HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Saturday, February 9, 2019

Bonanza la Muhimbili lafana, timu zagawana makombe

Bonanza la michezo lililoandaliwa na Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) limefana na kuleta ushindani mkubwa kwa timu shiriki za mpira wa pete na miguu za hospitali hiyo na hivyo timu hizo kugawana makombe.

Bonanza hilo limehusisha timu za Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH)-Upanga pamoja na Hospitali Taifa Muhimbili-Mloganzila ambapo katika mchezo wa mpira wa Pete Muhimbili-Upanga imeichapa Muhimbili-Mloganzila magoli 17 kwa 1. Katika mchezo huo timu ya Mloganzila ilionekana kuelemewa kwani walipokua wakifika langoni mwa timu pinzani walishindwa kufunga na hivyo kuwapa uhakika wa kushinda mabao mengi.

Kwa upande wa mpira wa miguu katika kipindi cha kwanza dakika ya 14 timu ya  Muhimbili Mloganzila imeichabanga bao 1 kwa 0 timu ya Muhimbili Upanga bao lililofungwa na mshambuliaji machachari  Edger  Mtitu. Katika kipindi hicho  cha kwanza timu ya Muhimbili Mloganzila ilitawala mpira na kusababisha Muhimbili Upanga kushindwa kufurukuta uwanjani.

Baada ya kumalizika kwa mchuano huo, Mkurugenzi Mtendaji wa Muhimbili Prof. Lawrence Museru alizungumzia umuhimu wa kuendeleza michezo mahala pa kazi ili kudumisha amani, umoja na upendo na pia watumishi kuwa na afya bora hatua ambayo italeta tija katika maeneo ya kazi.

“Nitaendelea kuunga mkono suala la michezo na kusapoti kadiri inavyowezekana maana michezo ni afya, hivyo nawasihi watumishi wa Hospitali ya Muhimbili Upanga na Mloganzila kuendeleza michezo na mjitokeze kwa wingi kushiriki katika michezo mbalimbali,"amesema Prof. Museru.

Kwa upande wao washiriki wa Bonanza hilo wameushukuru uongozi wa hospitali kwa kufanikisha shughuli hiyo ambayo imewaweka karibu watumishi wote wa MNH Upanga na Mloganzila. Bonanza la michezo la Hospitali ya Taifa Muhimbili, Upanga na Mloganzila limefanyika katika viwanja vya michezo vya Jakaya Kikwete Youth Park Kidongo Chekundu jijini Dar es salaam.
 Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Prof. Lawrence Museru akishangilia ushindi wa timu ya mpira wa pete baada ya timu hiyo kuifunga timu ya pete ya Hospitali ya Taifa Muhimbili-Mloganzila magoli 17-1 katika mchezo wa Bonanza uliofanyika katika  Viwanja vya Jakaya Kikwete Youth Park (Kidongo Chekundu) jijini Dar es Salaam.  Wengine katika picha ni  wakurugenzi na watumishi wa hospitali hizo wakishangilia pamoja.
 Kepteni wa timu ya mpira wa miguu wa Hospitali ya Taifa Muhimbili- Mloganzila akishangilia baada ya kuifunga timu ya Muhimbili ,Upanga bao moja kwa sifuri. Muhimbili Mloganzila 1-0 Muhimbili Upanga. Wengine katika picha hii ni Wakurugenzi wa Muhimbili Upanga na Muhimbili Mloganzila.
 Mashabiki wa timu ya mpira wa miguu ya Hospitali ya Taifa Muhimbili-Mloganzila wakishangilia pamoja baada ya timu yao kuifunga timu ya Muhimbili Upanga bao 1-0.
 Mashabiki wa mpira wa miguu wakifuatilia mechi kati ya timu ya Muhimbili Upanga na Muhimbili-Mloganzila.
 Mechi ikiendelea katika viwanja vya Jakaya Kikwete Youth Park (Kidongo Chekundu) leo.
 Wachezaji wa mpira wa pete wa Muhimbili Upanga wakiifungia timu yao bao la sita katika mchezo uliofanyika Jakaya Kikwete Youth Park (Kidongo Chekundu).  Muhimbili Upanga 17- 1 Muhimbili-Mloganzila.
 Baadhi ya mashabiki wakifuatilia mpira wa pete uliofanyika leo kwenye viwanya vya  Jakaya Kikwete Youth Park (Kidongo Chekundu).  
 Baadhi ya watumishi wa Muhimbili wakifanya mazoezi ya pamoja kabla ya kuanza kwa mchezo wa mpira wa pete na mpira wa miguu.
 Watumishi wa hospitali hizo wakiwa katika picha ya pamoja baada ya kumalizika kwa Bonanza hilo.
Wachezaji wa Muhimbili Upanga na Muhimbili-Mloganzila wakiwa katika picha ya pamoja.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad