Wafanyabiashara 15 Wanachama
wa Klabu za Biashara za Benki ya NMB (NMB Business Club), wameagwa
jijini Dar es Salaam leo asubuhi na kuondoka jioni kwenda Istanbul,
Uturuki kwenye ziara ya siku tisa - kutembelea Maonesho ya Biashara ya
Kimataifa (Trade Fairs 2022).
Hafla ya kuwaaga wafanyabiashara
hao imefanyika Makao Makuu ya NMB, ambako Afisa Mkuu wa Mikopo wa Benki
ya NMB, Bw. Daniel Mbotto, aliwakabidhi tiketi za safari hiyo,
akishuhudiwa na Afisa Mkuu wa Huduma Shirikishi NMB, Nenyuata Menjooli
na Mkuu wa Idara ya Biashara wa benki hiyo, Alex Mgeni.
Hii ni
mara ya pili kwa NMB kuratibu ziara za aina hiyo, mara ya kwanza ilikuwa
mwaka 2019, ambako wafanyabiasahara 10 walitembelea na kushiriki
Maonesho ya 125 ya Canton Fair 2019, yaliyofanyika mjini Guangzhou,
China, kabla ya janga la corona kukwamisha safari hizo miaka miwili ya
2020 na 2021.
Akizungumza kabla ya kuwakabidhi tiketi za safari
zao kwenda na kurudi katika ziara hiyo iliyogharamiwa na NMB, Mbotto
alisema lengo la kusafarisha wafanyabiashara hao ni kuwapa fursa ya
kupata ujuzi wa kimaendeleo yatakayowasaidia kukuza biashara zao na
kufundisha wengine pia.
Alivitaja vigezo vilivyotumika kupata
wafanyabiashara hao kuwa ni pamoja na historia yao nzuri ya ukopaji na
urejeshaji mikopo, kupitisha biashara zao kwa asilimia 95 katika benki
ya NMB, kusaidia kwao kuunganisha wafanyabiashara kujiunga NMB na uwezo
wa kuchangia asilimia kidogo za safari.
Aidha, aliwasihi
wafanyabiashara hao kuhakikisha ziara hiyo inaleta mabadiliko yao
kibiashara, wanatumia vema kila fursa watakayoiona na kurejea nyumbani
wakiwa na ujuzi mkubwa, sambamba na kutanua mtandao wa kibiashara ili
kukuza biashara zao na uchumi wa taifa.
Naye mwakilishi wa
wafanyabiashara 15 walio katika msafara huo, Paulo Lema, aliishukuru NMB
kwa fursa mbalimbali inazotoa kwa wateja wao wa kada mbalimbali katika
kuwaongezea nguvu ya kukua kiuchumi na kusisitiza kuwa kadri
wanavyoshikwa mkono, wanarahisishiwa ukuaji wao kibiashara.
Lakini
pia, kwa niaba ya wafanyabiashara waliopata fursa kama hiyo mwaka 2019,
Award Mpandila, ambaye ni Mwenyekiti wa NMB Business Club Mkoa wa Dar
es Salaam, alikiri kuwa ziara yao katika Maonesho ya Canton Fair
yamewasaidia kuwabadili kimfumo, kiuendeshaji na ufanyaji biashara.
Wafanyabiashara
hao watawasili Uturuki saa 12 jioni ya Oktoba 18 na Oktoba 19 2022
kuanza ziara ya kutembelea maonesho hayo ili kuwapa mwanga kibiashara na
watakuwa huko siku 9 wakijifunza mengi kutoka kwa wafanyabiashara
wengine wa kimataifa.
No comments:
Post a Comment