HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, September 11, 2019

MISS TANZANIA KATANGAZE VIVUTIO VYA UTALII-MAJALIWA


 Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, akizungumza na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Harrison Mwakyembe, ofisini kwake Mlimwa, jijini Dodoma, Septemba 11.2019.
 Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, akisalimiana na Miss Tanzania 2019, Sylivia Sebastian, nje ya Ofisi ya Waziri Mkuu, Mlimwa, jijini Dodoma, Septemba 11.2019.
 Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, akisalimiana na Miss Tanzania 2019, Sylivia Sebastian, ofisini kwake Mlimwa, jijini Dodoma, Septemba 11.2019, kushoto ni Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Harrison Mwakyembe.
 Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, akisalimiana na Mkurugenzi wa The Look Company Ltd, Basilla Mwanukuzi, ambaye ndiye muandaaji wa shindano la Miss Tanzania 2019, ofisini kwake Mlimwa, jijini Dodoma, Septemba 11.2019.
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, akizungumza na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Harrison Mwakyembe na waandaaji wa shindano la Miss Tanzania 2019 ofisini kwake Mlimwa, jijini Dodoma, Septemba 11.2019. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu).


WAZIRI MKUU, Kassim Majaliwa amemtaka Miss Tanzania 2019, Sylivia Bebwa (19) ahakikishe anakuwa balozi mzuri wa kutangaza vivutio vya utalii vilivyopo nchini, shughuli za maendeleo zinazofanywa na Serikali na aishi kwa kuzingatia utamaduni wa Mtanzania.

“Miss Tanzania lazima awe mbunifu na uelewa mpana katika masuala mbalimbali zikiwemo jitihada zinazofanywa na Serikali katika kuboresha maendeleo ya wananchi kama kuhamasisha elimu hususan kwa watoto wa kike ili waweze kutimiza ndoto zao.”

Waziri Mkuu ameyasema hayo leo (Jumatano, Septemba 11, 2019) wakati alipokutana na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt. Harrison Mwakyembe, waandaaji wa mashindano ya Miss Tanzania, Miss Tanzania na mshindi wa pili na watatu wa shindano hilo, ofini kwa Waziri Mkuu Mlimwa jijini Dodoma.

Amesema Miss Tanzania anatakiwa kutumia fursa hiyo kutangaza vivutio mbalimbali vya utalii vilivyopo nchini, shughuli zinazofanywa na Serikali katika kukuza uchumi pamoja na kuhamasisha wananchi washiriki katika kufanya kazi kwa ajili ya maendeleo yao na Taifa.

Kadhalika, Waziri Mkuu amesema Miss Tanzania pamoja na washiriki wengine wa mashindano hayo wanatakiwa waishi kwa kuzingatia utamaduni wa Mtanzania ikiwemo kuwa na nidhamu katika jamii ili waweze kuwashawishi wengine kushiriki.

Waziri Mkuu amempongeza Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt. Mwakyembe kwa namna anavyoratibu shughuli mbalimbali katika wizara hiyo. “Hata katika sekta ya michezo viwango vimeanza kuonekana.”

Waziri Mkuu amesema Serikali inaunga mkono masuala ya michezo na inapenda kuona viwango vinapanda, hatua ambayo itawawezesha wahusika kufanya vizuri katika mashindano mbalimbali wanayoshiriki.

Kwa upande wake, Waziri Dkt. Mwakyembe amemshukuru Waziri Mkuu kwa kukubali kuonana na ujumbe huo hususani Miss Tanzania ambaye anajiandaa kwenda kushiriki katika mashindano ya Miss World yanayotarajiwa kufanyika London, Uingereza Desemba 14 mwaka huu.

Waziri huyo amesema miaka ya nyuma Serikali haikuridhishwa na namna mashindano hayo yalivyokuwa yakiendeshwa lakini kwa sasa hali ni tofauti na yamekuwa na viwango vya kimataifa. Mashindano hayo kwa sasa yanasimamiwa na aliyekuwa Miss Tanzania 2008, Basilla Mwanukuzi kupitia kampuni ya The Look.

Naye,Mwandaaji wa Mashindano hayo, Basilla Mwanukuzi ametumia fursa hiyo kuishukuru Serikali kwa ushirikiano inaoutoa kwao na pia ameiomba izidi kuwaunga mkono kwa kuwa watatumia mashindano hayo katika kulitangaza Taifa.

Awali, Miss Tanzania 2019, Sylivia ameishukuru Serikali kwa fursa aliyopewa ya kukutana na Waziri Mkuu na alisema kuwa atajitahidi katika kuhakikisha anatekeleza majukumu yake ipasavyo ikiwemo kuiwakilisha Tanzania kwenye mashindano ya Miss World na kwamba anakwenda kutumia lugha ya kiswahili.

“Nimefurahi kwa heshima hii niliyopewa na Serikali ya kukutana na Mheshimiwa Waziri Mkuu, naahidi kwamba niyatekeleza maagizo yote aliyoyatoa ikiwa ni pamoja na kuishi kwa kuzingatia maadili ili wazazi wengine waweze kuwaruhusu watoto wao washiriki katika mashindano haya kwani urembo ni heshima.”

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad