HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, July 16, 2018

Wachimbaji Wadogo Handeni Kunufaika na Kituo cha Umahiri

Frank Mvungi- MAELEZO, Handeni
Serikali Wilayani Handeni imewataka wananchi kutumia fursa ya kujengwa kwa Kituo cha umahiri katika Wilaya hiyo kujiletea  maendeleo kupitia sekta ya madini.
Akizungumza katika mahojiano maalum kuhusu ujenzi wa kituo hicho kinachojengwa na Wizara ya Madini kupitia mkandarasi ambaye ni SUMA JKT,  Mkuu wa Wilaya hiyo Mhe. Godwin Gondwe amesema hiyo ni fursa  adhimu kwa wananchi wa Wilaya hiyo kwa kuwa watajengewa uwezo wa namna bora ya kushiriki katika uchimbaji wa madini kwa kuzingatia sheria na kanuni zinazosimamia sekta hiyo.
“Wananchi sasa hawatahitaji kusafiri kwenda mikoa mingine kujifunza namna ya kuchimba madini, kuchenjua na hata kushiriki katika kuendeleza sekta hii kwa kuwa kituo cha umahiri  ( Centre of  Excellence) kinajengwa hapa Handeni hivyo ni jambo la kuishukuru Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Uongozi wa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuona kuwa kuna umuhimu wa kuwainua wachimbaji wadogo kwa kuwaongezea ujuzi” Alisisitiza Mhe. Gondwe.
Akifafanua Gondwe amesema kuwa Wilaya hiyo ina hazina kubwa ya madini ya aina mbalimbali ambayo hayajachimbwa hivyo ujenzi wa kituo hicho utasaidia katika kuimarisha usimamizi wa rasilimali hizo na kuwainua wananchi kwa kuwa watachimba madini hayo kwa kuzingatia sheria ikiwemo kulipa kodi zote na hivyo kuondoa tatizo la uwepo wa wachimbaji wasiozingatia weledi na sheria ya madini.
Kwa upande wake mwakilishi wa SUMA JKT. Luteni Khalfani Mturi akizungumza kwa niaba ya Meneja wa ujenzi Kanda ya Kaskazini Meja Daudi Zengo  amesema kuwa dhamira yao baada ya kukabidhiwa eneo la ujenzi wa mradi ni kuhakikisha kuwa mradi unakamilika kwa muda uliopangwa kwa kuzingatia ubora na mkataba wa mradi huo kati yao na Wizara ya Madini inayotekleza mradi huo.
Aliongeza kuwa jukumu kubwa sasa ni kuanza utekelezaji wa ujenzi wa kituo hicho ili kukamilisha kazi hiyo kwa wakati.
Kwa upande wake Mjiolojia kutoka Wizara ya Madini Bi Veronica Nangale amesema kuwa wanamatumaini kuwa mkandarasi ambaye ni SUMA  JKT atakamilisha mradi  kwa wakati na kwa kuzingatia mkataba wa mradi huo.
Naye Msanifu Majengo kutoka kampuni ya InterConsult  Ltd inayosimamia mradi huo Bw. Beno Matata amesema kuwa Kampuni hiyo itasimamia mradi huo kwa kuzingatia  weledi ili ukamilike kwa wakati na kwa ubora unaotakiwa kwa mujibu wa mkataba na sheria za ujenzi.
Kujengwa kwa kituo cha umahiri katika Wilaya ya Handeni kutasaidia wachimbaji wadogo kujengewa uwezo wa kuchenjua madini kwa kutumia teknolojia rafiki kwa mazingira, biashara ya madini, mafunzo ya usalama na afya sehemu za kazi, utunzaji wa mazingira kwenye migodi.
Ujenzi wa vituo vya umahiri unatekelezwa kupitia mradi wa Usimamizi Endelevu wa Rasilimali Madini “Sustainable Management of Mineral Resouces Project- SMMRP”, Vituo hivyo vinajengwa katika maeneo mbalimbali hapa nchini ambapo mradi huo unathamani ya jumla ya zaidi ya bilioni 11 zitakazotumika kujenga vituo hivyo katika maeneo mbalimbali ikiwemo Handeni Mkoani Tanga.
 Mkuu wa Wilaya ya Handeni Bw. Godwin Gondwe akisisitiza umuhimu  wa Kituo cha umahiri  kwa wachimbaji wadogo wa madini Wilayani Handeni kinachojengwa na Wizara ya Madini ikiwa ni sehemu ya mikakati ya kuinua wachimbaji hao katika Wilaya hiyo na maeneo yote ya mikoa ya jirani na Wilaya hiyo.
 Luteni  Khalfani Mturi  kutoka Jeshi la Kujenga Taifa (JKT)akipokea ramani ya Kituo cha umahiri (Centre of Excellence) kwa wachimbaji wadogo wa madini kwa niaba ya meneja wa ujenzi wa SUMA JKT Kanda ya Kaskazini Meja. Daudi Zengo  kutoka kwa Mshauri muelekezi wa mradi huo Bw. Beno Matata kutoka Kampuni ya Inter Consult Ltd, mradi huo unatekelezwa na Wizara ya Madini katika Wilaya ya Handeni, kupitia Mradi wa Usimamizi Endelevu wa Rasilimali Madini unaotekelezwa na Wizara ya Madini  ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa ahadi za Serikali katika kuwainua wachimbaji wadogo.
 Msanifu majengo wa Kampuni ya Inter Consult Ltd Bw. Beno Matata akieleza mikakati ya kampuni hiyo katika kuhakikisha kuwa inasimamia mradi huo wa ujenzi wa Kituo cha Umahiri kitakachowanufaisha wachimbaji wadogo kinachojengwa Wilayani Handeni ikiwa ni sehemu ya Juhudi za Serikali kupitia Wizara ya Madini kuinua wachimbaji hao.
 Mjiolojia wa Wizara ya Madini Bi. Veronica Nangale akisisisitiza jambo  kwa mkuu wa Wilaya ya Handeni Godwin Gondwe (hayupo pichani) wakati walipomtembelea Ofisini kwake kabla ya hafla ya kukabidhiwa kwa eneo kitakapojengwa kituo  cha umahiri(Centre of Excellence) kwa wachimbaji wadogo wa madini, hafla hiyo ilifanyika Wilayani Handeni, ujenzi wa kituo hicho unafanyika kupitia  Mradi wa Usimamizi Endelevu wa Rasilimali Madini unaotekelezwa na Wizara ya Madini  ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa ahadi za Serikali katika kuwainua wachimbaji wadogo.
 Luteni  Khalfani Mturi  kutoka Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) akisisitiza jambo mara baada ya kukabidhiwa eneo na ramani ya Kituo cha Umahiri kwa wachimbaji wadogo wa madini kinachojengwa na mkandarasi SUMA JKT, ikiwa ni sehemu ya juhudi za Wizara ya Madini kuimarisha sekta hiyo na kuwainua wachimbaji wadogo.
Afisa Mipango mji wa Wilaya ya Handeni Bw. Byabato William akisisitiza jambo kwa Luteni  Khalfani Mturi  kutoka Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) wakati  wa hafla ya kukagua na kukabidhi eneo litakalotumika kujenga kituo cha Umahiri kinacholenga kuwajengea uwezo wachimbaji wadogo Wilayani Handeni.
(Picha zote na Frank  Mvungi- MAELEZO, Handeni- Tanga)

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad