HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, August 9, 2018

MCHEKESHAJI MZEE MAJUTO AAGA DUNIA

Msanii mkongwe  Mzee Amri Athuman al maarufu kama " King Majuto"  (pichani, enzi za uhai wake) amefariki dunia usiku huu katika hospitali ya Muhimbili jijini Dar es salaam alikokuwa amelazwa kwa siku kadhaa mara tu baada ya kurejea nchini kutoka nchini India alikopelekwa na serikali kwa matibabu.
Afisa habari wa Chama cha Filamu na Waigizaji, Masoud Kaftany, amethibitisha kifo cha King Majuto, wakati msanii maarufu mchekeshaji Lucas Lazaro Mhuvile maarufu kama Joti ameandika msiba huo katika mtandao wake wa Instagram, ikiambatana na picha yake akiwa na msanii Mpoki walipokwenda kumjulia hali hospiali.

Joti ameandika kwenye ukrasa wake wa Instagram: “R.I.P @Kingmajuto. metuachia Maumivu Makubwa sana ktk Tasnia ya Comedy Tanzania Sisi wanao,Tutakukumbuka kwa kazi zako,Upendo wako,Tabasamu lako Daima milele,Tulikupenda sana ila Mungu amekupenda zaidi,Pumzika kwa Amani Mzee wetu.”
Mwigizaji nyota wa vichekesho Steve Nyerere naye kwa masikitiko makubwa amethibitisha habari hiyo kwa kusema: "Kweli kaka, Mzee wetu katutoka. Tunalia kwa kumpoteza Mzee wetu..."
Muigizaji huyo alizaliwa mwaka 1948 jijini Tanga na kusoma shule Msambwini, huko huko Tanga.  Alianza fani ya kuigiza akiwa na umri mdogo wa miaka tisa, na toka wakati huo amekuwa kileleni katika fani ya uigizaji hadi mauti yalipomkuta.
Marehemu King Majuto alirejea nchini hivi karibuni akitokea nchini India alikokuwa amekwenda kwa ajili ya matibabu akisumbuliwa na ugonjwa wa tezi dume katika Hospitali ya Apollo. 
Mara aliporejea alipelekwa moja kwa moja katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kwa ajili ya uangalizi.
Kabla ya kupelekwa nchini India Mei 4, mwaka huu, King Majuto ambaye pia alikuwa akisumbuliwa na tatizo la nyonga, alilazwa katika Hospitali ya Tumaini jijini Dar, kisha akahamishiwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili.
Inna lillahi wa inna ilayhi raji'un 
( إِنَّا لِلّهِ وَإِنَّـا إِلَيْهِ رَاجِعُونَ‎)
Pumzika kwa amani King Majuto. 
Mola aiweke roho yako mahala pema peponi... 
AMIN.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad