HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, May 17, 2023

MTATIRO AWATAKA MAFUNDI WANAOJENGA MADARASA YA BOOST KUEPUKA UDANGANYIFU NA WIZI WA VIFAA

 

Na Muhidin Amri, Tunduru
SERIKALI wilayani Tunduru,imewataka mafundi wanaofanya kazi za ujenzi wa miradi ya maendeleo kuepuka kushirikiana na watendaji wasiokuwa waaminifu hasa maafisa manunuzi wa Halmashauri kufanya udanganyifu juu ya ubora wa miradi ili kujipatia fedha.

Kauli hiyo imetolewa jana na Mkuu wa wilaya hiyo Julius Mtatiro,baada ya kuzindua ujenzi wa vyumba tisa vya madarasa ambapo kati ya hivyo,viwili kwa ajili ya elimu ya awali,matunduu ya vyoo,jengo la utawala na kichomea taka katika shule ya msingi Ligoma wilayani humo.

Madarasa hayo na miundombinu mingine ya elimu, yanajengwa kupitia mradi wa kuboresho upatikanaji wa fursa sawa katika ujifunzaji bora kwa elimu ya awali na msingi(Boost) ambapo serikali imetoa jumla ya Sh.milioni 513,200,000.00.

Aidha Mtatiro ambaye ni mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama wilayani humo, amewaonya wahandisi kuhakikisha wanatekeleza miradi ya ujenzi kwa kuzingatia sheria za usimamizi wa fedha na manunuzi ya fedha za serikali za mitaa na siyo vinginevyo.

Amewakumbusha kuhusu umuhimu wa mradi huo, na kutothubutu kabisa kubadili matumizi ya fedha kwa kuwa serikali imeshafanya tathimini ya kina kuhusu maeneo yaliyopangwa kujengwa shule au kufanya ukarabati wa miundombinu katika maeneo yote.

Alisema,kupitia mpango wa Boost Serikali imeweka kipaumbele kwenye maeneo yenye msongamano mkubwa wa wanafunzi,vijiji visivyokuwa na shule,maeneo ambayo wanafunzi wake wanatembea umbali mrefu na shule zenye uchakavu.

Mtatiro,amempongeza RaiS Dkt Samia Suluhu Hassan kwa ubunifu wake wa kutafuta fedha ambazo zinakwenda kuondoa kero za ufundishaji kwenye shule za msingi wilayani Tunduru.

Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya hiyo Chiza Marando,amewaomba wananchi kusaidia ulinzi wa vifaa vya ujenzi pale vinavyotoka stoo hadi eneo la ujenzi kwani baadhi ya mafundi na wasimamizi wanatumia nafasi hiyo kuiba vifaa vinavyoletwa kwa ajili ya kazi.

Amemuagiza Mwalimu Mkuu wa shule hiyo,kuhakikisha vifaa vyote vinavyotoka stoo vinasindikizwa na wajumbe wa kamati ya ujenzi na kamati ya manunuzi kwani kuna baadhi ya watu wanaweza kukwamisha utekelezaji wa miradi ya Boost.

Amewaomba wananchi wa Ligoma na maeneo mengine ambayo miradi hiyo inatekelezwa,kutoa ushirikiano kwa kamati za ujenzi na kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wake ili iweze kukamilika kwa muda uliopangwa.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad