TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa TAKUKURU Mkoani Manyara, imemtaka Mkurugenzi wa kampuni ya Farm Green Implement (T) Ltd, Dunga Othman Omar kurudisha shilingi milioni 33.2 za wakulima wawili wa Wilayani Hanang' alizochukua ili awanunulie matrekta mawili.
Akizungumza
na waandishi wa habari Mjini Babati jana, Mkuu wa TAKUKURU mkoani
Manyara, Holle Joseph amesema Dunga anapaswa kurejesha fedha hizo kabla
ya Novemba 18 ili ziweze kurejeshwa kwa wakulima hao wawili wa Wilaya ya
Hanang'.
Makungu
amesema mkurugenzi wa kampuni hiyo Dunga alipewa fedha hizo na wakulima
hao wawili ili awanunulie trekta ila fedha hizo zikaingizwa kwenye
akaunti yake binafsi badala ya akaunti ya kampuni.
Amesema
walipata malalamiko kwa wakulima wawili wa wilayani Hanang' walitoa
shilingi milioni 17 na shilingi milioni 16.2 mwaka 2016 kuweka kwenye
akaunti yake binafsi ya Dunga ili wanunuliwe matrekta mawili ila hadi
sasa hawajapatiwa.
"Katika
uchunguzi wetu Takukuru mkoani Manyara imebaini kuwa Dunga alielekeza
fedha hizo kwenye akaunti yake binafsi badala ya kampuni jambo
linaloashiria nia ovu na kwa sheria zilizopo anaweza kushtakiwa kwa
makosa ya jinai yakiwemo ya kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu au
kutakatisha fedha hizo," amesema Makungu.
Amesema
Oktoba 25 mwaka huu Rais John Magufuli akiwa kwenye uwanja wa Kwaraa
mjini Babati moja ya ahadi zake ilikuwa kuhakikisha rushwa na dhuluma
zinakomeshwa na ikatoa mwamko kwa wana Manyara waliodhulumiwa miaka ya
nyuma kudai haki zao.
"Rais
Magufuli katika awamu yake ya pili ya uongozi wa nchi hii aliahidi
atahakikisha rushwa na dhuluma zinatokomezwa na sisi tunatekeleza hilo
kwa kufanyia kazi taarifa hii hata kama imetokea muda mrefu kwani jinai
haifi hadi mtenda jinai atangulie mbele ya haki," amesema Makungu.
Amemtaka
Dunga popote alipo awasilishe fedha hizo kwa mkuu wa Takukuru kabla ya
Novemba 18 ili ziweze kurejeshwa kwa wakulima hao na kushindwa
kutekeleza agizo hilo bila shuruti kutalazimisha kuchukua hatua zaidi
kwa misingi ya sheria zinazotawala eneo hilo.
"Ni
rai yetu iwapo kuna wakulima wengine ambao fedha zao zilichukuliwa na
Dunga kwa udanganyifu wakuletewa matrekta na hawakuletewa wawasilishe
malalamiko yao kupitia namba yetu ya dharura 113 au simu ya mkononi
0738150124 ili yashughulikiwe kwa pamoja," amesema Makungu.
Mkuu wa TAKUKURU Mkoani Manyara, Holle Joseph Makungu akizungumza na waandishi wa habari.
No comments:
Post a Comment