HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, March 26, 2019

MADAWATI YA JINSIA YA JESHI LA POLISI 450 YAANZISHWA KOTE NCHINI

Serikali inaendelea na utaratibu wa kuanzisha vituo vya mkono kwa mkono kote Nchini kama hatua muhimu ya kuzuia na kupunguza vitendo vya ukatili kwa wanawake na watoto na tayari baadhi ya vituo hivyo vimeanza kufanya kazi katika hospitali za Mwananyamala, Ilala pamoja na Tumbi.

Akiongea Mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Naibu Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile amesema vituo hivyo kimsingi vinalenga kupunguza mzunguko na mlolongo wa huduma kwa wahanga wa ukatili kwani huduma zote ikiwemo ya matibabu, polisi na unasihi zitapatikana kwa wakati na kwa haraka.

Dkt. Ndugulile ameimbia Kamati hiyo ya Bunge kuwa juhudi nyingine zinazofanywa na Serikali katika kupambana na vitendo vya ukatili dhidi ya Wanawake na Watoto ni kuanzishwa kwa takribani Madawati ya Polisi ya Jinsia 450 kote Nchini ambayo yamekuwa msaada mkubwa kwa wanawake wanaofanyiwa vitendo vya ukatili na kulitaka Jeshi la polisi kuongeza madawati hayo kwa kila kituo cha polisi kote Nchini.

Aidha, Naibu Waziri Ndugulile ameongeza kuwa Serikali inajipanga kuanzisha Dawati la Jinsia katika Shule zote Nchini ili kutoa nafasi kwa watoto ambao wanafanyiwa ukatili na hawana mahali pakutolea taarifa kutumia Dawati la Jinsia la Shule kutoa taarifa za vitendo vya ukatili.

Pamoja na mambo mengine Dkt. Ndugulile ameimbia Kamati ya Bunge ya Kudumu ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuwa Serikali inafuatilia vyema huduma zinazotolewa na Mashirika Yasiyo ya Kiserikali ili kuhakikisha Mashirika hayo yanatekeleza shughuli zao kwa kuzingatia Sheria. Ameongeza kuwa Wizara inakamilisha maboresho ya kanzidata ili kuongeza ufanisi katika uratibu wa shughuli za mashirika kwa kutambua kazi zinazofanyika na mchngo unaotolewa katika sekta mbalimbali

Aidha, Katibu Mkuu Wizara ya Afya Idara Kuu Maendeleo ya Jamii Dkt. John Jingu ameimbia kamati hiyo kuwa Wizara inajukumu la kupitia mitaala ya vyuo vya Maendeleo ya Jamii na imekuwa ikifanya hivyo kila baada ya miaka mitano na limekuwa likifanyika kufuatia matokeo ya utafiti ili kubaini mahitaji ya soko la ajira.

Dkt. Jingu alisema hayo alipokuwa akijibu swali la Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Bw. Peter Selukamba aliyetaka kujua kama mitaala ya vyuo hivyo ufanyiwa mapitio ili wataalamu wanaotolewa na vyuo hivyo waendane na mabadiliko ya Sayansi na Teknolojia.

Wizara ya Afya Idara Kuu Maendeleo ya Jamii imekutana leo mjini Dodoma na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa lengo la kuwasilisha rasimu ya Makadilio ya Bajeti ya Mwaka wa fedha wa 2019/2020.
Naibu Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile akiongea Mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii leo Jijini Dodoma.
Baadhi ya Wakufunzi wa Chuo cha Maendeleo ya Jamii wakifuatilia jambo wakati Naibu Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile alipokuwa akiwasilisho hoja Mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii leo Jijini Dodoma.
Baadhi ya Wakurugenzi wa Wizara ya Afya, Idara Kuu Maendeleo ya Jamii wakifuatilia jambo wakati Naibu Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile alipokuwa akiwasilisho hoja Mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii leo Jijini Dodoma.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad