Benki ya NMB imechangia kiasi
cha shilingi milioni 120 kufanikisha maandalizi na kufanyika kwa
mkutano mkuu wa 36 wa Jumuiya ya Tawala za Serikali za Mitaa (ALAT) wa
mwaka huu unaonza leo jijini Mbeya.
Akikabidhi mfano wa hundi ya
mchango huo kudhamini shughuli hiyo ya siku tatu, Afisa Mtendaji Mkuu
wa NMB, Bi. Ruth Zaipuna, alisema wataendelea kushirikiana na ALAT
kulihudumia Taifa huku wakiendeleza mahusiano mema baina yao.
“Uhusiano
kati yetu na ALAT ni wa muda mrefu na umekua wa manufaa makubwa kwa
pande zote mbili. Kwa miaka mingi tumekuwa na mashirikiano na ALAT
katika ngazi zote kuanzia halmashauri hadi ngazi ya Taifa. Katika
kuendelea kuimarisha mahusiano yetu, kama benki tumeona ni vyema
tushiriki katika kufanikisha mkutano huu utakaoanza leo kwa kuchangia
kiasi cha shilingi milioni 120,” alisema Ruth.
Makamu wa Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt Philip Mpango, anatarajiwa kuwa
mgeni rasmi wa mkutano huo ambao kauli mbiu yake, inasisitiza kuongeza
tija katika ukusanyaji na matumizi ya mapato katika halmashauri kama
msingi bora wa maendeleo endelevu ya wananchi.
Benki ya NMB
inatambua kazi kubwa inayofanywa na ALAT chini ya uongozi wa Mwenyekiti
wa ALAT Taifa - Bwana Murshid Ngeze na Katibu Mkuu wake - Ndugu
Elirehema Kaaya, katika kusimamia na kutekeleza malengo yake.
Uongozi
wa ALAT ukiongozwa na Katibu Mkuu wake ndugu Elirehema Moses Kaaya,
uliishukuru Benki ya NMB kwa ajili ya udhamini huo, huku ukisisitiza
kuwa benki hiyo imekuwa sio tu mshiriki mwema wa ALAT, lakini pia kwa
serikali kwa ujumla kwani wamekuwa wakishiriki katika shuguli zake
nyingi lakini hata katika kuchangia shuguli za kimaendeleo, hususani
katika sekta ya elimu na afya.
NMB pia ilidhamini Mkutano Mkuu
wa ALAT wa mwaka jana uliofanyika Jijini Dodoma na kuhudhuriwa na zaidi
ya washiriki 500 kutoka halmashauri 185 za majiji, wilaya na manispaa
kote nchini.
Afisa
Mtendaji Mkuu wa Benki ya NMB - Bi. Ruth Zaipuna akimkabidhi mfano wa
hundi yenye thamani ya shilingi Milioni 120 Makamu Mwenyekiti wa Jumuiya
ya Tawala za Mitaa (ALAT) Mheshimiwa Sima Constatine Sima, ikiwa ni
udhamini wa benki hiyo katika mkutano mkuu wa Jumuiya hiyo, unaotarajiwa
kifunguliwa rasmi na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Dkt. Philip Mpango leo na kumalizika siku ya Jumatano ya tarehe 14
jijini Mbeya.
No comments:
Post a Comment