HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, February 1, 2021

Mico Halal International kusimamia machinjio yote nchini Inapima nyama kuwahakikishia usalama walaji



Na Mwandishi Wetu

TAASISI ya Mico Halal International Bureau imeleta neema mpya kwa walaji wa nyama ambapo sasa itasimamia machinjio yote nchini kuhakikisha nyama inayopatikana inakuwa salama kwa afya.

Hayo yamesemwa jijini Dar es Salaam na Katibu wa taasisi hiyo, Shehe Jumanne Kasonso, wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu kuanza kazi kwa taasisi hiyo Januari mwaka huu.

Amesema MICO imepewa kibali na Baraza la Kiislamu Tanzania (Bakwata) kwaajili ya kusimamia machinjio hayo kwa kupima nyama inayopatikana kuwa safi na salama kwa matumizi ya binadamu na kutoa vibali kwa wale wanaozisafirisha nje ya nchi.

Shehe Kasonso amesema mbali na nyama taasisi hiyo itasimamia pia viwango vya vyakula na vinywaji kuhakikisha watanzania wanapata huduma yenye ubora wa hali ya juu na hawapati madhara kiafya.

“Sisi ni wakala wa Bakwata tunafanya kazi chini yake na mbali na kupima ubora wa nyama MICO inasimamia na kutoa mafunzo juu ya uchinjaji bora halali pamoja na kutoa mafunzo na ithibati kwa nyama halali zinazosafirishwa nje ya nchi,” alisema

Ametaja baadhi ya wanyama ambao taasisi hiyo imekuwa ikisimamia kuhakikisha nyama yake inakuwa na ubora na salama kwa matumizi kuwa ni mbuzi, ng’ombe , kondoo na ndege wanaoliwa.

Shehe Kasonso amesema taasisi hiyo imenunua mashine maalum na za kisasa ambazo zitatumika kwaajili ya kupima nyama kwa matumizi ya binadamu ili kujua kama inamadhara kiafya au la.

“Mtanzania jali na ipende afya yako hivyo unapotaka huduma ya kupimiwa nyama wasilianana sisi tuko Magomeni Mapipa jengo la Diamond Trust tutakuhudumia kuhakikisha unapata nyama ilisayo safi na isiyo na magonjwa,” amesema Shehe Kasonso

Aidha ametoa wito kwa wananchi kuhakikisha wanakula nyama iliyopimwa isiyo na magonjwa kama zile ambazo zimechomwa sindano za zandigana na zinginezo ambazo mnyama husika hatakiwi kuliwa ndani ya siku 30 ili kupisha dawa hiyo itoke.

“Kuna dawa ambazo mnyama akichomwa nyama yake haitakiwi kuliwa ndani ya siku 30 na maziwa yake kama anakamuliwa yasinywewe mpaka zipite siku saba sasa watu wengine wasiowaaminifu wanaweza kuyaingiza sokoni kazi yetu itakuwa kuyapima kuona kama yanafaa na kama hayafai yanatolewa,” ameongeza

Amesema tangu taasisi hiyo ianze kutoa huduma mwezi Januari mwaka huu mwitikio umekuwa mkubwa kwani watu mbalimbali wamekuwa wakifika kwaaajili ya kuchukua vibali kutoka MICO kwaajili ya kusafirisha nyama hiyo nje ya nchi.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad