katika hatua nyingine, Dkt.Kalemani alifanya mkutano na wanakijiji wa kijiji cha Isanzu, wilayani Nzega mkoani humo na kuwaeleza kuwa mkandarasi wa kutekeleza mradi wa kusambaza umeme katika wilaya hiyo amekwisha patika na muda wowote ataanza kufanya kazi kwakuwa fedha ya kutekeleza mradi huo ipo. 

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Philemon Sengati aliwataka wananchi wa mkoa huo hasa katika vijiji ambavyo havijafikiwa na mradi huo kuchangamkia fursa ya kuweka umeme katika nyumba zao kwa kwamba serikali imetenga fedha nyingi kuhakikisha umeme unawafika katika kila kijiji.

Sengati aliwaeleza kuwa lengo la serikali ni kufikisha umeme kwa kila mtanzania ili atumie Umeme huo katika kufanya shughuli mbalimbali za maendeleo na pia kutunza mazingira kwa kuwa Umeme ukitumika kama nishati ya kupikia, utasaidia kuhifadhi mazingira kwa kutunza misitu nchini kwa kuepusha ukataji wa kuni na kuchoma mkaa.

Mkuu wa mkoa huo, amewataka wawekezaji kwenda kuwekeza katika mkoa wa Tabora kwa kuwa una fursa nyingi za uwekezaji kutoka na shughuli mbalimbali za Kilimo,ufugaji pamoja na uchimbani madini kwa kuwa kuna Umeme wa kutosha.

Na katika uzinduzi huo, Dkt. Kalemani alitumia fursa hiyo kukabidhi vyeti vya kutambua kazi nzuri ya Mameneja na Wakuu wa Kanda, Mkoa na Wilaya Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), na Wakala wa Nishati Vijijini (REA),waliofanya kazi vizuri ya kusimamia mradi wa usambazaji wa umeme vijiji na kuunganisha wateja kwa mradi uliotangulia.  




No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad