Makamu na Balozi Wright 02.08.22
Zanzibar
MAKAMU Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe. Othman Masoud Othman, amesema kwamba Serikali ya Zanzibar ipo tayari kushirikiana na Marekani katika utekelezaji wa masuala ya kiuchumi na ujenzi wa Demokrasia na amani.
Mhe. Othman ameyasema hayo Ofisini kwake Migombani mjini Zanzibar alipozungumza na Balozi wa Marekani nchini Tanzania Donald Wright, aliyetaka kufahamu utekelezaji wa masuala ya ushirikiano mbali mbali ukiwemo ujenzi wa demokrasia na utekelezaji wa serikali ya Umoja wa Kitaifa Zanzibar.
Amefahamisha kwamba Zanzibar inaendelea kutekeleza na kutegemea sana sera ya uchumi wa huduma za utalii na ukarimu na kwamba suala la kuwepo utulivu na amani ya kweli katika nchi linabakia kuwa na umuhimu wa pekee katika ujenzi na maendeleo ya nchi.
Amesema kwamba uchumi huo pia unategemea sana kuwepo uwekezaji mkubwa wa aina na sekta mbali mbali mbali na kwamba hakuna muwekezaji anayeweza kuwekeza katika taifa lisilokuwa na amani ya kweli.
Amefahamisha kwamba Viongozi kupitia serikali ya Umoja wa Kitaifa inaendelea na juhudi kubwa ya kuondoa mgawanyiko na kuunganisha wananchi kuwa kitu kimoja jambo ambalo litasaidia sana katika kukuza uchumi wa nchi na kuharakisha maendeleo.
Akizungumzia suala la Serikali ya Umoja wa Kitaifa Mhe. Othman , amesema kwamba suala hilo kuwepo katika Katiba ni fursa muhimu ya kuisaidia nchi na viongozi kuanda na kuweka mfumo bora na miundo imara ya kuimarisha serikali hiyo hatua kwa hatua.
Hata hivyo, Mhe. Othman amesema kwamba tayari kuna hatua na maendeleo makubwa ya uimarishaji wa suala hilo katika maeneo mbali mbali licha kwamba utekelezaji wake kwa baadhi ya masuala unakwenda pole pole.
Amefafanua kwamba hali hiyo imeleta matumaini kwa wananchi na kuona kwa kuna jitihada kubwa zinazofanywa na viongozi wao na ndio maana Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi ameshauri Baraza la Vyama Vya siasa kuunda Kikosi kazi kitakachopewa jukumu la kushughulikia masuala maalumu yanayohusu Zanzibar.
Naye Balozi wa Marekani Donald Wright, amesema kwamba serikali yake itaendelea kushirikiana na Zanzibar katika mauala mbali mbali ikiwemo kuwakuza vijana wa Zanzibar kufaidi fursa za maendeleo na kiuchumi kupitia sekta mbali mbali ikiwemo kilimo, ujasiriamali na kuunga mkono juhudi za SMZ katika kukuza uchumi wa bluu Zanzibar kwa maendeleo ya wananchi.
Balozi huyo pia amesema kwamba hatua hiyo inatokana na serikali ya Marekani kuvutiwa sana na kuwepo utekelezaji wenye matumaini wa serikali ya Umoja wa Kitaifa Zanzibar jambo ambalo litakuza Demokrsia na kuimarisha amani nchini.
Amesema kwamba nchi yake itaendelea kuwa tayari kuunga mkono Zanzibar katika juhudi zozote za kuleta mageuzi ya kiuchumi na kisiasa yatakayohitajika katika sekta tofauti ikiwemo fursa za kuwaleta pamoja wawekezaji na wafanyabishara wa Marekani na Jumuiya za Kimataifa kupitia makongamano mbali mbali kutoa fursa muhimu ya kuchangia juhudi za kuleta maendeleo Zanzibar.
Mwisho
Imetolewa na Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar kupitia Kitengo cha Habari leo tarehe 02.08.22.
MAELEZO YA PICHA
MOJA
Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe. Othman Masoud Othman, akifurahia jambo wakati wa mazungumzo na Balozi wa Marekani nchini Tanzania Donald Wright, leo tarehe 02.08.22. Balozi Wright alifika ofisini kwa Makamu Migombani kwa mazungomzo yanayohusu masuala mbali mbali ya Ushirikiano ikiwemo utekelezaji wa serikali ya Umoja wa Kitaifa na Ujenzi wa Demokrasia nchini. ( Picha na Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Kitengo cha Habari
MBILI
Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe. Othman Masoud Othman, akizungumza na Balozi wa Marekani nchini Tanzania Donald Wright leo tarehe 02.08.22. Balozi Wright alifika ofisini kwa Makamu Migombani kwa mazungomzo yanayohusu masuala mbali mbali ya Ushirikiano ikiwemo utekelezaji wa serikali ya Umoja wa Kitaifa na Ujenzi wa Demokrasia nchini. ( Picha na Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Kitengo cha Habari
TATU
Balozi wa Marekani nchini Tanzania Donald Wright akimtambulisha kwa makamu wa kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe Othman Masoud ofisa ,mwandamizi wa Ubalozi huo Kristin Mencer wakati Balozi huyo alipowasili Ofisini kwa Makamu Migombani mjini Zanzibar kwa ajili ya mazungumzo yanayohusu masuala mbali mbali leo tarehe 02.08.22
NNE
Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe. Othman Masoud Othman, akizungumza na Balozi wa Marekani nchini Tanzania Donald Wright leo tarehe 02.08.22. Balozi Wright alifika ofisini kwa Makamu Migombani kwa mazungomzo yanayohusu masuala mbali mbali ya Ushirikiano ikiwemo utekelezaji wa serikali ya Umoja wa Kitaifa na Ujenzi wa Demokrasia nchini. (Picha na Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Kitengo cha Habari
TANO
Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe. Othman Masoud Othman, akiwa katika picha ya pamoja na Balozi wa Marekani nchini Tanzania Donald Wright, leo tarehe 02.08.22. baada ya kumaliza mazungumzo yao huko ofisini kwa Makamu Migombani mjini Zanzibar. Balozi Wright alifika ofisini kwa Makamu kwa mazungomzo yanayohusu masuala mbali mbali ya Ushirikiano ikiwemo utekelezaji wa serikali ya Umoja wa Kitaifa na Ujenzi wa Demokrasia nchini. ( Picha na Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Kitengo cha Habari
No comments:
Post a Comment