Na Munir Shemweta, KILOSA
Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi William Lukuvi amesema
wizara yake itapitia upya mashamba yote yaliyofutwa na Raisi katika
wilaya ya Kilosa mkoa wa Morogoro.
Lukuvi amesema hayo tarehe 16 Mei 2019 katika kata ya Chanzulu tarafa
ya Kimamba wilaya ya Kilosa mkoa wa Morogoro alipozungumza na wananchi
wa kata hiyo wakati alipokwenda kutatua mgogoro wa Ardhi katika wilaya
hiyo ikiwa ni jitihada za wizara kumaliza migogoro ya ardhi nchini.
Waziri Lukuvi alisema, katika maeneo mbalimbali yapo mashamba
yaliyofutwa na Raisi lakini hayajawekewa utaratibu wa kuyatumia na
hivyo kutoa fursa kwa wajanja wachache kujigawiwa na mengine kuyauza
kwa wananchi bila kufuata utaratibu.
Alisema, katika kuhakikisha mashamba yote yaliyofutwa na Rais katika
wilaya ya Kilosa na kuzua mgogoro baina ya wananchi na wamiliki
wizara yake imeamua kupeleka timu kutoka wizarani kwa ajili ya
kuyafanyia uhakiki mashamba yote yaliyofutwa katika wilaya ya Kilosa.
Kwa mujibu wa Lukuvi timu hiyo inajumuisha Kamishna wa ardhi nchini
Mary Makondo, Kaimu Mkurugenzi wa Upimaji na Ramani Samweli Katambi,
Mthamini Mkuu wa Serikali Evalyne Mugasha, Kamishna Msaidizi wa Ardhi
Kanda ya Kati Ezekiel Kitlya na Wataalamu kutoka idara za Mipango Miji
Wizarani.
Alisema, uamuzi wa kwenda na timu kutoka Wizarani unalenga kumaliza
kabisa migogoro ya ardhi katika wilaya hiyo hasa baada ya kubaini
ofisi za wilaya na mkoa wa Morogoro kushindwa kutatua mgogoro huku
viongozi wa wake wakituhumiwa.
Waziri wa Ardhi alitaja kazi kubwa itakayofanya timu hiyo kuwa ni
kupitia mashamba 15 yaliyofutwa na raisi sambamba na kufufua mipaka
ya mashamba hayo na kazi hiyo itafanywa kwa na ushirikiano wa ngazi za
wilaya.
" Tutayapitia mashamba yote yaliyofutwa na Raisi na kujua kilichomo
ndani yake na timu ya uhakiki niliyokuja nayo itanilitea mapendekezo
ya namna ya kutumia mashamba na mengine watapewa wanaostahili na si
kila mtu atapewa" alisema Lukuvi
Huku akishangiliwa na wananchi wa Chanzulu Lukuvi alisema, wale wote
waliojimilikisha mashamba yaliyofutwa na Rais watanyang'anywa na
kupatiwa wanaostahili na mengine yatatolewa kwa Kituo cha Uwekezaji
Tanzania (TIC) kwa ajili ya kupatiwa wawekezaji.
Mkuu wa Idara ya Ardhi, Maliasili na Mazingira katika halmashauri ya
Kilosa Ibrahim Mndembo alisema, Jumla ya mashamba 25 yenye ukubwa wa
ekari 23,596 kwenye maeneo ya Msowero, Magole na Chanzulu katika
wilaya ya Kilosa yamebatilishwa umiliki baada ya wamiliki wake
kushindwa kuyaendeleza ambapo kati ya mashamba hayo mashamba 15
yalibatilishwa miliki zake katika kipindi cha uongozi wa serikali ya
awamu ya tano.
Mashamba yenye mgogoro na wananchi katika wilaya ya Kilosa ni Noble
Agriculture Enterprises, Magereza dhidi ya wananchi wa Mabane, Mbigiri
na Mabwegere, Chadulu Estate, Shamba la Swai dhidi ya wananchi wa
Ilonga na shamba la Mauzi Estate Malangali.
Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi William Lukuvi akizungumza na wananchi wa Chanzulu Kilosa mkoani Morogoro alipokwenda kutatua migogoro ya ardhi ikiwa ni jitihada za Wizara ya Ardhi kumaliza migogoro ya ardhi nchini.
Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi William Lukuvi
akizungumza na viongozi wa wilaya ya Kilosa alipokwenda kutatua
migogoro ya Ardhi katika wilaya hiyo ikiwa ni jitihada za wizara ya
Ardhi kumaliza migogoro ya ardhi nchini. (PICHA NA WIZARA YA ARDHI)
No comments:
Post a Comment