HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, February 21, 2023

SERIKALI ITAENDELEA KUSHIRIKIANA NA WANANCHI-MAJALIWA

Baadhi ya wanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Wasichana, Lucas Maria ya Ruangwa Mkoani Lindi wakimsikiliza Waziri Mkuu na Mbunge wa Ruangwa, Kassim Majaliwa wakati alipozungumza baada ya kukagua mradi wa ujenzi wa Bweni shuleni hapo, Februari 21, 2023.

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa ambaye pia ni Mbunge wa Ruangwa akizungumza na wanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Wasichana, Lucas Maria wilayani Ruangwa baada ya kukagua Mradi wa Ujenzi wa Bweni shuleni hapo, Februari 21, 2023. Kulia ni mkewe Mary Majaliwa. 
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa ambaye pia ni Mbunge wa Ruangwa akikagua mradi wa ujenzi wa Maabara katika Shule ya Sekondari, Mary Majaliwa wilayani Ruangwa Mkoa wa Lindi, Februari 21, 2023. Kulia ni Mkewe Mary Majaliwa na wa pili kulia ni Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Zainab Telack. 
(Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)


WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa amesema Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan itaendelea kuungana na wananchi katika kuimarisha miundomibu ya elimu ili kuhakikisha watoto Wakitanzania wanapata elimu bora na kutimiza ndoto zao.


Waziri Mkuu amesema kuwa Mheshimiwa Rais Dkt. Samia ameendelea kuweka mikakati ya kuhakikisha watoto wanapata elimu bora kuanzia ngazi ya elimu msingi hadi chuo.


Amesema hayo leo (Februari 21, 2022) alipotembelea shule za Sekondari za Lucas Malia na Mary Majaliwa zilizopo Ruangwa Mkoani Lindi. “Rais Dkt. Samia anaweza sababu amekuwa kiongozi imara, ameendelea kusisitiza kuwa yupo pamoja nanyi.”


Waziri Mkuu amesema kuwa pamoja na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia kuweka mkazo katika kuipa hadhi sekta ya elimu, pia amewekeza kwenye elimu ya mtoto wa kike kwa kuweka sheria zitakazo muwezesha mtoto wa kike kutimiza ndoto zake


“Pamoja na kwamba Mheshimiwa Rais wetu Dkt. Samia anasimamia ubora wa elimu kwa watoto wote ikiwemo wakiume, watoto wetu wa kike tumewawekea mikakati mahsusi ikiwemo sheria kali kwa wanaotaka kumkwamisha na sisi tunazisimamia ili aanze darasa ya awali mpaka atakapomaliza akiwa salama.”


“Wazazi hii shule ni yetu, watoto ni wetu ni lazima tuwalinde na kuchangia kasi ya maendeleo katika shule hii, tuwatembelee walimu wetu ili tuwatie moyo, tunataka watoto wasome ili wafikie ndoto zao.”


Naye, Mkuu wa Mkoa wa Lindi Zainab Telack amesema kuwa mkoa huo unatekeleza mpango mkakati ambao unafanyiwa mapitio kila mwaka ili kuona kwenye mapungufu kwa lengo la kurekebisha walipokosea na kukuza ufaulu kwa shule mkoani Lindi.


Ameongeza kuwa kupitia mpango huo wamefanikiwa kupunguza daraja sifuri kwa asilimia 40 na daraja la nne kwa zaidi ya asilimia 45. “Asilimia zaidi ya 50 ya waliomaliza mwaka jana wataenda kidato cha tano na tunauhakika mtoto aliyemalia kidato cha sita mkoani Lindi anakwenda chuo kikuu.”
Kwa upande wake, Mke wa Waziri Mkuu mama Mary Majaliwa amewataka wanafunzi hao wasome kwa bidii na wasijihusishe na makundi ovu na badala yake waweke malengo katika masomo yao ili waweze kutimiza ndoto zao kielimu.


“Nawahusia watoto wangu someni ili muweze kupata sifa za kuwa viongozi na kuajiriwa ili muweze kuitumikia nchi yetu, Mheshimiwa Rais Dkt. Samia amefanya mambo makubwa sana katika kuliinua Taifa.”

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad