HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, April 4, 2024

SIMALENGA AKUNWA NA JITIHADA ZA KILIMANJARO ONE KUKUZA UTALII WA KIUTAMADUNI BARIADI

 

Mkuu wa Wilaya ya Bariadi, Simon Simalenga (kulia) akisalimiana na Mkurugenzi wa Kilimanjaro One Travel and Tours walipokutana leo Aprili 4, 2024 katika ofisi ya mkuu wa mkoa ili kufanya mazungumzo kuhusu tamasha la Lake Zone Cultural and Tourism Festival linalotarajiwa kufanyika Bariadi mwezi Julai mwaka huu.

Na Mwandishi wetu.
MKUU wa Wilaya ya Bariadi, Simon Simalenga amaipongeza kampuni ya Kilimanjaro one Travel and Tours kwa kuunga mkono kwa vitendo juhudi za serikali katika kukuza utalii wa kiutamaduni

Mkuu huyo wa Wilaya amesema hayo ofisini kwake wakati akifanya mazungumzo na baadhi ya viongozi wa kampuni ya Kilimanjaro One waliomtembelea ili kufanya mazungumzo kuhusu tamasha la Lake Zone Cultural and Tourism Festival ambalo litafanyika Bariadi Simiyu Julai 5, 6 na kilele chake ni Julai 7, 2024.

“Tamasha hili linaendana na azma ya Rais Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha kila halmashauri inaandaa tamasha la utamaduni na utalii,” amesema.

Simalenga amesema serikali iko tayari kutoa ushirikiano kwa waandaaji hao na kuwakumbusha kuwa wasukuma wanathamnini utamaduni wao na kuwa wako tayari kuutangaza muda wote.

“Tunataka wageni waje kwa wingi wajionee utamaduni wa wasukuma na tunaamini kuwa jambo hili litawavutia watu wengi zaidi kwani mkoa wetu wa Simiyu una vivutio vingi vya kitamaduni na kitalii.

Pia, ametoa wito kwa mashirika mbalimbali ya umma na ya binafsi yanayofanya shughuli zake katika eneo hilo kuhakikisha yanadhamini tamasha hilo ambalo litaenda sambamba na maonyesho ambayo yatawapa wadhamini nafasi ya kutangaza bidhaa na huduma zao.

Aidha ametoa wito kwa waandaaji hao pia kuhakikisha wanatangaza tamasha hilo kwa njia mbalimbali ikiwemo vyombo vya habari na magari ya matangazo ili ujumbe ufike kwa watu wengi zaidi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Kilimanjaro One Travel and Tours, Mohamed Hatibu amesema kampuni yake imejiandaa vizuri kuratibu tamasha hilo ambalo linafanyika kwa mara ya kwanza lakini litakuwa inafanyika kila mwaka katika Wilaya ya Bariadi Mkoa wa Simiyu.

“Tunatarajia kukusanya watu wasiopungua 7,000 katika tamasha hili maarufu kama mbina ambalo huwa ni hafla maalumu kuadhimisha kilele cha msimu wa mavuno katika jamii ya wasukuma.

Amesema tamasha hilo pia lina lengo la kuwavutia watalii wa ndani na nje na kusisitiza kuwa muda mwafaka ni sasa wa kuutangaza utamaduni wa Simiyu ili dunia nzima ifahamu,” amesema.

Pia, Hatibu amemueleza Mkuu wa Wilaya kuwa mipango inaendelea vizuri ili kuhakikisha tamasha hilo linafanyika kwa kiwango cha hali ya juu na kuongeza kuwa hakutakuwa na kiingilio kwa watu wote ambapo watapata fursa ya kujionea matukio mbalimbali katika tamasha hilo.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad