HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, August 6, 2019

WANANCHI SIMIYU WAFURAHIA HUDUMA ZA NHIF NANE NANE

Wananchi katika Mikoa ya Simiyu,  Mara na Shinyanga wamepongeza na kufurahia huduma zinazotolewa na Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) katika maonesho ya Wakulima yanayofanyika Kitaifa mkoani Simiyu.

Huduma hizo ni pamoja na Usajili wa Wanachama,  elimu juu ya huduma za matibabu, upimaji wa afya bure na elimu ya kuepukana na magonjwa yasiyoambukiza.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti,  Mwenyekiti wa Chama cha Msingi cha Sandai Wilayani Bariadi Bw. Elisha Nkubira alisema kuwa huduma zinazotolewa na Mfuko zimewalenga wananchi wote wakiwemo wa kipato kikubwa na kipato kidogo.
 Ofisa Uhusiano wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF),  Grace Michael akimuelekeza jambo mmoja wa wakazi wa Kata ya Nyakabindi, Bariadi mkoani Simiyu, waliojitokeza kupima afya zao katika Banda la NHIF, kwenye maonyesho ya Nane Nane, yanayoendelea Mkoani Simiyu.

"Huu Mfuko unafanya kazi kubwa sana na hizi huduma ambazo wanazitoa kwenye viwanja hivi hakika ni za mfano wa kuigwa na zimelenga kutusaidia Sisi wananchi ili tujue hali za Afya zetu na kuweza kujikinga na maradhi," alisema Bw. Nkubira.

Naye Mkazi wa Bunda Bw. Lameck Mwita ambaye pia ni mwanachama wa Mfuko alitoa wito kwa wananchi wengine kuchukua hatua ya kujiunga na huduma za NHIF ili kuwa na uhakika wa kupata matibabu wakati wote.
 Sehemi ya wakazi wa mkoa wa Simiyu, wakipima afya zao katika Banda la NHIF, kwenye maonyesho ya Nane Nane, yanayoendelea Mkoani Simiyu.

Alisema kuwa kitendo cha familia kuwa na kadi za matibabu za NHIF ni kinga kubwa ya kuepukana na umasikini kutokana na ukweli kwamba maradhi huja bila taarifa na gharama zake ni kubwa.

Naye Ofisa Uhusiano wa Mfuko,  Grace Michael aliwaomba wananchi kutumia fursa hii kutembelea banda la NHIF katika viwanja vya Nyakabindi ili kupata huduma lakini pia kujiunga na Mfuko kupitia makundi mbalimbali yakiwemo ya Toto Afya Kadi, Ushirika Afya, Mwanachama Binafsi na mengine.
"Mbali na hapa NHIF inashiriki pia katika Maonesho ya Nane Nane Kikanda katika mikoa ya Arusha,  Mbeya, Mwanza, Lindi na Morogoro hivyo wananchi wafike na wapate huduma," alisema Grace Michael.



No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad