HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, June 7, 2019

WATANZANIA WAISHIO DENMARK,ICS WASHEREHEKEA SIKUKUU YA EID -EL-FITR NA WATOTO WENYE UALBINO

Shirika lisilo la kiserikali la Investing in Childrean and Societies (ICS Africa) kwa kushirikiana na Watanzania Waishio Denmark,shirika la CIS na familia ya Robert Mugeta iliyopo Marekani wamesherekea Sikukuu ya Eid El-Fitr pamoja na Watoto wenye mahitaji maalumu (wenye ualbino,viziwi na wasioona) waliopo katika bweni la Shule ya Msingi Buhangija 'Kituo cha Buhangija' Mjini Shinyanga.

Wadau hao wa watoto wameungana na watoto hao leo Juni 5,2019 kusherehekea Sikukuu ya Eid kwa kucheza,kunywa,kula pamoja na kuwapa zawadi mbalimbali  ikiwemo sabuni,pipi na biskuti. 

  Akizungumza wakati wa sherehe hizo, Meneja wa Shirika la ICS nchini Tanzania linalohusika na masuala mbalimbali ikiwemo malezi na makuzi bora ya watoto,ulinzi na usalama kwa watoto, Kudely Sokoine Joram amesema wanapenda watoto hivyo furaha yao ni kuona watoto hao wanafurahi kama watoto wengine katika jamii. 

  “Tumefanikisha jambo hili kwa kushirikiana na Watanzania wenzetu waishio Denmark,shirika la CIS la Denmark na familia ya Robert Mugeta iliyopo Marekani .Tumekuja hapa kusherehekea na watoto sikukuu ya Eid El Fitr lengo ni kuwafanya watoto hawa wajisikie wanathaminiwa,wanapendwa na tunawajali waone kuwa wao ni sehemu ya jamii”,ameeleza Sokoine. 

  “Watoto hawa wengi wakiwa ni wenye ualbino wanaishi pamoja hapa Buhangija,tumeona ni vyema kusherehekea nao pamoja tofauti na watoto waliopo majumbani ili kuwapa furaha.Tunaushuru serikali na uongozi wa shule kwa kuturuhusu kujumuika nao. Kwa kweli watoto wamefurahia sana”,amesema Sokoine.  

Sokoine ameongeza kuwa wataendelea kushirikiana na wadau wote wakiwemo Watanzania Hawa waliopo Denmark,Marekani pamoja serikali kuhakikisha wanapata ufumbuzi wa changamoto mbalimbali zinazoikabili shule ya Buhangija ‘Kituo cha Buhangija ikiwemo kuhakikisha watoto hao wanakua salama na kupata Haki zao za msingi ikiwemo mazingira salama.

  “Sisi ICS Africa kwa kushirikiana na marafiki zetu pamoja na wadau wengine tutaendelea kushirikiana na serikali kutatua changamoto zilizopo hapa,Tukio la leo ni hatua za mwanzo za kutengeneza mahusiano lakini Mwenyezi Mungu akitujalia tuna kazi kubwa ya kufanya hapa shuleni siku zijazo”,amesema.  

Aidha amewataka watoto hao kuwa watiifu,kufuata maelekezo wanayopewa na walimu na kusoma kwa bidii,kushirikiana na kuwapenda wenzao ili waweze kutimiza ndoto zao. Kwa upande wao,watoto hao wameeleza kufurahia ujio wa wadau hao huku wakizitaja baadhi ya changamoto wanazokabiliana nazo kuwa ni ukosefu wa fensi na taa kwenye mabweni mapya yaliyojengwa hivyo kuomba wadau kujitokeza kuwasaidia.
Meneja wa Shirika la ICS Africa Tanzania Kudely Sokoine Joram akizungumza na watoto wenye ualbino,wasioona na viziwi katika bweni la Shule ya Msingi Buhangija wakati wa kusherehekea Sikukuu ya Eid - El-Fitr leo Juni 5,2019. Sherehe hiyo imeandaliwa na shirika la ICS kwa Kushirikiana na Watanzania waishio Denmark na Marekani - Picha zote na Kadama Malunde - Malunde1 blog
Meneja wa Shirika la ICS Africa Tanzania Kudely Sokoine Joram akizungumza na watoto wanaoishi katika bweni la Buhangija.
Meneja wa Shirika la ICS Africa Tanzania Kudely Sokoine Joram na watoto wakizungumza live kwa njia ya simu 'Video Call' na Watanzania waishio Denmark ambao hawajafanikiwa kufika Buhangija kusherehekea Sikukuu ya Eid El-Fitr pamoja na watoto.
Kulia ni Meneja wa Shirika la ICS Africa Tanzania Kudely Sokoine Joram akikabidhi zawadi ya sabuni za kufulia maboksi nane kwa ajili ya watoto hao.
Watoto wakishindana kucheza muziki.
Meneja wa Shirika la ICS nchini Tanzania Kudely Sokoine Joram akicheza wimbo wa Diamond Platnmuz 'Tetema' na Watoto.
Meneja wa Shirika la ICS Tanzania Kudely Sokoine Joram akitoa zawadi ya pipi kwa watoto waliocheza muziki.
Afisa Huduma kwa jamii kutoka Idara ya huduma za uangalizi,Wizara ya Mambo ya Ndani, Monica Dawa akigawa juisi kwa watoto.
Zoezi la kugawa zawadi likiendelea.
Watoto wakilishukuru shirika la ICS na Watanzania waishio Denmark,shirika la CIS na familia ya Robert Mugeta iliyopo USA kwa kusherehekea nao pamoja sikukuu ya Eid El- Fitr na kueleza changamoto ya ukosefu wa fensi na taa kwenye mabweni mapya. 
MC wakati wa sherehe hizo,Mwalimu Jackson Leonard akitoa neno la shukrani kwa shirika la ICS na Watanzania waishio Denmark,shirika la CIS na familia ya Robert Mugeta iliyopo USA.
Mwalimu mlezi wa watoto hao,Flora Gelard akizungumza na kueleza changamoto walizonazo kuwa ni kukosa ajira hivyo wanafanya kazi kwa kujitolea zaidi.
Ugawaji chakula kwa watoto ukiendelea. Nyama ya kuku,nyama ya ng'ombe,pilau,chips,matunda,maji,soda kama kawaida.
Afisa Huduma kwa jamii kutoka Idara ya huduma za uangalizi,Wizara ya Mambo ya Ndani, Monica Dawa akiwafungulia soda watoto huku wakiendelea kula chakula.
Huku Meneja wa Shirika la ICS Africa Tanzania Kudely Sokoine Joram akigawa soda upande mwingine Afisa Huduma kwa jamii kutoka Idara ya huduma za uangalizi,Wizara ya Mambo ya Ndani, Monica Dawa akifungua soda.
Wadau wakiwa katika picha ya pamoja na watoto wenye mahitaji maalumu Buhangija.
Picha ya pamoja baada ya sherehe : Kikosi kilichofanikisha maandalizi ya sherehe za sikukuu ya Eid El Fitr kwa watoto wenye ualbino,wasioona na Wasiosikia katika bweni la Buhangija mjini Shinyanga.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad