HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, February 26, 2019

Hii ndio Nafasi ya pekee kwa timu hizi kushinda Kombe Coppa Italia

Kwa timu zilizosalia kwenye Coppa Italia, shindano hili ndio nafasi ya wazi au nafasi pekee kwa timu hizo kushinda Kombe msimu huu. Baada ya kutolewa kwa Juventus ambao wameshinda kombe hilo kwa miaka minne mfululizo timu za AC Milan, Fiorentina, Lazio na Atalanta iliyowafunga Juventus katika robo fainali watategemea kushinda Kombe hilo.

Bahati nzuri hatua ya nusu fainali huwa na mechi za marudiano. Hii inatoa fursa kwa timu zote kutumia vizuri viwanja vya nyumbani.  Lazio dhidi ya AC Milan ndiyo mechi ya kwanza, mchezo huo utapigwa katika dimba la Stadio Olimpico. Lazio maarufu kama I Biancocelesti, wao wanatafuta kushinda Kombe la Coppa Italia kwa mara ya saba, mzunguko uliopita walihitaji mikwaju ya penati ili kufuzu sasa wanakutana na mtihani mwingine dhidi ya wenzao wa jiji la Milan.

Kwa upande wa Rossoneri (AC Milan) watategemea magoli ya straika wao mpya Krzysztof Piatek aliyejiunga nao akitokea Genoa baada ya Gonzalo Higuain kujiunga na Chelsea. Mshambuliaji huyo raia wa Poland amekuwa katika kiwango kizuri tangu ajiunge na AC Milan, amefunga magoli sita katika mechi tano, huku magoli yake mawili yakiwaondoa Napoli katika michuano hiyo. Mchezo wa Lazio vs AC Milan utapigwa Jumanne saa 5:00 Usiku na utarushwa LIVE kupitia ST World Football pekee.

Siku ya Jumatano Fiorentina watacheza dhidi ya Atalanta. Licha ya kuwahi kufika fainali mara tatu pekee, timu ya Atalanta wanaamini wana kila sababu ya kushinda Kombe hasa baada ya kuwang’oa mabingwa Juventus kwa ushindi wa kuvutia 3-0 mashabiki wao wana kila sababu ya kuamini huu ni mwaka wao. Mcolombia Duvan Zapata ndio kinara wao katika ufungaji huku akifunga mabao mawili dhidi ya Juve ya Ronaldo. Mshambuliaji huyo amekuwa na kiwango kizuri mbele ya goli baada ya kutua Atalanta kwa mkopo akitokea Sampdoria.

Fiorentina nao wako katika morali ya hali ya juu baada ya kuwatoa Roma. Fiorentina waliwaadhibu Roma kwa mabao 7-1 katika mchezo ambao mtoto wa Kocha Diego Simeone, Giovanni Simeone alifunga mabao mawili. Mchezo wa Fiorentina vs Atalanta utapigwa Jumatano saa 5:00 Usiku na utarushwa LIVE kupitia ST World Football pekee. Mechi za marudiano zinatarajiwa kupigwa katika wiki ya mwisho ya mwezi April.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad