HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, October 16, 2018

WANANCHI WALIOPISHA MRADI UMEME WA KV400 KUTOKA SINGIDA HADI NAMANGA WAANZA KULIPWA FIDIA

Na Zuena Msuya,  Singida
SERIKALI imeanza kulipa fidia kwa wananchi 4000 waliopisha mradi wa kusafirisha umeme wa msongo mkubwa wa kilovolti 400  kutoka Singida hadi Namanga ambapo zoezi la ulipaji fidia litakamilika hivi karibuni.
Mradi huo wa kusafirisha umeme wa kV400 kutoka Singida hadi Namanga utaunganisha nchi za Tanzania na Kenya na unafahamika kama  (Kenya – Tanzania Power Interconnector Project), (KTPIP).

Naibu waziri wa Nishati, Subira Mgalu alisema hayo alipotembelea eneo la kuhifadhia vifaa vya mradi huo (yard)  katika kijiji cha Nangwa wilayani Hanang mkoani Manyara, mwishoni mwa wiki, ili kukagua vifaa hivyo vitakavyotumika katika ujenzi wa miundombinu ya umeme.

Mgalu alisema kuwa, kazi za awali za utekelezaji wa mradi huo zilikwishaanza na kinachosubiriwa sasa ni kukamisha zoezi la ulipaji fidia kwa wananchi waliopisha mradi husika ili wakandarasi waanze rasmi kazi ya ujenzi.

Mgalu aliweka wazi kuwa, katika utekelezaji wa mradi huo, vijiji 14 vilivyopitiwa na mradi vitapata umeme ambapo vijiji 7 ni vya  Mkoa wa Singida, 2 kutoka Mkoa wa Manyara na 5 ni vya Mkoa wa Arusha.

Alisema kuwa, mradi huo, pia utawezesha ujenzi wa kituo kipya cha kupoza umeme mjini Arusha na kupanua kituo cha kupoza umeme mkoani  Singida.
Alisema kukamilika kwa mradi huo kutatimiza azma ya Serikali ya kuwa na umeme mwingi na wa kutosha ifikapo 2020, na pia kuuza umeme katika nchi za Afrika Mashariki zitakazokuwa zina uhitaji, kupitia Ushirikiano wa pamoja katika Sekta ya Nishati ujulikanao kama East African Power Pool, (EAPP) unaoshirikisha nchi za Uganda, Ethiopia, Rwanda, Burundi, Sudan Kusini pamoja na Kenya.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya na Hanang, John Mkirikiti  alisisitiza kuwa utekelezaji wa mradi huo uzingatie na kutoa kipaumbele cha ajira kwa vijana wenye nguvu walio katika maeneo yanayopitiwa na mradi.

Pia aliahidi kutoa ushirikiano wakati wa utekelezaji wa mradi huo hususan kuimarisha ulinzi na usalama, na  kuwataka vijana watakaopata fursa ya kufanya kazi katika mradi kuwa waaminifu  na wakazi wa maeneo ya mradi kuwa walinzi wa miundombinu hiyo ya umeme.

Akizungumzia ujenzi wa mradi huo, Meneja Msimamizi mkuu wa Utekelezaji wa Mradi huo, kutoka Shirika la Umeme Tanzania ( TANESCO) Mhandisi Oscar Kanyama alisema kuwa upande wa Tanzania mradi huo utajengwa kwa urefu wa kilometa 414 na kwa upande wa Kenya utajengwa kwa urefu wa kilometa 96 kutoka kituo cha kupoza umeme Isinya hadi Namanga.

Mhandisi Kanyama alisema mapema mwezi ujao kazi za kuchimba mashimo pamoja mitaro kwa ajili ya kujenga misingi ya mradi huo itaanza.

Aliweka wazi kuwa mradi huo umefadhiliwa na Serikali ya Tanzania iliyotoa Dola za Marekani  milioni 44, Wadau wa Maendeleo ikiwemo Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) iliyotoa Dola za Marekani milioni 258 na Shirika la Mandeleo la Japani ( JICA) lililotoa Dola za Marekani milioni 89, mradi huo unatarajia kukamilika mwezi Februari 2020.
 Naibu waziri wa Nishati, Subira Mgalu, akikagua yadi ya kuhifadhia miundombinu ya kujenga mradi mkubwa wa kusafirisha umeme wa 400kv kutoka Singida hadi Namanga.
 Naibu waziri wa Nishati, Subira Mgalu( kushoto) akipata maelezo kutoka kwa Meneja Msimamizi wa mradi wa kusafirisha umeme wa msongo mkubwa  wa 400kV, Mhandisi Oscar Kanyama,( kulia) wakati wa ziara ya Naibu Waziri huyo alipotembelea yadi hiyo kukagua vifaa na miundombinu ya kutekeleza mradi huo. 
Baadhi ya vifaa vilivyohifadhiwa katika yadi ya kuhifadhia vifaa na miundombinu ya kujenga mradi wa kusafirisha umeme wa msongo mkubwa wa 400kV kutoka Singida hadi Namanga.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad