HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Saturday, September 26, 2020

WIZARA YA FEDHA MSIMAMIZI RASMI WA WANAMIPANGO NCHINI

 

 

Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango na Mlipaji Mkuu wa Serikali, Bw. Doto James, akifunga Kongamano la Wanamipango la Mwaka 2020, ambapo ameahidi Wanamipango (hawapo pichani) kutatua changamoto mbalimbali zinazowakabili wakati wa kutekeleza majukumu yao, jijini Dodoma.

Kamishna wa Mipango ya Kitaifa Wizara ya Fedha na Mipango, Dkt. Nicolaus Shombe, akiahidi utekelezaji wa maadhimio waliyokubaliana kwa Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango na Mlipaji Mkuu wa Serikali, Bw. Doto James, ambaye ni Mlezi wa Wanamipango wote nchini (hayupo pichani), wakati wa kufunga Kongamano la Wanamipango la Mwaka 2020, jijini Dodoma.
Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango na Mlipaji Mkuu wa Serikali, Bw. Doto James, akiteta jambo na Kamishna wa Mipango ya Kitaifa Wizara ya Fedha na Mipango, Dkt. Nicolaus Shombe, wakati wa kufunga Kongamano la Wanamipango la Mwaka 2020, jijini Dodoma.
Meza Kuu ikiongozwa na Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango na Mlipaji Mkuu wa Serikali, Bw. Doto James (katikati), kulia ni Kamishna wa Mipango ya Kitaifa wa Wizara ya Fedha na Mipango Dkt. Nicolaus Shombe na kushoto ni Kaimu Kamishna wa Sera wa Wizara ya Fedha na Mipango, Bw. Wiliam Mhoja, wakifuatilia maoni yaliyokuwa yakitolewa na Wanamipango wakati wa Kongamano la Wanamipango la Mwaka 2020, jijini Dodoma.

Wanamipango wakiendelea kufuatilia kwa karibu hotuba ya Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango na Mlipaji Mkuu wa Serikali, Bw. Doto James, ambaye ni Mlezi wa Wanamipango wote nchini wakati wa kufunga Kongamano la Wanamipango la Mwaka 2020, jijini Dodoma. 
Mkurugenzi wa Sera na Mipango Ofisi ya Rais TAMISEMI, Bw. John Cheo akitoa neno la shukrani kwa niaba ya Wanamipango wakati wa kufunga Kongamano la Wanamipango la Mwaka 2020, jijini Dodoma. 

(Picha na Josephine Majura , WFM – DODOMA). 

********************************** 

Na. Farida Ramadhani na Ivona Tumsime, WFM, Dodoma 

Wizara ya Fedha na Mipango imeanza rasmi kuisimamia Kada ya Wanamipango nchini ili kuwalinda na kuwawezesha kutekeleza majukumu yao ya kupanga na kusimamia miradi mbalimbali ya maendeleo nchini bila kuingiliwa. 

Akizungumza jijini Dodoma wakati wa kufunga Kongamano la Wanamipango la Mwaka 2020, Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango na Mlipaji Mkuu wa Serikali, Bw. Doto James alisema Wizara hiyo imewatambua rasmi Wanamipango kama inavyofanya kwa Wahasibu, Wakaguzi na Wagavi. 

“Tutawawezesha kitaaluma maana nimesikia malalamiko mengi, nimeambiwa katika ngazi ya Halmashauri Wanamipango nikama wametelekezwa, wanaitwa majina mengi yanayowashushia morali ya kazi, kwa hiyo kuanzia sasa hatutokubali hilo litokee kwa Wanamipango”, alisema. 

Bw. James alisema kuwa Wizara itatengeneza namna nzuri ya kuwasiliana na Wanamipango wote nchini kwa ajili ya kutatua changamoto mbalimbali zinazowakabili na itawalinda kwa gharama yoyote wale wote wanaoonewa katika utekelezaji wa majukumu yao kwa mujibu wa sheria. 

Alisema Wizara inaangalia namna ya kutenga Bajeti kwa ajili ya kuwawezesha Wanamipango kutekeleza majukumu yao huku akiwatahadharisha kuwa fedha hizo hizitatolewa kiholela kwa kuwa utatengenezwa utaratibu mzuri wa kuwafikia wote ambao watafuata utaratibu wa matumizi ya fedha hizo katika majukumu yao. 

“Wanamipango lazima ufuatilie kile ulichopanga na utekelezaji wake, kule kwenye utekelezaji ndio kumekuwa na madudu, kitu chakufuatilia kila siku kwa mwaka mtu haendi, wakija wakaguzi kwenye mradi na yeye ndio anaenda, unakuta yeye ni mgeni kwenye mradi wake. Kila kitu hajui, mambo haya hatutokubali yatokee tena”, aliongeza. 

Bw. James aliahidi kuyachukua masuala yote yaliyojitokeza kwenye majadiliano na maazimio yaliyofikiwa katika kongamano hilo kwa kuwa yatasaidia kufanikisha na kuboresha usimamizi wa upangaji na utekelezaji wa sera na mipango ya maendeleo. 

Naye Kamishna wa Mipango ya Kitaifa kutoka Wizara ya Fedha na Mipango, Dkt. Nicolaus Shombe, alisema katika kongamano hilo la siku mbili Wanamipango walipata nafasi ya kujadili mada mbalimbali ikiwemo uandaaji wa Mpango wa Tatu wa Taifa wa Miaka Mitano unaotarajiwa kuanza mwaka 2021/22. 

Alisema walijadili kwa kina kada ya Wanamipango kuhusu umuhimu na mchango wake katika maendeleo ya nchi na changamoto ambazo wanakumbana nazo katika utendaji kazi zao pamoja na kutoa mapendekezo ya kukabiliana nazo. 

Kwa upande wa Mkurugenzi wa Sera na Mipango kutoka Ofisi ya Rais TAMISEMI, Bw. John Cheo ambaye ni miongoni mwa washiriki wa Kongamano hilo ameipongeza Wizara ya Fedha na Mipango kwa kuchukua jukumu la kuwalea Wanamipango kwa kuwa anaamini uamuzi huo utachochea ubunifu katika kupanga mipango mbalimbali ya maendeleo nchini.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad