HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, May 12, 2023

TAKUKURU PWANI YABAINI MADUDU KISARAWE UPOTEVU WA MIL.29.4 UJENZI JENGO LA ICU

Kamanda wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU)  Mkoa wa Pwani Christopher Myava akizungumza na waandishi wa habari.

Na Khadija Kalili
TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Pwani imebaini mapungufu ya vifaa vya ujenzi vyenye thamani ya Mil. 29.4 kutokuwepo kwenye mradi wa Ujenzi wa Jengo la Wagonjwa Mahututi (ICU) la Wilaya ya Kisarawe lenye thamani ya milioni 300.

Akizungumza kwenye mkutano na Waandishi wa Habari Mjini Kibaha Mei 11 Kamanda wa Takukuru Mkoa wa Pwani Christopher Myava ameelezea utendaji kazi kipindi cha miezi mitatu Januari hadi Machi mwaka huu.

Myava amesema kuwa TAKUKU Mkoa wa Pwani wamegundua kuwa vifaa hivyo vimenunuliwa kwa bei kubwa tofauti na ile ya soko na havikutumika kwenye ujenzi na havikuwepo kabisa kwenye eneo la ujenzi.

"Kufuatia mapungufu hayo tumebaini uchunguzi unaendelea na ukikamilika hatua kali na za kisheria zitachukuliwa kwa wahusika,"amesema Kamanda Myava.

Amesema kuwa mradi huo ni moja kati ya miradi mitatu iliyokutwa na mapungufu baada ya kufanyiwa ufuatiliaji yenye thamani ya Bilioni 4.9 kati ya 40 iliyochunguzwa yenye thamani ya Bilioni 9.6 katika kipindi hicho.

"Kwenye mradi wa pili wa maendeleo ya jamii ni kutokuwepo kwa miradi iliyoombewa mikopo na kupitishwa na Kamati ya fedha ambapo kikundi cha Twaweza kilichopo Kata ya Tangini Halmashauri ya Mji Kibaha kimepewa mkopo wa Milioni 21kwa ajili ununuzi wa nafaka badala yake wakaanzisha duka la nyama na hawajarejesha mkopo tangu wakope mwaka 2022,"amsema Kamanda Myava.

Aidha amebainisha kwa kusema kuwa fedha hizo zilizokopeshwa ni sehemu ya fedha zinatokana na asilimia 10 ya mapato ya Halmaahauri ya Mji Kibaha ambapo ni Bilioni 4.5 na makundi maalumu yanayokopeshwa ni wanawake, vijana na watu wenye ulemavu.

Amesema kuwa mradi wa tatu wa ujenzi Shule ya Msingi Madege Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha umekutwa na mapungufu ya kukosekana kwa ubora wa sakafu ya madarasa mawili na Ofisi ya Mwalimu na uwepo wa mipasuko kati ya fremu za milango na kuta kwenye mradi wenye thamani ya Milioni 112.5.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad