HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, July 19, 2023

PROF. MKENDA AMEITAKA TCU KUSIMAMIA VYUO KUFANYA TAFITI MAENEO BOBEZI

 Na Karama Kenyunko, Michuzi Tv

WAZIRI wa Elimu Sayansi na Teknolojia Profesa Adolf Mkenda, ameitaka Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU) kusimamia vyuo vyake kufanya tafiti katika maeneo bobezi yanayotatua changamoto za kijamii na kuchapisha matokeo yao kwenye majarida ya kimataifa.

Aidha, ameagiza tume hiyo kuongezea juhudi katika kudhibiti ubora wa vyuo ili mitaala itakayokuwepo ijibu mahitaji ya soko.

Profesa Mkenda ameyasema hayo leo Julai 18,2023 katika wakati akifungua maonyesho ya 18 ya vyuo vikuu nchini yenye kaulimbiu "Kukuza ujuzi nchini kupitia elimu ya juu, Sayansi na Teknolojia kwa uchumi imara na shindani.

Amesema kuwa ni wakati wa TCU kuhakikisha inasimamia tafiti na kutoa ushauri kwa vyuo nchini ili vitoe majibu ya changamoto yanayoikabili jamii.

Ameeleza kuwa vyuo hivyo vinapaswa kuimarisha ushirikiano na taasisi za utafiti na sekta binafsi ili kuweka utaratibu wa kuendeleza teknolojia zinazoanzishwa nchini na kuhamasisha matumizi yake ili kupata maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Aidha, Profesa Mkenda ameiagiza vyuo vikuu vyote kutumia fursa zilizopo nchini ili kuhimili ushindani ndani na nje ya nchi.

Awali, Mwenyekiti wa Bodi ya TCU, Profesa Penina Mlamba amesema wataendelea kusimamia vyuo kutoa elimu yenye tija kwa wahitimu na Taifa kwa ujumla.

Amesema wataendelea kuboresha maonyesho hayo ili kuwa chachu ya kuzifanya taasisi za elimu ya juu kuwa chachu kwa maendeleo.

""Serikali ipo kwenye mabadiliko ya mitaala TCU itaendelea kuchagiza vyuo vikuu kupokea mabadiliko hayo,"amesema Profesa Mlamba.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila amesema wahitimu wa vyuo hawapaswi kuelekeza lawama kwenye mitaala wanapokosa ajira kwani kupitia mitaala iliyopo wapo wanafunzi walioajiriwa na kujiajiri.

Ameeleza kuwa pamoja na maboresho ya mitaala, wana wajibu wa kujisimamia ili maisha yafanikiwe.

Maonyesho hayo ya 18 yameanza Julai 17 na yatahitimishwa Julai 22 mwaka huu, huku taasisi 83 za elimu zikishiriki ikilinganishwa na taasisi 75 zilizoshiriki mwaka jana.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Adolfu Mkenda, (kulia) akisikiliza maelezo kutoka kwa Katibu Mtendaji wa Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU), Prof. Charles Kihampa, (kushoto) wakati alipokuwa akikagua Mabanda ya Taasisi mbalimbali za elimu ya juu zilizoshiriki Maonesho ya 18 ya Elimu ya Juu, Sayansi na Teknolojia yanayofanyika katika viwanja vya Mnazi Mmoja Jijini Dar es Salaam
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Adolf Mkenda, (katikati) akimsikiliza Katibu Mtendaji Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU), Prof. Charles Kihampa, (kushoto) alipokuwa akifafanua jambo wakati Waziri huyo alipofika katika Banda la TCU kufahamu mambo mbalimbali kuhusu maonesho hayo, aliyoyafungua rasmi Julai 18,2023 katika Viwanja vya mnazi mmoja Jijini Dar es Salaam.



No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad