HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, December 30, 2022

MAGARI RUKSA KUPITA JUU MAKUTANO YA UHASIBU

  WAZIRI wa Ujenzi na Uchukuzi Prof. Makame Mbarawa ameruhusu magari kuanza kupita juu katika makutano ya barabara ya Kilwa na Mandela jijini Dar es Salaam ili kupunguza msongamano kwa watumiaji wa barabara hizo.


Akizungumza alipokagua na kuruhusu magari kuanza kupita katika barabara hiyo, Prof. Mbarawa amesema lengo la Serikali ni kuhakikisha inapunguza msongamano jijini Dar es Salaam na kuwawezesha wananchi kusafiri kwa uhakika na wakati.

“…TANROADS hakikisheni magari yanatumia barabara za juu kuanzia leo ili kumuwezesha mkandarasi kuendelea kujenga barabara za chini,” amesisitiza Prof. Mbarawa.

Waziri huyo wa Ujenzi amesema kuanzia mwaka 2023 barabara inayoishia Mbagala itaendelea kujengwa kuanzia Mbagala hadi Vikindu KM 17 ili kupunguza kabisa msongamano katika barabara hiyo ya Kilwa.

Amemtaka Mkandarasi BOTEX anayejenga sehemu ya katikati ya Jiji kufanya kazi usiku na mchana ili kukamilisha haraka eneo hilo na kuondoa usumbufu kwa watumiaji wa barabara hizo.

Kwa upande wake Meneja wa Mradi wa Mabasi yaendayo Haraka, BRT, Eng. Barakael Mmari amemhakikishia Waziri Mbarawa kuwa kazi ya ujenzi wa barabara hizo itakamilika kama ilivyopangwa mwezi Machi mwakani na ujenzi kwa sasa umefikia asilimia 82.

Naye Mbunge wa Mbagala Mhe. Abdallah Chaurembo amesema ujenzi wa barabara hiyo utapunguza adha ya usafiri kwa wakazi wa Mbagala iliyokuwepo kwa zaidi ya miaka 15.
Muonekano wa magari mara baada ya kuruhusiwa kupita katika barabara ya juu katika makutano ya barabara ya Kilwa na Mandela jijini Dar es Salaam.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad