Baadhi ya watumishi wa Shirika la umeme nchini, Tanesco mkoawa Rukwa
wakifuatilia hotuba ya Naibu Waziri Subira Mgalu wakati aliwahutubia
wananchi wa kata ya Mtowisa mkoani Rukwa leo, ambapo yupo katika ziara
ya kikazi ya kukaguautekelezaji wa miradi ya REA awamu ya tatu.(0150)
Na Mwandishi wetu, Rukwa.
Naibu Waziri wa Nishati, Subira Mgalu amemuagiza Mkuu wa wilaya ya Sumbawanga, Dk. Halfan Haule kutumia mamlaka yake kuwatupa ndani saa 48 wasimamizi wa utekelezaji wa mradi wa usambazaji umeme vijijini (REA) awamu ya tatu wa Kampuni ya Nakuroi Investment iwapo watasuasua katika ujenzi wa miundombinu ya umeme wilayani humo.
Naibu Waziri huyo, ametoa agizo hilo leo akiwa katika kijiji cha Kilyamatundu kilichopo mpakani mwa mikoa ya Mbeya na Songwe tarafa ya Kipeta wilayani Sumbawanga mkoani Rukwa, ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya kikazi inayolenga kukagua utekelezaji wa miradi ya REA awamu ya tatu mkoani humo.
Kabla ya kuoa agizo hilo, Naibu Waziri huyo alionyeshwa miundombinu inayowezesha upatikanaji wa umeme katika kijiji jirani cha Kamsamba iliyopo umbali wa mita 100 na kuonyesha kushangazwa kwanini Kijiji cha Kilyamatundu kinashindwa kunufaika na huduma ya umeme kwa kuwa miundombinu ipo jirani kiasi hicho.
"Mkandarasi nataka nguzo na vifaa vingine vifike hapa Alhamisi ijayo kama ulivyoahadi na ujenzi wa miundombinu ya umeme ianze mara moja,.......mkuu wa wilaya hakikisha inatumia mamlaka yako kuwatupa ndani saa 48 hawa jamaa kama watasuasua kutekeleza mradi huu, sisi lengo letu umeme upatikane hapa kijijini haraka iwezekanavyo" alisema
Aliongeza kwamba hatua hizi zichukuliwe kwa kuwa kampuni hii imekuwa ikishindwa kutekeleza mradi huu kwa wakati, hivyo kuonyesha dalili ya kushindwa kumaliza kwa muda uliopangwa.
Kwa upande wake, mkuu wa wilaya hiyo Dk. Haule aliahidi kutekeleza agizo hilo kwa kuwa serikali imechoka kuendelea kuchonganishwa na wananchi kwa uzembe wa baadhi ya watu hivyo sheria lazima ichukue mkondo wake.
Aidha, Mbunge wa jimbo hilo Iginas Malocha alisema kuwa iwapo eneo hilo litapata huduma ya umeme ni wazi kwamba thamani ya mazao yao kama vile mpunga itaongezeka na wakulima kuwa na uhakika wa soko.
No comments:
Post a Comment