HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, March 26, 2019

MAFUNZO YA MADAKTARI WA WATOTO WACHANGA KUTOKA AFRIKA MASHARIKI NA KATI YAFANYIKA ZANZIBAR

Na Ramadhani Ali - Maelezo Zanzibar

Mkurugenzi Kinga na Elimu ya Afya Zanzibar Dk. Fadhil Mohd Abdalla amesema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inaendelea kuweka mikakati ya kupunguza vifo vya watoto wachanga chini ya mwezi mmoja vinavyotokana na maambukizi.

Aliitaja mikakati hiyo kuwa ni pamoja na kuhakikisha huduma za maradhi ya maambukizi yanayowasumbua watoto ndani ya wiki ya kwanza tokea kuzaliwa zinatolewa katika vituo vyote vya afya badala Hospitali kuu pekee.

Dk. Fadhil alitoa kauli hiyo alipokuwa akifungua mafunzo ya siku tano ya madaktari wakufunzi kutoka nchi za Afrika Mashariki na Kati katika Hoteli ya Golden Tulip Malindi.

Alisema Zanzibar imepiga hatua kubwa katika kupunguza vifo vya watoto wenye umri wa mwaka mmoja hadi mitatu lakini vifo vya watoto wachanga wa siku saba za mwanzo tokea kuzaliwa bado imekuwa ni changamoto.

Mkurugenzi Kinga na Elimu ya Afya alisema Wizara itaendelea kufundisha Madaktari wa vituo vya ya afya msingi ili kuhakikisha kila kituo kinaweza kutoa tiba ya maambukizi.

“Lengo ni kuhakikisha dawa za maambukizi zilizokuwa zikitolewa Hospitali kuu sasa zinasambazwa katika vituo vya afya ili kupunguza vifo vya watoto wachanga” alisisitiza Dk. Fadhil.

Mwakilishi wa Shirika la Afya Ulimwenguni (WHO) Ofisi ya Brazzaville Congo, ambae ni mtaalamu wa afya ya watoto wachanga Dk. Assumpta Muriizhi, alisema akinamama wanapitia kipindi kigumu katika kipindi cha miaka miwili baada ya kujifungua kutokana na kupambana na afya ya mtoto ambae hawezi kujieleza.

Alisema wapo baadhi ya wazazi hawaoni umuhimu wa kuwapeleka watoto wao Hospitali wanapopata maambukizi jambo linapelekea kuathirika zaidi na hatimae kupoteza maisha.

Aliwashauri akinamama wanapogundua watoto wao wachanga wanasumbuliwa na maradhi kuwawahisha mapema vituo vya afya vya karibu kupata huduma ya awali kabla ya kuwapelekwe Hospitali kuu iwapo matatizo yataongezeka.

Alisema hakuna umuhimu mkubwa kwa watoto wachanga kuwaanzisha huduma za afya katika Hospitali kuu hasa kwa Zanzibar ambapo vituo vya afya vinapatikana kila sehemu.

Mkutano huo unahudhuriwa na Madaktari Wataalamu wa watoto wachanga kutoka Zambia, Zimbabwe, Msumbiji, Kenya, Uganda, Tanzani Bara, Zanzibar na Maafisa

Wawakilishi wa Mashirika ya Kimataifa ya WHO na UNICEF.
 Mwakilishi wa Shirika la Afya Ulimwenguni (WHO) Ofisi ya Brazzaville Congo Dk. Assumpta Muriizhi akizungumza na washiriki wa mafunzo ya madaktari wa watoto katika Hoteli ya Golden Tulip Malindi Mjini Zanzibar.
 Mkurugenzi Kinga na Elimu ya Afya Zanzibar Dk. Fadhil Mohd Abdalla akifungua Mafunzo ya siku tano ya madaktari wa watoto wachanga kutoka nchi za Afrika Mashariki na Kati katika Hoteli ya Golden Tulip Malindi Mjini Zanzibar.
 Baadhi ya washiriki wa Mafunzo ya madaktari wa watoto wachanga kutoka nchi za Afrika Mashariki na Kati wakimskiliza Mkurugenzi Kinga na Elimu ya Afya Zanzibar Dk. Fadhil Mohd Abdalla (hayupo pichani) alipokuwa akifungua mafunzo hayo.
 Mshauri wa afya ya watoto wachanga Dk. Samira Aboubakar akijadiliana na baadhi ya washiri wa mafunzo ya watoto wachanga katika Hoteli ya Golden Tulip Malindi Mjini Unguja. 
 Picha ya pamoja washiriki wa mafunzo ya siku tano ya madaktari wakufunzi wa watotot wachanga kutoka nchi za Afrika Mashariki na Kati na mgeni rasmin. Picha na Makame Mshenga.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad