Shirika la Viwango Tanzania (TBS) limeendelea kutoa elimu kwa wadau wa sekta ya ujenzi kuhusu umuhimu wa kuzingatia viwango, katika Maonesho ya 22 ya Wahandisi yanayoendelea kufanyika kwenye ukumbi wa Mlimani City, Dar es Salaam.
Akizungumza kwenye Maonesho hayo leo Septemba 26, 2025, Meneja wa Viwango wa TBS, Mhandisi Yona Afrika, amesema shirika hilo limeshiriki kwenye maonesho hayo kwa lengo la kuwakumbusha wahandisi kuhakikisha bidhaa zinazotumika katika miradi mbalimbali ya ujenzi zinapimwa na kuthibitishwa na maabara za TBS
“Wanatakiwa kutumia bidhaa zilizothibitishwa katika maabara zetu. Tuna jumla ya maabara kuu tisa, lakini tatu kati ya hizo ndizo zinazohusiana moja kwa moja na uhandisi, ambazo ni maabara ya mitambo, maabara ya umeme na maabara ya ujenzi,” amesema Mhandisi Yona.
Aidha amesema kuwa wahandisi wanapaswa kuhakikisha vifaa vyao vinapimwa kupitia vipimo vya ugezi vinavyopatikana TBS, ili kujiridhisha kuhusu umahiri na ubora wake kabla ya kuvihusisha katika ujenzi wa makazi, madaraja na miundombinu mingine.
Pamoja na hayo Mhandisi amesema vipimo vinavyotolewa na shirika hilo vinazingatia usahihi wa vifaa vinavyotumika kwenye sekta ya ujenzi na umeme, ikiwemo waya, taa na vifaa vingine vinavyohitaji kudumu kwa muda stahiki.
“Tunataka vipimo vyetu viwe sambamba na matokeo sahihi, ili bidhaa zinazozalishwa ziwe na viwango vinavyokubalika kitaifa na kimataifa,” ameongeza.
Vilevile, amewataka wahandisi kutumia rejea ya viwango vya Kitanzania wanapoandaa upembuzi yakinifu wa miradi mbalimbali, ili kuhakikisha miradi hiyo inatekelezwa kwa ubora na usalama unaohitajika.






No comments:
Post a Comment