HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Sunday, August 4, 2019

TIGO YAZINDUA MTANDAO WA 3G PANGANI, TANGA

Na Mwandishi Wetu.

Kampuni inayoongoza katika maisha ya kidigitali nchini Tanzania, Tigo, imezindua mnara ulioboreshwa kutoka mtandao wa 2G hadi 3G mjini Madanga wilaya ya Pangani ili kuboresha mawasiliano katika mji huo unaojulikana kwa utajiri mkubwa kihistoria na biashara ya uvuvi.  

Akiongea katika sherehe za uzinduzi katika mji wa Madanga, Meneja wa mauzo wa Tigo mkoani Tanga, Robert Kasulwa, alisema upatikanaji wa mtandao wa 3G katika eneo hilo utaleta mabadiliko chanya katika ustawi wa mji huo na ni muhimu katika kuleta maendeleo ya uchumi na kuhamasisha utengenezaji wa ajira. 

"Kwa kuboresha mnara huo kutoka 2G hadi 3G katika mji wa Madanga, tunawaletea huduma bora zaidi wateja wetu kuweza kufurahia huduma za kidigitali za Tigo zinazo ongezeka kila siku na maudhui ambayo yametengenezwa kwa ajili ya elimu, burudani na biashara.  Jambo hili kwa hakika litafungua fursa mpya za kibiashara na kukuza maendeleo ya kiuchumi kwa jamii"

Kasulwa alisema kwamba pamoja na spidi ya Intaneti, mtandao wa 3G una ubora zaidi katika kupiga simu na kiwango chake cha upatikanaji. 

"Mteja atakayenunua kifurushi chochote cha intaneti kutoka katika mtandao ulioboreshwa kutoka 2G kwenda 3G atazawadiwa kifurushi cha 100MB kila mara atakapo nunua. Ofa hii itatumika mpaka kufikia siku 30 tangu kuzinduliwa kwa mnara," alisema. 

Kuzinduliwa kwa huduma ya Tigo ya mtandao wa 3G mjini Madanga ni muendelezo wa uzinduzi wa mtandao wa aina hiyo katika kila mkoa nchi nzima. 

Uzinduzi huu ni wa tisa kati ya maeneo 52 nchi nzima ambayo yako katika orodha ya uboreshwaji kwenda katika mtandao wa 3G au 4G LTE hasa katika kanda ya Kati, Pwani, Kusini, Kaskazini na kanda ya Ziwa.
Meneja wa mauzo wa Tigo mkoani Tanga, Robert Kasulwa, akihutubia wakazi wa Madanga wilayani Pangani wakati wa hafla ya kuzindua mnara ulioboreshwa kutoka mtandao wa 2G hadi 3G

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad