KATIKA
kuhakikisha Mwaka wa Mtoto sambamba na malengo ya Mkataba wa
utekelezaji wa afua za lishe yanafanikiwa, Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mh.
Joachim Wangabo amewataka Wakurugenzi wa Halmashauri mkoani humo
kuhudhuria vikao vya tathmini ya lishe ngazi ya mkoa ili kuweza kujibu
hoja zinazowakwamisha kufikia malengo ya mkataba huo hasa wakati huu
ambapo nchi inajipanga kufikia uchumi wa juu.
Wangabo amesema kuwa ni dhahiri kuwa lishe bora katika jamii ni
kichocheo cha maendeleo katika nyanja zote za Afya, Kilimo, Elimu,
Biashara, na Uchumi, Hivyo malengo ya maendeleo katika nyanja hizi
yataweza kupatikana endapo athari za lishe duni au utapiamlo
zitakapodhibitiwa.
“Sasa nchi yetu tumeingia kwenye uchumi wa kati, na tuna malengo ya
kufikia uchumi wa juu, sasa hapa tulipo tunaweza tukashindwa kama Watoto
wetu watakuwa na lishe duni, lakini pia itakuwa ngumu sana kufikia
uchumi wa juu, kama huku chini Watoto wetu watakuwa na utapiamlo. Lazima
tupige vita utapiamlo ili malengo yetu, maono yetu ya kitaifa, mikakati
yetu yote, na mambo mengine yafanikiwe,” Alisema.
Mh. Wangabo ameyasema hayo katika kikao cha Tathmini ya hali ya Lishe
Mkoani humo, vikao ambavyo hufanyika mara mbili kwa mwaka katika ngazi
ya mkoa, na mara moja katika ngazi ya kitaifa ambapo Wakuu wa Mikoa,
Makatibu Tawala wa Mikoa pamoja na Waganga wakuu wa mikoa huudhuria ili
kutathmini hali ya lishe Kitaifa.
Aidha, Mh. Wangabo ametaka kikao hicho kirudiwe ili wawepo
wakurugenzi wa halmashauri ambao wanaweza kujibu hoja za kushindwa
kutekeleza makataba huo na si kuwatuma wawakilishi na hivyo kukwepa
kuwajibika jambo litakalosababisha kuwajibishwa endapo hawatahudhuria
kikao hicho cha marudio kitakachofanyika mwishoni mwa mwezi wa Agosti.
“Hatuwezi kwenda tunaaibika kule wenyewe hawapo, ndio maana
umezungumza suala la kuongeza ushiriki kwenye vikao vya kitaifa, lakini
kama hapa hawaji hata kule si watakwepa hivyo hivyo, na hata wakifika
kule wakati tumekwishaaibika tutakuwa hatujafanya kitu kwahiyo ni lazima
tukamatane hapa hapa, kabla ya kwenda huko mbeleni, kabla ya kile kikao
cha mwaka cha nchi nzima ni lazima tuwe tumeshikana vizuri mashati,”
Alisema.
Halikadhalika, Mh. Wangabo amewashukuru wadau wa mradi wa Lishe
Endelevu ambao umekuwa ukitekelezwa katika Mkoa kwa kuwa msaada mkubwa
katika kupambana na Utapiamlo na Udumavu ambao wamechangia Mkoa kufikia
hali ya katikati katika utekelezaji wa mkataba huo.
Kwa upande wake Mganga Mkuu wa Mkoa huo Dkt. Boniface Kasululu wakati
akielezea viashiria vinavyohitaji kuwekewa mikakati ili kufikia malengo
ya mkataba huo amesema kuwa kiasi cha fedha zinazotolewa kwa shughuli
za lishe zinapungua mwaka hadi mwaka huku akitoa mfano wa Mwaka wa fedha
2019/2020 kuwa fedha zilizotengwa kwaajili ya shughuli hizo zilikuwa
Shilingi 357,027,077/= huku fedha iliyotumika ikiwa Shilingi
108,254,259/= ambayo ni sawa na asilimia 30.
“Ni muhimu kwa Wakurugenzi kusimamia utoaji wa fedha zilizotengwa
kwaajili ya shughuli hii ya kutokomeza utapiamlo na udumavu katika mkoa
wetu, pia ni vyema wakurugenzi wakasimamia uwajibikaji wa wataalamu
wanaohusika na uratibu na utekelezaji wa shughuli za lishe pamoja na
kuwawezesha kufanya shughuli za lishe,” Alimalizia.
Kwa mujibu wa Utafiti wa Kidemografia wa Afya na Viashiria vya
Malaria (Demographic Health Survey and Malaria Indicator) wa mwaka
2015/2016 Ulionyesha Mkoa wa Rukwa una asilimia 56.3 ya Udumavu na
Utapiamlo. Na utafiti wa masuala ya Lishe (Tanzania National Nutrition
Survey) Kitaifa wa Mwaka 2018 unaonesha kuwa Mkoa una asilimia 47.9 ya
Watoto walio na Umri chini ya Miaka mitano waliodumaa.
Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo (wa pili toka kushoto)
akimkabidhi Mkuu wa Wilaya ya Sumbwanga Dkt. Khalfan Haule Cheti Maalum
baada ya Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga kuongoza katika viashiria
vya utekelezaji wa Mkataba wa Afua za Lishe katika Mkoa.
No comments:
Post a Comment