HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, October 4, 2022

TAARIFA KWA UMMA: UZINDUZI WA WIKI YA WAWEKEZAJI KATIKA MASOKO YA MITAJI DUNIANI 2022

 



Mamlaka ya Masoko Ya Mitaji na Dhamana (CMSA) imeanzishwa chini ya Sheria ya Masoko ya Mitaji na Dhamana sura ya 79 na kupewa jukumu la kuendeleza, kuratibu na kusimamia masoko ya mitaji nchini.

CMSA kwa kushirikiana na Taasisi ya Kimataifa inayohusika na Usimamizi na watoaji wa viwango vya Kimataifa vya masoko ya mitaji ulimwenguni yaani International Organization of Securities Commissions (IOSCO) inashiriki katika kuadhimisha wiki ya wawekezaji ulimwenguni iliyoanza Oktoba 3 mpaka Oktoba 7 2022.

 Lengo la kushiriki katika Wiki ya Wawekezaji Duniani ni kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa elimu kwaUmma na ulinzi wa maslahi ya wawekezaji kwa kuangazia jitihada mbalimbali zinazofanywa na Mamlaka za usimamizi wa masoko ya mitaji katika maeneo haya muhimu.

Wiki ya Wawekezaji Ulimwenguni inahusisha Mamlaka za usimamizi wa masoko ya mitaji ambazo ziko chini ya IOSCO pamoja na wanachama wengine wa IOSCO katika mabara sita ambazo hufanya shughuli mbalimbali ikiwa ni pamoja na uzinduzi wa njia za mawasiliano na huduma zinazomlenga mteja, kukuza ushindani wenye tija unaolenga kuongeza wigo wa mikakati mbalimbali ya utoaji wa elimu ya wawekezaji, kuandaa warsha na makongamano, pamoja na kutumia Mamlaka zao kuendesha kampeni za kitaifa.

 Wiki ya wawekezaji inatoa nafasi ya upendeleo maalumu kwa wanachama wa IOSCO kufanya kazi kwa kushirikiana na wadau wote wanaotoa elimu ya uwekezaji kwa umma kwa ngazi ya kitaifa, kikanda na kimataifa. Kauli mbiu ya mwaka huu ni “Uhimilivu wa wawekezaji na Mitaji Endelevu”.

Wiki ya Wawekezaji Ulimwenguni inatarajiwa itaongeza uelewa wa fursa na faida za kutumia masoko ya mitaji nchini ambao unalenga “ Kutambua Ushindani na Maendeleo ya Viwanda kwa Maendeleo ya Watu”. Wiki ya Wawekezaji Ulimwenguni pia inalenga kuongeza ushiriki wa wawekezaji katika masoko ya mitaji hivyo kuwezesha utekelezaji wa Mpango wa Kitaifa wa Huduma Jumuishi za Kifedha na Mpango Mkuu wa Taifa wa Maendeleo ya Sekta ya Fedha.

Pia ushiriki wa CMSA katika Wiki ya Wawekezaji Ulimwenguni umeambatana na maono ya Serikali ya awamu ya sita chini ya uongozi uliotukuka wa Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, ambao unalenga kuweka mazingira wezeshi kwa maendeleo ya sekta ya fedha kwa kuchochea maendeleo na ukuaji wa uchumi Nchini.

Katika kuadhimisha wiki hii, CMSA itafanya shughuli mbalimbali zinazolenga kuongeza uelewa, upatikanaji, ushiriki na kulinda maslahi ya mwekezaji katika masoko ya mitaji kuanzia tarehe 3 mpaka 7 Oktoba 2022. Programu hii inalenga kuimarisha uelewa kuhusu masoko ya mitaji hivyo kuchangia kwenye ajenda ya Taifa ya kuboresha Huduma Jumuishi za kifedha na maendeleo ya uchumi.

CMSA kwa kushirikiana na wadau wa masoko ya mitaji imezindua programu hii tarehe 3 Oktoba 2022 saa 4 kamili asubuhi katika ofisi za Mamlaka.

Tunawatakia wadau wetu wote mafanikio katika kuadhimisha Wiki ya Wawekezaji Ulimwenguni.

Imetolewa na:

CPA. Nicodemus D. Mkama,
Afisa Mtendaji Mkuu,

Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA)
Ghorofa ya 6 , Jengo la PSSF, Mtaa Ohio / Garden ,



No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad