HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, December 18, 2018

NKANA FC KUTUA LEO JIONI, SIMBA KUBADILI KIKOSI DHIDI YA KMC KESHO



Na Zainab Nyamka, Globu ya Jamii.

Kikosi cha Nkana Fc 'The Devil' kinatarajia kutua leo usiku kwa ajili ya mchezo wa marudiano wa kimataifa wa Kombe la Klabu Bingwa Afrika dhidi ya timu ya Simba utakaochezwa siku ya Jumapili Desemba 23 kwenye dimba la Uwanja wa Taifa. 

Katika mchezo wa kwanza wa timu hizo uliishia kwa Simba kufungwa goli 2-1 uliochezwa mwishoni mwa wiki iliyopita nchini Zambia. 

Taarifa ya kuwasili kwa kikosi hicho imetolewa na Ofisa Habari wa Klabu ya Simba Hajji Manara kuwa Nkana wataingia nchini usiku wa leo wakitokea Zambia kwa ajili ya mchezo wao wa marudiano. 

"Nkana FC wataingia leo usiku wakitokea kwao Zambia kuja kuwakabili Simba kwenye mchezo wa marudiano wa klabu bingwa Afrika na watakuja kwa usafiri wa shirika la ndege la Kenya,kwahiyo leo usiku ndiyo watatua pale Uwanja wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere," alisema Manara. 

Nkana ambayo inatumikiwa na mchezaji wa kitanzaia Hassan Kessy inatua kucheza mchezo huo wa marudiano ikiwa tayari na mtaji wa ushindi wa bao 2-1 waliouvuna kwenye mchezo wa kwanza waliocheza wakiwa nyumbani wiki iliyopita. 

Katika mchezo huo, Simba wanatakiwa wapate ushindi wa goli 1-0 au zaidi ili kuweza kuingia hatua ya makundi ya Klabu bingwa Afrika ila sare yoyote inamuondoa Simba kwenye michuano hiyo na kushuka mpaka Kombe la Shirikisho Afrika.

Mbali na hilo Uongozi wa Simba umesema kuwa utabadilisha kikosi kitakachovaana na wapinzani wao KMC kesho katika uwanja wa Taifa ili kuwapa nafasi wachezaji wengine kujiandaa na mchezo wao dhidi ya Nkana FC ya Zambia.Simba kesho wanakibarua cha kucheza na KMC katika mchezo wa ligi kuu ikiwa ni kiporo chao kutokana na kushiriki mashindano ya Ligi ya Mabingwa Afrika.


 Manara amesema wanatambua wana kazi nzito ya kutetea ubingwa na kuweza kusonga mbele kwenye hatua ya makundi hivyo wamejipanga kuweza kupata matokeo.



"Tuna kazi ya kucheza na KMC kesho, tunawaheshimu wapinzani wetu na tunatambua ushindani uliopo ila tumejipanga kupata matokeo katika mchezo huo na tutabadili kikosi chetu.



"Tutawapa nafasi wachezaji wetu kwenye kikosi ili wengine waendelee na maandalizi dhidi ya Nkana FC ya Zambia, sapoti ya mashabiki ni muhimu katika hili," alisema.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad