HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, August 18, 2020

MGALU ATOA AGIZO ZITO KWA WAKANDARASI MRADI WA REA

 

Naibu Waziri wa Nishati, Subira Mgalu,(wa tatu kulia) akikata utepe kuashiria kuwashwa kwa Umeme katika Shule ya Sekondari ya Namonge,kata ya Namonge Wilaya ya Bukombe, Mkoani Geita,Agosti 17,2020(wa nne kulia) ni Mkuu wa Wilaya ya Bukombe Said Nkumba.


Hafsa Omar - Geita


Naibu Waziri wa Nishati, Subira Mgalu, amesema Serikali haitapokea mradi wowote kutoka kwa wakandarasi wanaotekeleza mradi wa REA mpaka pale itakapofanya ukaguzi na kujiridhisha kuwa masharti yote ya mkataba yamezingatiwa.


Ameyasema hayo, Agosti 17,2020, kwa nyakati tofauti wakati akiwa Wilayani Chato na Bukombe, Mkoani Geita, kwenye ziara ya ukaguzi wa kazi za usambazaji umeme vijijini.


Aidha,amesema wakandarasi wa mradi wa REA III mzungo wa kwanza unaotarajiwa kumalizika Septemba 15 mwaka, wakae tayari kwaajili ya ukaguzi na uhakiki kabla ya kukabidhi mradi huo.


“Wakandarasi wote wa miradi ya REA tutawakagua tuone ni namna gani walivyofanya kazi zao kwamba ni kweli idadi ya kilometa walizopewa zote wamezifanyia kazi,tutakagua idadi ya wateja, transfoma, tutakagua kila kitu kama mkataba unavyosema,”alisema Mgalu.


Aidha, wametoa wito kwa wakandarasi hao kutuondoka katika maeneo ya kazi mpaka pale makabidhiano yatakapofanyika kwa mujibu wa taratibu za kisheria zilizowekwa.


Alieleza kuwa, Wizara ya Nishati inajivunia mafanikio yaliyopatika katika kipindi cha miaka mitano ambapo mpaka sasa takribani Taasisi za Umma 15,000 zimeunganishwa na umeme ukilinganisha na hapo awali.


Aliongeza kuwa, Serikali baada ya kuona imefanikiwa katika jitihada za kupeleka umeme vijijini, kwasasa imeamua kuelekeza nguvu za kupeleka umeme kwenye vitongoji ambapo zaidi ya shilingi bilioni 800 zimetengwa kwaajili ya kazi ya usambazaji umeme kwenye vitongoji.


Pia, amewashukuru viongozi wa Wilaya na Mkoa kwa kumsimamia kikamilifu mkandarasi anayetekeleza mradi wa REA mkoani humo.


Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Bukombe Said Nkumba, amesema kuwa atahakikisha anamsimamia kikamilifu mkandarasi wa Mkoa huo, ili aweze kumaliza kufanya kazi zake kwa mujibu wa muda aliopewa na Serikali.


Vilevile, amesema amefurahishwa na dhamira ya Serikali ya kuhakikisha umeme unafika katika Taasisi mbalimbali za Umma ambapo umeme huo utasaidia kuboresha huduma zinazotolewa katika Taasisi hizo.


Naibu waziri, katika ziara yake hiyo, pia aliwasha umeme katika shule ya Msingi Itanga iliyopo katika kijiji cha Itanga, Kata ya Minkoto, Wilaya ya Chato na katika Shule ya Sekondari ya Namonge,kata ya Namonge Wilaya ya Bukombe, na alikagua njia ya kusafirishia umeme katika kijiji cha Kazibizyo, Wilaya ya Bukombe, Mkoani Geita.

Naibu Waziri wa Nishati, Subira Mgalu(mwenye ushungi) Mkuu wa Wilaya ya Bukombe Said Nkumba(mwenye kofia) wakimsikiliza Mhandisi Bakar Abdallah(wa kwanza kulia) wakati walipokuwa kwenye ukaguzi wa njia ya kusafirishia umeme katika kijiji cha Kazibizyo, Wilaya ya Bukombe, Mkoani Geita, Agosti 17,2020.

Naibu Waziri wa Nishati, Subira Mgalu, akizungumza na wananchi(hayapo pichani) wa kijiji cha Namonge, Kata ya Namonge, Wilaya ya Bukombe, Mkoani Geita, kabla ya kuwasha umeme kwenye kijiji hicho,Agosti 17,2020.

Naibu Waziri wa Nishati, Subira Mgalu,akiwasha umeme katika Shule ya Msingi Itanga iliyopo katika kijiji cha Itanga, Kata ya Minkoto, Wilaya ya Chato,Mkoani Geita, Agosti 17,2020.

Naibu Waziri wa Nishati, Subira Mgalu,(Kushoto) Mkuu wa Wilaya ya Chato Mhandisi Charles Kabeho (kulia),wakielekea kwenye darasa nililoandaliwa kwaajili ya kukata utepe katika Shule ya Msingi Itanga iliyopo katika kijiji cha Itanga, Kata ya Minkoto, Wilaya ya Chato,Mkoani Geita, Agosti 17,2020.

Wananchi Pamoja na wanafunzi wa Shule ya Msingi Itanga iliyopo kwenye kijiji cha Itanga,kata ya Minkoto,Wilaya ya Chato, Mkoani Geita,wakimsikiliza Naibu Waziri wa Nishati,Subira Mgalu (hayupo pichani) wakati akiwa kwenye ziara ya ugakuzi wa kazi ya usambazaji umeme vijijini, Agosti 17,2020.



No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad