HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, February 27, 2019

SERIKALI YAISHUKURU CHINA KWA KUIPATIA CHUO CHA UTUMISHI WA UMMA KOMPYUTA MPAKATO 20


Serikali ya Tanzania imeishukuru China kwa kuipatia Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) kompyuta mpakato 20 zitakazowasaidia katika shughuli za ufundishaji na kuboresha utendaji kazi kwa watumishi wa chuo hicho.
Akipokea kompyuta hizo kutoka kwa Balozi wa Jamhuri ya Watu wa China nchini Tanzania, Wang Ke, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Kapt (Mst) George Mkuchika (Mb) amemshukuru Balozi huyo kwa mchango wao katika kuboresha Chuo hicho kwa maendeleo ya taifa.
Mhe. Mkuchika amepongeza ushirikiano ambao China imekuwa nao kwa Chuo cha Utumishi wa Umma katika masuala mbalimbali ya kuboresha utendaji ikiwa ni pamoja na watumishi wa chuo hicho kushiriki semina mbalimbali nchini China ambazo zinawasaidia kuongeza ujuzi.
Ameomba ushirikiano huu uzidi kudumu kwani China imekuwa na mahusiano mazuri na Tanzania kwa muda mrefu sasa tangu Serikali ya awamu ya kwanza mpaka sasa.
Pia, Mhe. Mkuchika amemuomba Balozi huyo kusaidia katika ujenzi wa tawi jipya la chuo hicho linalotarajiwa kujengwa jijini Dodoma baada ya Serikali kuhamishia shughuli zake Makao Makuu ya nchi Dodoma na kuongeza kuwa ujenzi wa chuo hicho utatoa fursa kwa watumishi waliohamia Dodoma na mikoa jirani kuongeza ujuzi katika Chuo hicho.
Akikabidhi kompyuta hizo, Balozi Wang Ke amesema, lengo lao ni kuboresha utendaji kazi wa watumishi katika chuo hicho hususan katika kufundisha.
Balozi Wang Ke amefafanua kuwa, anatamani kukiona Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania kikitoa elimu bora zaidi na kikizalisha watumishi wa umma bora nchini.
Aidha, Balozi Wang Ke ameahidi kuendeleza ushirikiano ulioanza kati ya Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania na vyuo vya mafunzo vilivyoko nchini China ili kukuza ushirikiano zaidi na kuendeleza utamaduni wa kujifunza baina ya Tanzania na China.

Hafla hiyo imefanyika katika ukumbi wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania jijini Dar es Salaam na kuhudhuriwa na maafisa kutoka ubalozi wa China nchini Tanzania wakiongozwa na Balozi Wang Ke, Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Utumishi na baadhi ya watumishi wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania.
 Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Kapt (Mst) George Mkuchika (Mb), akizungumza katika hafla fupi ya makabidhiano ya kompyuta kwa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania yaliyofanyika kwenye ukumbi wa chuo hicho jijini Dar es Salaam.
 Mtendaji Mkuu na Mkuu wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania, Dkt. Henry Mambo akitoa neno la utangulizi wakati wa hafla fupi ya makabidhiano ya kompyuta kwa Chuo chake yaliyofanyika kwenye ukumbi wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania jijini Dar es Salaam.
 Balozi wa Jamhuri ya Watu wa China nchini Tanzania, Wang Ke akizungumza kabla ya kukabidhi kompyuta kwa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) wakati wa hafla fupi iliyofanyika kwenye ukumbi wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania jijini Dar es Salaam. Kulia ni Mwenyekiti wa Bodi ya Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC), Dkt. Charles Msonde.
 Baadhi ya watumishi wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania wakimsikiliza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Kapt (Mst) George Mkuchika (Mb) (hayupo pichani) katika hafla fupi ya makabidhiano ya kompyuta kwa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania yaliyofanyika kwenye ukumbi wa chuo hicho jijini Dar es Salaam.
 Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Kapt (Mst) George Mkuchika (Mb) akimkabidhi zawadi Balozi wa Jamhuri ya Watu wa China nchini Tanzania, Wang Ke baada ya hafla fupi ya makabidhiano ya kompyuta kwa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania yaliyofanyika kwenye ukumbi wa chuo hicho jijini Dar es Salaam.
 Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Kapt (Mst) George Mkuchika (Mb), akisalimiana na Balozi wa Jamhuri ya Watu wa China nchini Tanzania, Wang Ke alipowasili Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania kukabidhi kompyuta kwa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania yaliyofanyika kwenye ukumbi wa chuo hicho jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Kapt (Mst) George Mkuchika (Mb) akipokea moja ya kompyuta mpakato kutoka kwa Balozi wa Jamhuri ya Watu wa China nchini Tanzania, Wang Ke katika hafla fupi ya makabidhiano ya kompyuta kwa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania yaliyofanyika kwenye ukumbi wa chuo hicho jijini Dar es Salaam. Anayeshuhudia ni Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Utumishi, Dkt. Laurean Ndumbaro.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad