HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, October 5, 2018

WAZIRI MPINA AAPA KUTOENDELEA KUTUMIA MABILIONI KUAGIZA BIDHAA ZA SEKTA ZA MIFUGO NA UVUVI NJE YA NCHI


WAZIRI wa Mifugo na Uvuvi, Luhaga Mpina akitoa hotuba yake ya uzinduzi wa Dawati la Sekta Binafsi la kusaidia sekta za mifugo na uvuvi linaloundwa kwa ushirikiano kati ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB), ASPIRES kwa kushirikiana na SAGCOT, USAID pamoja na Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji jijini Dodoma jana.Walioketi kushoto kwake ni Katibu Mkuu Mifugo, Profesa Elisante Ole Gabrieli, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge, Kilimo, Mifugo na Maji, Mahmoud Mgimwa na Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Abdallah Ulega.

WAZIRI wa Mifugo na Uvuvi, Luhaga Mpina( wa tano kutoka kushoto walioketi) akiwa katika picha ya pamoja na viongozi wa Serikali na taasisi mbalimbali wadau wanaounda Dawati la Sekta binafsi la kusaidia sekta za mifugo na uvuvi nje ya ofisi ya Dawati hilo jijini Dodoma, nyuma ya jengo la Bunge jana . Waliosimama nyuma ni wataalam wa dawati hilo.
WAZIRI wa Mifugo na Uvuvi, Luhaga Mpina akitia saini kitabu cha wageni kwenye ofisi mpya ya Dawati la Sekta Binafsi la kusaidia sekta za mifugo na uvuvi linaloundwa kwa ushirikiano kati ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB), ASPIRES kwa kushirikiana na SAGCOT, USAID pamoja na Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji jijini Dodoma jana. Kushoto kwake anayeshuhudia ni Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Benki ya Kilimo TADB, Japhet Justine, Kulia kwake ni Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Abdallah Ulega

Na John Mapepele, DODOMA
WAZIRI wa Mifugo na Uvuvi, Luhaga Mpina amesikitikishwa na kitendo cha Tanzania kutumia takribani sh. bilioni 100 kila mwaka kuagiza samaki, maziwa na nyama kutoka nje ya nchi licha ya Tanzania kuwa na ng’ombe milioni 30.5 na samaki tani milioni 2.7 walioko kwenye maziwa, mito na bahari bidhaa ambazo zingeweza kuzalishwa nchini na kuleta ajira na kujenga uchumi wa Taifa.

Mpina ametoa kauli hiyo jana jijini Dodoma wakati wa akizindua Dawati la Sekta Binafsi la kusaidia sekta za mifugo na uvuvi linaloundwa kwa ushirikiano kati ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB), ASPIRES kwa kushirikiana na SAGCOT, USAID pamoja na Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji ambapo amesema Serikali ya awamu ya tano haitakubali tena hali hiyo iendelee.

Mpina alisema kutokana na changamoto zilizopo wizara yake imeona kuna umuhimu wa kuunda dawati hilo ili kuunganisha na kuweka daraja baina ya wizara na sekta binafsi, daraja ambalo kwa sasa ni kama limevunjika ili kutoa suluhisho la changamoto zinikazoikabili sekta binafsi katika biashara na uwekezaji kwenye sekta hizo hali itakayoamsha na kuvutia uwekezaji katika mashirika ya Serikali ya NARCO na TAFICO.

“Tumechoka kuona wawekezaji wa Business Plan, michoro , vikao na mawasilisho kibao lakini uwekezaji hakuna, tumechoka kuona nchi yetu inageuzwa kuwa soko la viwanda vya nje vya mazao ya mifugo na uvuvi huku sehemu kubwa ya malighafi ikitokea nchini,tumechoka kuona ajira za watanzania zikipelekwa nje ya nchi, pia Serikali kukosa mapato”alisema Waziri Mpina.

Hivyo Dawati hilo litawaunganisha wadau katika mabenki na Taasisi za fedha ndani na nje ya nchi na kutoa suluhisho la kiutawala na kifedha katika viwanda na maeneo mengine ya wawekezaji.Pia litahusisha maafisa wabobezi kwenye masuala ya Sekta Binafsi, masuala ya kibenki na biashara.

Mpina alisema Ilani ya uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015-2020 ibara ya 25 a-q na ibara ya 27 a-p inaiagiza Serikali kufanya mageuzi katika sekta ya mifugo na uvuvi ili kuongeza uzalishaji, thamani na masoko ya uhakika,mipango ya Serikali kutekeleza majukumu hayo yameainishwa katika ASDPII,FYDPII.

Aliongeza kuwa Rais, Dk. John Pombe Magufuli, wakati wa kampeni za uchaguzi za mwaka 2015 na hata baada ya kuchaguliwa ameahidi kufanya mageuzi makubwa katika sekta za mifugo na uvuvi ambapo pia katika vikao na mikutano mbalimbali ameonyesha kutokuridhishwa na yanayoendelea katika sekta ya mifugo na uvuvi.

“Mhe Rais amekuwa akihoji mara kwa mara kwanini tuagize samaki nje ya nchi, wakati tuna bahari, maziwa na mito yenye raslimali nyingi?? Kwa nini tuagize viatu na nyama kutoka nje wakati tunayo mifugo mingi inayotuzunguka?? Kwa nini tumekuwa na viwanda vingi ambavyo havifanyi kazi maswali haya ya Mheshimiwa Rais ni maagizo na maelekezo kwa Wizara yangu ni lazima yapate ufumbuzi”alisema Mpina.

Hivyo Waziri Mpina akasisitiza kuwa maagizo na maelekezo yote ya Rais Dk. Magufuli ni lazima yapatiwe majibu ya vitendo kabla ya kumalizika kwa awamu ya kwanza ya uongozi wake mwaka 2020.“Tunaapa kutokushindwa na Mwenyezi Mungu atatusaidia. ‘Leaders must be willing to sacrifise for the sake of the vision,for the sake of their people, for the sake of the National’.Pia tunakumbuka maneno mazuri ya Mwandishi wa Dk. Reginald Abraham Mengi katika kitabu chake cha I can, I must, I will the Spirit of Success hivyo hivyo na sisi We can, We Must, We Will. Hatutashindwa” alisisitiza Mpina.

Kwa upande wake Katibu Mkuu- Mifugo, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Prof. Elisante Ole Gabriel alisema wazo la kuundwa kwa dawati hilo limeasisiwa na Waziri Mpina na kwamba wao kama watendaji wakuu wa wizara watasimamia kikamilifu kuhakikisha matokeo ya haraka yanapatikana kutokana na kuanzishwa kwa dawati hilo na kuwezesha mchango wa sekta ya mifugo katika pato la taifa kuongezeka kutoka asilimia 6.9 mwaka 2017.

Naye Katibu Mkuu- Uvuvi, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Dk. Rashid Tamatama changamoto kubwa iliyokuwa inakabili ukoaji wa sekta hiyo ni mikopo hali iliyochangia sekta hiyo kuchangia asilimia 2.2 katika pato la taifa hivyo kuanzishwa kwa dawati hilo kutasaidia kuinua sekta hiyo na kuleta mageuzi makubwa ya kiuchumi.

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Benki ya Kilimo TADB, Japhet Justine aliwawakishia kuwa kwa sasa wavuvi na wafugaji wanakopesheka hivyo kupitia dawati hilo ni dhamira mageuzi ya haraka yatapatikana.Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Kuendeleza Kilimo Nyanda za Juu Kusini (SAGCOT), Geofrey Kirenga kwa sasa taasisi hiyo itaongeza wigo wa kusaidia sekta za mifugo na uvuvi kutokana na kuwepo mipango madhubuti ya kusaidia sekta hizo.


Mratibu wa Mradi wa ASPIRES, Prof. David Nyange kuanzishwa kwa dawati hilo ni fursa kwao kuendelea kuunga mkono juhudi za Serikali katika kufikia uchumi wa viwanda kupitia sekta za mifugo na uvuvi.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad