NA EMMANUEL MBATILO, MICHUZI TV
Kampuni ya mawasiliano ya Airtel Tanzania kwa kushirikiana na Baraza la Taifa la Uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) pamoja na wadau wengine wa mazingira, wamefanya zoezi la usafi katika fukwe za bahari eneo la Mbezi Beach B, jijini Dar es Salaam.
Akizungumza na waandishi wa habari leo Juni 13,2025 katika zoezi hilo Mkurugenzi wa Mawasiliano na Udhibiti wa Airtel Tanzania, Beatrice Singano amesema kuwa Airtel imejikita katika kuhakikisha mazingira yanabaki kuwa salama kwa kuelimisha wateja wake kupitia ujumbe mfupi kuhusu umuhimu wa usafi, hasa katika mikoa yenye uzalishaji mkubwa wa taka.

Aidha Beatrice ameongoza ujumbe wa taasisi ya Airtel kwa vitendo kwa kuwapatia vifaa vya kuhifadhia taka wakazi wa eneo hilo ambapo amewasihi kudumu kuendelea kufanya zoezi hilo si kwaajili ya viumbe vya baharini pekee lakini pia kwaajili ya afya zao.
Sambamba na hayo Beatrice kwaniaba ya Mkurugenzi Mkuu wa kampuni ya Airtel ameahidi kuandaa mazungumzo rasmi na NEMC kwa ajili ya kufanya zoezi hilo kuwa endelevu kwa lengo la kudumisha mazingira salama kwa viumbe hai wa bahari lakini pia kwaajili ya binadamu.

Kwa upande wake,Kaimu Mwenyekiti wa NEMC Kanda ya Mashariki Jeremiah Nyakwaka ametoa rai kwa wazalishaji wa taka hatarishi kama plastiki na makopo kuhakikisha wanazihifadhi ipasavyo ili kuepusha madhara ya kimazingira, na akazihimiza taasisi na wananchi kwa ujumla kuwa mabalozi wa uhifadhi wa mazingira.
Nae,Mwenyekiti wa mtaa Mbezi Beach-B Asha Vionatis ameishukuru Airtel na NEMC kwa kushirikiana nao katika juhudi za usafi, akieleza kuwa hatua hiyo ni muhimu kwa afya ya jamii na uchumi wa taifa kupitia sekta ya uvuvi.
“Takataka zinazoingia baharini huathiri moja kwa moja viumbe hai kama samaki, ambao ni sehemu muhimu ya pato la taifa,” amesema Asha.


























No comments:
Post a Comment