HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Sunday, November 25, 2018

NAIBU WAZIRI WA NISHATI SUBIRA MGALLU AMEZINDUA HUDUMA YA UMEME WA BEI NAFUU REA JARIBU MPAKANI MKOANI PWANI

Na  Linda Shebby,  Pwani
NAIBU Waziri wa Nishati Subira Mgallu  amezindua  huduma ya usambazaji wa umeme wa vijijini  REA katika nyumba 22 za awali   katika  kijiji cha Jaribu Magharibi  kilichopo katika Halmashauri ya Wilaya ya  Kibiti Mkoani Pwani ambapo mpango huo umejipanga kuhakikisha  inapeleka huduma  ya umeme huo wa bei rahisi katika vijiji 7,873 vilivyopo nchini kote.

Alisema kuwa, huduma hiyo  ya usambazaji wa umeme Vijijini chini ya REA kwasasa umefikia  hatua ya mzunguko wa pili ambapo mpaka sasa tayari Vijiji 235 tayari  vimepata umeme na huku mzunguko wa tatu utaanza Machi mwakani.

Mgallu alisema kuwa huduma hiyo  ya umeme  wa Vijijini inatolewa kwa gharama ya Sh. 27,000 tu kwa kaya moja  na kwamba Serikali imeweka kiwango hicho ili kuhakikisha kila Mtanzania anayeishi maeneo ya Vijijini ananufaika na huduma hiyo .

“Serikali ya awamu ya tano chini ya Rais Dkt.John Magufuli imejipanga na imeelekeza nguvu zake  katika kuhakikisha mnafikiwa na huduma ya umeme popote mlipo ndiyo maana imeweka gharama nafuu ili kusudi kila mwananchi anayeishi Kijijini aweze kumudu gharama na kupata huduma  hii ya umeme,”alisema Mgallu.

Alisema kuwa kupatikana  kwa huduma hiyo  ya umeme Vijijini inachochea maendeleo ambapo aliwaomba wananchi wanaofikiwa na huduma hiyo kuitumia kikamilifu katika kufanya shughuli zao za uzalishaji kupitia biashara zitakazoweza kuwaongezea kipato.

Hatahivyo,Mgallu aliziomba kaya ambazo bado hazijalipia ni vyema zikachangamkia fursa hiyo ili waweze kunufaika na huduma hiyo kwa haraka kwakuwa Serikali imekusudia kupeleka umeme huo kwa kila aina ya nyumba  zote iwe ya udongo ama  iliyojengwa kisasa zote ziwe na umeme  bila ya ubaguzi.

“Serikali itapeleka umeme huu kwa kila nyumba iwe ya Tembe,Udongo au Matofali, hatutobagua nyumba ila cha msingi ni kuhakikisha unaweka miundombinu ya waya vizuri(Wiring) na unalipia kiasi cha Sh .27,000 tu za kuunganishiwa kwahiyo nawaomba mtumie fursa hii kikamilifu,”alisema

Kwa upande wake Mhandisi Mkuu wa Shirika la Umeme (TANESCO) Mkoa wa Pwani Selemani Mgwira,alisema kuwa Mkoa wa Pwani mpaka sasa unajumla ya Vijiji 150 na kwamba jitihada za kusambaza umeme huo bado zinaendelea kama ambavyo Serikali imeweka mipango yake.

Kuhusu Halmashauri ya Kibiti Mgwira alisema kuwa Kibiti inajumla ya Vijiji 19 ambapo kati yake Vijiji vinne tayari vimepata huduma hiyoya  umeme wa bei nafuu( REA) na kwamba  watahakikisha wanapeleka huduma hiyo katika vijiji vingine  na kwamba  watahakikisha kila anayehitaji umeme huo anapata huduma haraka.
 Naibu  Waziri wa Nishati Subira Mgallu akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Jaribu Magharibi kilichopo katika Wilaya ya Kibiti Mkoani Pwani kuhusiana na  usambazaji wa umeme wa vijijini REA huku akiwataka wachangamkie  fursa  hiyo ili kila nyumba  iwake taa za umeme na kuachana na  matumizi ya vibatari na mishumaa kwani matumizi hayo yanahatarisha usalama wa mali na  maisha yao.
Naibu Waziri wa Nishati  Subira Mgallu akibonyeza swichi ya umeme kwenye  nguzo akiashiria kuwasha umeme  wa REA  katika kijiji cha Jaribu Mpakani kilichopo katika Halmashauri  ya Kibiti Mkoani Pwani.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad