HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, July 27, 2018

Naibu Katibu Mkuu ataka vikwazo vya lugha kuondolewa kwenye mitaala Afrika

Na Mwandishi wetu
NAIBU Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Elimu ya Ufundi, Avemaria Semakafu ametaka kuvunjwa kwa vikwazo vya lugha vinavyosababisha mkanganyiko wa utoaji elimu barani Afrika kwa kutumia Kiswahili.

Alisema mataifa ya Afrika yamekuwa yakibabaika katika matumizi ya lugha za kikoloni ambazo zimesababisha pia kuwa na ulingafu dhaifu wa utoaji elimu kwa bara hili.

Alisema hayo kwenye kongamano la Mataifa zaidi ya 16 yaliyo Kusini mwa Jangwa la Sahara ambayo yamekuwa yakikutana kuanzia Jumatano kujadiliana namna bora ya kutengeneza mitaala na vifaa vya kufundishia ili kuboresha mbinu za kufundisha na kujifunza.

Alisema ipo haja ya kuondokana na mifumo ya mapokeo ambayo imejaa taratibu za kikoloni zinazompima mtu kwa mitihani na akifeli kuonekana hana uwezo, wakati waliofeli ndio wanafanya vyema katika maisha ya kawaida ya kila siku.

Akizungumza na wawakilishi hao ambao wanashiriki katika kongamano la siku tatu katika Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT), Kinondoni Dar Es Salaam, Naibu Katibu Mkuu huyo alisema ipo haja ya kuangalia mfumo mzima na kupata vigezo halali vya kutathmini mafanikio ya elimu kwa kuangalia elimu yenyewe mitaala na namna ya uwekaji wa ulinganifu wa matokeo.

Alitaka mataifa ya Afrika kutumia lugha moja ya Kiswahili katika ufundishaji ili kuondokana na kikwazo cha lugha ambacho alisema ni moja ya kifaa cha utamaduni wa utoaji elimu.

Alisema lugha ndio inamfinyanga mtu na watu waweza kusikiklizana kwa kutumia lugha moja wanayoelewana lakini si katika mazingira ya sasa ambapo ndani ya mkutano zaidi ya lugha tatu zinatumika kuwezesha mawasiliano.

“Tumekubaliana katika nchi za Afrika Mashariki, zipo sita sasa kutumia Kiswahili kwa kuweza kuwafikia watu wetu na kujipima kwa lugha tunayoifahamu yenye utamaduni tunaouelewa… Alisema Naibu huyo.

Aidha alisema watoaji elimu ni laizma kuangalia upatikanajai wa elimu wenyewe ambao unapaswa kuzingatia mahitaji ya kila kundi badala ya kuwa na elimu jumuishi ambayo inawaweka watu pamoja lakini hawawezi kupata msaada.

Alitaka kuwepo na upatikanaji wa elimu kwa wote kwa kuzingatia mahitaji halisi na si kuchanganya watu wote katika kundi moja na kufundishwa na walimu wasiojua mahitaji ya makundi maalumu.

Alitaka washiriki kuona udhaifu uliopo katika utungaji wa mitaala, ufundishaji na upimaji kwa lengo la kuhakikisha kwamba sehemu zote hizo tatu zinashirikiana katika kutoa matokeo chanya ya elimu kwa watu wa bara la Afrika.

Aidha alishukuru Unesco kwa kuandaa kongamano hilo ambalo alisema kwamba limekuja wakati muafaka, wakati ambapo mataifa mengi ya Afrika yanahangaika kujua kumetokea kasoro gani katika mifumo yao ya elimu huku ikishindwa kutoa ushindani miongoni mwa wanaomaliza madarasa ya msingi kuelekea vyuo vikuu pia kutoa majawabu yanayokanganya kwa walioshindwa katika mitihani kuwa bora zaidi katika maisha.

Naye Anna Theresa, mwakilishi wa UNESCO kanda ya Afrika Mashariki akiwa na makao nchini Kenya aliwataka washiriki kutoa nafasi ya kubadilishana elimu kuhusiana na utungaji wa mitaala, ufundishaji na upimaji wenye lengo la kutanzua tatizo la watu wengi kutokuwa na elimu katika ukanda huu.

Aliwataka washiriki kuangalia changamoto zilizopo katika sehemu zote tatu za utoaji elimu, changamoto ambazo zinasababisha utoaji elimu kuwa mgumu au kuwa na matokeo yanayojali zaidi kushinda kwa mitihani.

Alisema changamoto kubwa ni kuweka pamoja maeneo yote matatu ili yaweze kusaidia kutoa maarifa ya kweli kwa wahusika.

Wawakilishi hao watatumia kongamano hilo kubadilishana uzoefu wa namna ya kushirikiana na kufanyakazi kimtandao ili kuboresha mazingira ya kujifunza kwa mamilioni ya wananchi wake ambao hawajui kusoma wala kuandika.

Mataifa hayo 16 yanakutana wakati soko la wahitimu limekuwa likibadilika sana huku likihitaji elimu kiasi kidogo sana cha shule lakini utaalamu mkubwa na uwezo wa kuendelea kujifunza kwa kipindi kirefu

Nchi zinazokutana kutafakari mitaala na namna ya kuiboresha ili kutekeleza moja ya malengo ya maendeleo endelevu SDGs, lengo la nne ni pamoja na Benin, Burkina-Faso, Burundi,Jamhuri ya Afrika ya Kati, Chad, Gambia, Lesotho, Liberia, Malawi, Mali, Niger, Senegal, Ethiopia, Sudan Kusini,Comoro, Zimbabwe, Mwenyeji Tanzania na Uganda.

Katika kongamano hilo la siku tatu ambalo litafuatiwa pia na mafunzo ya Online kwa wiki nane yamelenga kutambua udhaifu katika mitaala na namna ya kukabiliana nayo ili elimu iweze kuwa rafiki na inayowezekana kwa wote.

Kongamano hilo ambalo limeandaliwa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni, UNESCO wakisaidiana na Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT), linaendeshwa na mtandao wa TALENT ambapo Mratibu wake Valérie Djioze-Gallet kutoka UNESCO ofisi ya Kikanda iliyopo Dakar, Senegal alisema kwamba kongamano hilo linatakiwa kutoa matokeo chanya kuhusiana na namna ya kujifunza.

Anasema lengo ni kufanya elimu ya msingi na sekondari kuwa na misingi halisi ya kujifunza kwa kuwa na mtaala bora huku watoto wakiwa tayari kujifunza na kuendelea kujifunza bila ukomo kwa kuzingatia mahitaji yao ya darasani na nje.

Pia kongamano hilo linaangalia namna ya kukuza idadi ya watu wanaojua kusoma kuandika na kuhesabu na pia elimu ya stadi za maisha zinazotolewa kwa vijana.

Mratibu huyo amesema kwamba wakati watu milioni 202 wakiwemo watoto na vijana hawasomi ni asilimia 51 tu wanaofika na kuchukua masomo. Anasema kutokana na hali hiyo Unesco imeamua kutafuta sababu ya idadi kubwa ya watu kutojifunza kuangalia uzito wa tatizo na kutafuta njia ya kubadilika na kuwezesha watoto zaidi kuingia katika masomo na kuelewa.

Mada kadhaa zenye kuelekeza na kuchanganua masuala ya mitaala na mafunzo zinatarajiwa kujadiliwa na kufikiwa muafaka wa namna bora ya kuendesha masuala ya elimu kwa kuwa na mtaala ambao unajibu mahitaji ya wananchi na si mahitaji ya watahini.

Kongamano hilo linalofanyika katika ukumbi wa Chuo Kikuu Huria likimalizika litakuwa limewawezesha washiriki wake ambao ni watunga sera, watu wa mitaala,wadau wa elimu na pia asasi zisizio za kiserikali zinazoshughulikia elimu,timu za mitaala za kitaifa, kutoa majawabu ya nini kifanyike na kwanini kwa lengo la kuwa na ufanisi katika mafunzo na elimu.

Naye Hugo Labate mmoja wa wataalamu waliofika kutoa mada katika kongamano hilo amesema kwamba japokuwa tehama inafanya shughuli za kujifunza kuwa rahisi, shida ipo katika kuangalia kwanini kutoa elimu hiyo, namna ya kutoa elimu na nini watu wapewe kama elimu.

Huga aliwauliza washiriki nini maana hasa ya mtaala katika dunia ya leo na suala llinalokwenda sanjari la ubora elimu.

Aliwataka washiriki kujadiliana kwa undani masuala ya mitaala kwa kuielewa na kuona namna nzuri ya kuioanisha na mahitaji halisi ya elimu kwa mazingira ya sasa na kwa kutumia tehama kwa nguvu zake zote.

Alisema wakati jamii inapambana na hali yake kuondokana na umaskini na kutengwa kibaguzi kwa kukosekana elimu ipo haja kwa jamii yenyewe kutengeneza mfumo utakaowezesha kuwa na mafanikio ya kujifunza kwa kuwa na mtindo shirikishi ambao waliojifunza wote wanatumia elimu yao kwa maendeleo.

Hata hivyo alisema hali ya sasa ambapo maana ya elimu imefinywa na wanafunzi wengi kujikuta wakijifunza kwa ajili ya kujibu mitihani, kunafanya elimu ya darasani kutokuwa na maana nje ya madarasa hayo.

Alishauri watunga mitaala kuangalia kwa makini suala la mtaala na aina nya watu wanaozalishwa na mitaala hiyo huku wazazi wakihofia mabadiliko yanayowafanya vijana wao wasijiandae na hali mbaya ya baada ya wao kuwa kazini au kumaliza shule.

Alisema jamii inatoa mkanganyiko wa haja mbili na kufanya mambo kuwa magumu yanayohitaji watunga mitaala kutuliza akili zao na pia kushirikiana kupata kitu chenye uhakika.

“Nipatie elimu ambayo nitaielewa, kuimiliki, kuipima kwa vipimo vya kawaida kama mitihani na kupanga madaraja, lakini pia uwaandae watoto wangu kwa hali ya baadae isiyotabirika” anasema Hugo.

Mtaalamu huyo amewataka walimu kuangalia mitaala na kuibadili ili ijibu haja ya sasa badala ya kuwa na mtaala wa zamani ambao ulikuwa na hoja za kujibu za wanazuoni lakini si kwa maisha halisi.
Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Elimu ya Ufundi, Dk . Avemaria Semakafu akifungua kongamano la kikanda kuhusu ulinganifu wa mafunzo, mitaala, mafunzo kwa walimu na vifaa vya kufundishia mataifa zaidi ya 16 yaliyo Kusini mwa Jangwa la Sahara ili kubadilishana uzoefu wa namna ya kushirikiana na kufanyakazi kimtandao ili kuboresha mazingira ya kujifunza kwa mamilioni ya wanafunzi kwenye nchi hizo liliofanyika jijini Dar es Salaam. Kongamano hili limeandaliwa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni-UNESCO na linaendeshwa na mtandao wa TALENT.
Mkurugenzi wa UNESCO kanda ya Afrika Mashariki na Afisa Mwakilishi wa Unesco nchini, Ann Therese Ndong- Jatta akizungumzia umuhimu wa mafunzo hayo wakati wa kongamano la kikanda kuhusu ulinganifu wa mafunzo, mitaala, mafunzo kwa walimu na vifaa vya kufundishia lililokutanisha nchi 16 ili kutekeleza moja ya malengo ya maendeleo endelevu SDGs, lengo la nne lililofanyika Jijini Dar es Salaam. Kongamano hili limeandaliwa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) na linaendeshwa na mtandao wa TALENT.
Mratibu wa mtandao wa watoa elimu na mafunzo kwa mabadiliko (TALENT) kutoka UNESCO Dakar, Valérie Djioze-Gallet akizungumzia madhumuni kuratibu kongamano hilo la kikanda linalojadili kuhusu ulinganifu wa mafunzo, mitaala, mafunzo kwa walimu na vifaa vya kufundishia ili kukabiliana na changamoto zilizopo katika sekta ya elimu hasa kwenye nchi zilizo Kusini mwa Jangwa la Sahara (SSA) ili kufikia lengo la nne la maendeleo endelevu (SDGs) katika elimu. Kongamano hili limeandaliwa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) na linaendeshwa na mtandao wa TALENT.
Mtaalamu Mwandamizi wa Elimu kutoka Taasisi ya Global Partnership for Education, Ramya Vivekanandan akizungumza kwenye kongamano la kikanda kuhusu ulinganifu wa mafunzo, mitaala, mafunzo kwa walimu na vifaa vya kufundishia mataifa zaidi ya 16 yaliyo Kusini mwa Jangwa la Sahara ili kubadilishana uzoefu wa namna ya kushirikiana na kufanyakazi kimtandao ili kuboresha mazingira ya kujifunza kwa mamilioni ya wanafunzi kwenye nchi hizo liliofanyika jijini Dar es Salaam. Kongamano hili limeandaliwa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) na linaendeshwa na mtandao wa TALENT.
Mkufunzi kutoka nchini Argentina, Hugo Labate akitoa mada namna ya kutumia mitaala inayoendana na nchi husika wakati wa kongamano la kikanda kuhusu ulinganifu wa mafunzo, mitaala, mafunzo kwa walimu na vifaa vya kufundishia ili kukabiliana na changamoto zilizopo katika sekta ya elimu hasa kwenye nchi zilizo Kusini mwa jangwa la Sahara (SSA) lilinalofanyika kwa simu tatu jijini Dar es Salaam. Kongamano hili limeandaliwa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO)na linaendeshwa na mtandao wa TALENT.
Mkufunzi kutoka makao makuu ya Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) nchini Ufaransa,  Maya Prince akizungumzia tathmini kwenye masomo yanayotumika katika sekta ya elimu hasa kwenye nchi zilizo Kusini mwa Jangwa la Sahara (SSA) wakati wa kongamano lililowakutanisha wadau wa elimu kutoka nchi mbalimbali barani Afrika.
Mkufunzi kutoka Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE), Enas Abulibdeh akitoa mada kuhusu mfumo wa elimu unaotumika katika nchi hizo kwa kuhusanisha na mitaala inayotumika kwenye nchi mbalimbali za barani Afrika ili kuongeza ufanisi kwenye nchi hizo wakati wa kongamano hilo linalofanyika jijini Dar es Salaam.

Baadhi ya wadau kutoka nchi mbalimbali wakichangia mada kwenye kongamano la kikanda linalohusu ulinganifu wa mafunzo, mitaala, mafunzo kwa walimu na vifaa vya kufundishia ili kukabiliana na changamoto zilizopo katika sekta ya elimu hasa kwenye nchi zilizo Kusini mwa Jangwa la Sahara (SSA).
Baadhi ya wanakamati ya maandalizi ya kongamano hilo kutoka Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO)
Baadhi ya wadau kutoka nchi mbalimbali wakifuatilia mada kwenye kongamano la kikanda linalohusu ulinganifu wa mafunzo, mitaala, mafunzo kwa walimu na vifaa vya kufundishia ili kukabiliana na changamoto zilizopo katika sekta ya elimu hasa kwenye nchi zilizo Kusini mwa Jangwa la Sahara (SSA).
Ofisa Mradi wa Shirika la Sayansi, Elimu na Utamaduni la Umoja wa Mataifa ( UNESCO) nchini, Jennifer Kotta akizungumza jambo wakati wa kongamano la kikanda kuhusu ulinganifu wa mafunzo, mitaala, mafunzo kwa walimu na vifaa vya kufundishia mataifa zaidi ya 16 yaliyo Kusini mwa Jangwa la Sahara ili kubadilishana uzoefu wa namna ya kushirikiana na kufanyakazi kimtandao ili kuboresha mazingira ya kujifunza kwa mamilioni ya wanafunzi kwenye nchi hizo liliofanyika jijini Dar es Salaam. Kongamano hili limeandaliwa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni-UNESCO na linaendeshwa na mtandao wa TALENT.
Mgeni rasmi Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Elimu ya Ufundi, Dk . Avemaria Semakafu katika picha ya pamoja ya washiriki wa kongamano la kikanda kuhusu ulinganifu wa mafunzo, mitaala, mafunzo kwa walimu na vifaa vya kufundishia mataifa zaidi ya 16 yaliyo Kusini mwa Jangwa la Sahara ili kubadilishana uzoefu wa namna ya kushirikiana na kufanyakazi kimtandao ili kuboresha mazingira ya kujifunza kwa mamilioni ya wanafunzi kwenye nchi hizo liliofanyika jijini Dar es Salaam. Kongamano hili limeandaliwa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni-UNESCO na linaendeshwa na mtandao wa TALENT.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad