HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, November 22, 2018

MAJALIWA AFUNGUA MKUTANO WA BARAZA LA MAWAZIRI LA NCHI ZA BONDE LA MTIO NILE

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwaamesema Serikali ya Tanzania itaendelea kushirikiana na nchi za Ukanda wa Maziwa Makuu katika kusimamia matumizi endelevu ya maji ya Mto Nile kwa ustawi wa kiuchumi wa nchi zote.
Ameyasema hayo leo (Alhamisi, Novemba 22, 2018) wakati akifungua mkutano wa 21 wa Baraza la Mawaziri la Nchi za Bonde la Mto Nile zilizopo Ukanda wa Maziwa Makuu uliofanyika jijini Dar es Salaam kwa niaba ya Rais Dkt. John Magufuli.
Amesema nchi wanachama hazina budi kuimarisha ushirikiano ili ziweze kusimamia vizuri matumizi endelevu ya maji ya Mto Nile pamoja na kushughulikia changamoto zinazolikabili Bonde la Mto Nile. 
Waziri Mkuu ametaja baadhi ya changamoto zinazolikabili Bonde la Mto Nile kuwa ni pamoja na kushindwa kufikia makubaliano ya kuanzisha Kamisheni ya Kudumu ya Bonde la Mto Nile. “Kwa takribani miaka 10 sasa tumeshindwa kufikia makubaliano.”
Amesema, sambamba na changamoto hiyo nchi wanachama zimekuwa zikichelewa sana kutoa michango yao ili kuziwezesha taasisi zao kutekeleza ipasavyo majukumu yao, jambo ambalo si tu linachelewesha maendeleo bali linatishia usalama wa maji katika Bonde la Mto Nile.

Kufuatia hali hiyo, Waziri Mkuu ametoa mapendekezo mbalimbali ili kuhakikisha kunakuwa na matumizi endelevu ya rasilimali za maji kwenye Bonde la Mto Nile pamoja na kusaidia nchi wanachama kupata maendeleo.

Moja ya mapendekezo yaliyotolewa na Waziri Mkuu ni pamoja na nchi wanachama kutoa elimu kwa wananchi wake kuhusu matumizi sahihi ya maji na umuhimu wa kutunza vyanzo vyake ili kuhakikisha kunakuwepo na matumizi endelevu ya maji.

“Suala jingine ni ulipaji wa michango. Taasisi zetu haziwezi kutekeleza majukumu yake kama hatulipi michango tena kwa wakati maana miradi ya maendeleo haiwezi kutekelezwa kwa haraka kwa kutegemea wafadhili. Ni vema nchi zikalipa michango.”

Kadhalika, Waziri Mkuu amesema maji ni rasilimali muhimu duniani kwa ajili ya uhai wa binadamu, maendeleo ya kiuchumi na kijamii hususani katika kuendesha shughuli za kilimo, uvuvi, ufugaji, utalii na ujenzi, hivyo lazima vyanzo vitunzwe.

Amesema Bara la Afrika ni miongoni mwa maeneo yanayokabiliwa na matatizo makubwa ya maji duniani, ambapo takwimu zinaonesha kuwa takribani nchi 14 hivi sasa zinakabiliwa na uhaba ama upungufu wa maji huku zingine 11 zinatarajiwa kuingia katika kundi hilo ifikapo 2025.

Waziri Mkuu amesema kutokana na hali hiyo mikakati ya makusudi inahitajika ili kuhakikisha chanzo hiko cha maji kinalindwa na rasilimali ya maji katika Bonde la Mto Nile inatumika vizuri.

Mkutano huo umehudhuriwa na Waziri wa Maji, Profesa Makame Mbarawa ambaye ndiye Mwenyekiti wa Baraza la Mawaziri wa Nchi za Bonde la Mto Nile zilizopo kwenye Ukanda wa Maziwa Makuu, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Augustine Mahiga, Waziri wa Nishati Dkt. Medard Kalemani.

Wengine ni Naibu Waziri wa Maji, Jumaa Awesu, Mabalozi wanaoziwakilisha nchi zao nchini, watendaji wa Sekretarieti ya Bonde la Mto Nile kutoka Ukanda wa Maziwa Makuu pamoja na Ukanda wa Mashariki na maafisa wengine wa Serikali.


 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza wakati alipofungua Mkutano wa Baraza la Mawaziri  la Nchi za Bonde la Mto Nile za Ukanda wa Maziwa Makuu kwenye hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam, Novemba  22, 2018. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akisalimiana na Waziri wa Maji, Profesa Makame Mbarawa wakati alipowasili kwenye hoteli ya Serena jijini Dar es salaam kufungua Mkutano wa Baraza la Mawaziri  la Nchi za Bonde la Mto Nile za Ukanda wa Maziwa Makuu kwenye hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam Novemba 22, 2018. 
 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akipata maelezo kutoka kwa Bw. George Lugomela (kulia) kuhusu mashine ya kutambua uwepo wa maji ardhini  kabla ya kufungua Mkutano wa Baraza la Mawaziri la Nchi za Bonde la Mto Nile za Ukanda wa Maziwa Makuu kwenye hoteli ya Serena, Novemba 22, 2018.
 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akitazama burudani ya ngoma  wakati alipowasili kwenye hoteli ya Serena jijini Dar es salaam kufungua Mkutano wa Baraza la Mawaziri  la Nchi za Bonde la Mto Nile za Ukanda wa Maziwa Makuu, Novemba 22, 2018. Wapili kulia ni Waziri wa Maji, Profesa Mbarawa Makame na watatu kulia ni Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano  wa Afrika ya Mashariki,  Balozi Dkt.  Augustine Mahiga. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad