HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, May 19, 2025

WAKANDARASI WOTE ILALA IFIKAPO JUNI 2025 MIRADI IKAMILIKE - DC MPOGOLO.


Wakandarasi waliopewa kazi za ujenzi wilayani ilala,  Mkoani Dar es salaam,  wametakiwa kuhakikisha hadi ifikapo mwezi juni mwaka huu wawe wamekamilisha miradi yote ya barabara kwa wakati. 

Kauli hiyo imetolewa na  Mkuu wa wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo, katika ziara yake ya kukagua utekelezaji wa ilani ya Chama Cha Mapinduzi katika  miradi ya maendeleo kwenye  sekta ya miundombinu alipokagua  barabara na madaraja. 

Mpogolo amesema kuwa  wakandarasi waliopewa kazi katika halmshauri ya jiji watumie muda uliobaki baada ya mvua kukatika kurudi katika miradi hiyo kuendelea na ujenzi ili wananchi waendelee kupata huduma baada ya miradi hiyo kusimama kutokana na mvua. 

Mpogolo, amekagua miradi ya   barabara yenye urefu kilometa 7 na madaraja zaidi ya matatu yanayojengwa kwa mapato ya ndani,  katika jimbo la Segerea, Ilala na Ukonga. 

Mkuu huyo wa wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo amemshukuru Rais Dokta Samia Suluhu Hassan kwa  kuidhinisha kiasi cha shilingi  bilioni  10. 7 kwa ajili ya ujenzi wa  barabara za ndani zinazojengwa kwa kiwango cha  lami pamoja na madaraja ili kurahisha mawasiliano kwa wananchi.  

Amesema fedha hizo tayari zimeanza kujenga  madaraja 3 katika jimbo la Ukonga na Segerea na ujenzi wa  barabara zenye urefu wa kilometa 7  ambazo zinajengwa katika maeneo ya  liwiti,  kariakoo na pugu halisi. 

Mpogolo ametumia nafasi hiyo  kuwashukuru wabunge wote watatu wanaotoka katika halmashauri ya jiji la Ilala kwa jitihada kubwa walizofanya pamoja na baraza la madiwani kwa kuhakikisha bajeti ya mwaka huu inapitishwa ili kukamilisha miradi ya maendeleo. 

Ambapo pia  amewaomba  wananchi kuendelea kuwa na subira kutokana na changamoto zilizojitokeza wakati wa ujenzi wa miradi hiyo, na kuwahimiza  wakandarasi kufanya kazi  zao na kutimiza wajibu wao ili wakamilishe miradi hiyo. 

Amesema wakandarasi ambao walikwama kutokana na mvua kushindwa kubeba malighafi kufika eneo la ujenzi sasa waanze kazi kutokana na mvua kuanza kupungua, na halmashauri itatumia vifaa vyake ili kukarabati barabara za pembezoni zirudi katika hali ya kawaida. 

Mpogolo, amebainisha baraza la madiwani katika  halmashauri ya jiji la Dar es salaam, kwa kushirikiana na mkurugenzi wa jiji Helihuruma Mabelya wanaendelea kutoa fedha kwa ajili ya utekelaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo na kuhakikisha wakandarasi wanalipwa fedha zao kwa wakati. 

Aidha Mpogolo,  amewataka tarura wilayani ilala, kuwachukulia hatua wakandarasi wasiomaliza kazi, wasumbufu na kulalamika bila kutimiza wajibu wao wasipewe kazi nyingine kwa kushindwa kutimiza wajubu wao. 

Amesema wakandarasi wenye sifa na wanaofanya kazi zao vizuri katika miradi ndiyo wawe na sifa za kuendelea kufanya kazi ili fedha zinazotolewa ziendane na kazi zinazifanywa kwa kuleta tija kwa wananchi wenye  changamoto ya miumdombinu katika maeneo yao.  

Kuhusu wananchi waliojenga pembezoni mwa madaraja makubwa yanayopitisha maji mengi, Mpogolo amewasihi wananchi hao kuondoka na kuwapongeza wale ambao wamechukua hatua za kuhama baada ya kuona wapo katika mikondo ya maji hali inayohatarisha usalama wao. 

Kwa upande wake Mwandisi Greyson Nzunda wa  halmashauri ya wilaya ya Ilala,  amemuhakikishia mkuu huyo wa wilaya, Tarura itahakikisha inawasimamia wakandarasi wanarudi katika maeneo ya miradi mara moja baada ya mvua zinazoendelea kukatika. 

Amesema nia ya tarura ni kuhakikisha miundombinu yote iliyokua na changamoto inajengwa na kurudisha mawasiliano kwa wananchi kwa kata moja  na nyingine. 

Mzunda ameishukuru serikali kwa kuendelea kutoa fedha hivyo wananchi wategemee ukamilikaji wa miradi hiyo na wao kuendelea kupata huduma nzuri za kijamii ili waendelee kujiletea maendeleo. 

Amesema kipindi hiki cha mvua miradi mingi ilisimama na wakandarasi wengi kushindwa kuendelea na kazi hivyo watahakikisha kazi zote zilizosimama zinaendelea baada ya mvua kukatika.









No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad