RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ametoa wito kwa Mashirika na Taasisi za Umma kuhakikisha yanawajibika ipasavyo katika kulinda na kuendeleza uwekezaji wa Serikali kwenye mashirika hayo, na kuchangia kikamilifu kwenye maendeleo ya kiuchumi.
Kwa Mujibu wa taarifa iliyotolewa na Shaaban Kissu, Naibu Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu, imeeleza kuwa Rais Dkt. Samia ametoa wito huo leo katika hafla ya kupokea gawio na michango kutoka kwa Taasisi na Mashirika ya Umma na Kampuni ambazo Serikali ina hisa.
Katika hotuba yake, Rais Dkt. Samia amesema kuwa mageuzi makubwa yanayotekelezwa na Serikali kwenye usimamizi na uendeshaji wa Mashirika ya Umma yameanza kuonesha mafanikio, ikiwemo Mashirika 11 kati ya 13 yaliyokuwa na mtaji hasi kuhamia kwenye kundi lenye mtaji chanya, na Mashirika mengine nane katika hayo yaliyokuwa yanapata hasara sasa yameanza kupata faida.
Katika kuzidi kuongeza mchango wa Mashirika kwenye uchumi, Rais Dkt. Samia amemuagiza Msajili wa Hazina, Bw. Nehemiah Mchechu kuendelea kuwajengea uwezo watendaji na kuhakikisha mashirika yanaongeza ubunifu na kuimarisha matumizi ya TEHAMA.
Vilevile, amemtaka Msajili wa Hazina kufanya tathmini ya kuangalia namna ya kuongeza ushiriki wa wananchi katika umiliki wa mashirika kupitia soko la hisa.
Rais Dkt. Samia pia amesisitiza umuhimu wa kutambua Mashirika na Taasisi ambazo hazitoi mchango wa fedha moja kwa moja kwa Serikali, bali huchangia kupitia kuboresha utoaji huduma kwa wananchi.
Serikali imepokea gawio la jumla ya Shilingi Trilioni 1.028 kutoka katika Mashirika na Taasisi za Umma ikiwa ni ongezeko la asilimia 34 ikilinganishwa na Shilingi Bilioni 767 zilizotolewa mwaka jana.
Aidha, idadi ya Mashirika na Taasisi zilizochangia imeongeza kufikia 213, huku kampuni zenye hisa chache za Serikali zikiwa miongoni mwa wachangiaji wakubwa, zikiwemo Twiga Minerals (Shilingi Bilioni 93.6), Airtel Tanzania (Shilingi Bilioni 73.9) na NMB Bank (Shilingi Bilioni 68.1).
No comments:
Post a Comment