HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Saturday, July 30, 2022

IFM WAADHIMISHA MIAKA 50 TANGU KUANZISHWA, WAASWA KUKIDHI MAHITAJI YA SOKO LA AJIRA

Naibu Katibu Mkuu Wa Wizara ya Fedha na Mipango, Amina Khamis Shaaban na Mkuu wa Chuo wakishangilia baada ya kuzindua miaka 50 ya  hicho Maadhimisho yaliyofanyika leo Julai 29, 2022 Katika Ukumbi wa Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere.
Naibu Katibu Mkuu Wa Wizara ya Fedha na Mipango, Amina Khamis Shaaban akimkabidhi Mkuu wa Chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFM), Dkt. Imanueli Mzava Muundo mpya wa Masomo ya Chuo cha  Usimamizi wa Fedha (IFM), Mkuu wa Chuo hicho wakati wa Maadhimisho ya miaka 50 yaliyofanyika leo Julai 29, 2022 Katika Ukumbi wa Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere.

CHUO Cha Usimamizi wa Fedha (IFM) kinawajibu wa kuendelea kufanya tathmini za mara kwa mara ili kuona namna gani kinaweza kuongeza wabunifu katika shughuli zake za ufundishaji, utafiti na utoaji ushauri wa kitaalamu ili kukidhi mahitaji endelevu ya soko la ajira nchini na duniani.

Hayo yamesemwa leo Julai 29, 2022 na Naibu Katibu Mkuu Wa Wizara ya Fedha na Mipango, Amina Khamis Shaaban wakati akizungumza katika Maadhimisho ya Miaka 50 ya chuo hicho tangu kuanzishwa kwake. Amesema kuwa Umri wa Chuo hicho unatosha kabisa kuwa ni mtaji mzuri kuongoza harakati za mabadiliko chanya katika sekta za usimamizi wa fedha na zinazoshabihiana na hizo.

Pia ameuutaka Uongozi wa Chuo uendelee na mikakati ya kutumia fursa zote zinazoweza kupatikana kufikia malengo waliyojiwekea na kutatua changamoto zinazowakabili.

"Fursa hizo zinaweza kupatikana Serikalini, kutoka kwa wafadhili wa maendeleo hasa upande wa utafiti, na kutumia nguvu ya wahitimu waliosoma katika Chuo hiki."Amesema Amina

Amesema kuwa uwekezaji mkubwa uliofanywa katika rasilimaliwatu utumike kuleta ari ya kufanya kazi kwa bidii na weledi ili kutatua changamoto zinazoikabili jamii.

Amina amesema kuwa Maadhimisho ya miaka 50 ya Chuo cha Usimamizi wa Fedha tuakisi safari ndefu ya Chuo hiki katika kuwahudumia wananchi kulingana na malengo ya uanzishwaji wake.

IFM kama ilivyo kwa vyuo vyote vya elimu ya juu nchini imejengwa katika misingi ya kutoa malezi ya kitaaluma na kitaalamu, ili kupata idadi kubwa ya Watanzania walioelimika na wanaopenda kujielimisha zaidi ili waweze kuchangia katika kufikia malengo ya maendeleo ya Taifa letu.

Hivyo katika maadhimisho haya tunaakisi hazina kubwa ya uono waliokuwa nao waanzilishi wa Chuo hiki katika kujenga misingi imara ya utoaji maarifa hasa ya Usimamizi wa Fedha kwa ngazi mbalimbali.

Jambo ambalo linadhihirisha kuwa uongozi wenye maono hujenga misingi imara ya Taasisi kukidhi mahitaji endelevu ya jamii katika nchi yetu.

Wageni waalikwa,Takwimu zinaonesha kuwa katika miaka 50 ya Chuo hiki kumekuwa na maendeleo makubwa kama Kaimu Mkuu wa Chuo na Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi la Chuo walivyobainisha.

Kumekuwa na ongezeko la kozi za mafunzo, ongezeko la wanafunzi wanaodahiliwa na wanaohitimu. Aidha, katika kuongeza wigo wa kutoa na kusogeza huduma kwa jamii, Chuo kimeanzisha kampasi katika mikoa ya Dodoma, Mwanza na Simiyu.

"Naambiwa muhula mpya wa masomo ifikapo Novemba 2022 Kampasi ya Chato nayo inatarajiwa kuanza kudahili wanafunzi.

Nawapongeza sana IFM kwa ukuaji na maendeleo hayo. Mwenyekiti wa Baraza, Wakati tukisherehekea miaka 50 ya Chuo hiki ni muhimu tutafakari ni kwa viwango gani maendeleo ya kitaaluma na kitaalamu ambayo Chuo kimeyapata yameweza kutatua changamoto zinazoendelea kuwakabili wananchi na Taifa kwa ujumla kwa viwango bora zaidi kuliko huko tulikotoka.

Kwa Upande wa Mkuu wa Chuo hicho, Dkt. Imanueli Mzava amesema kuwa Chuo cha Usimamizi wa Fedha kimedhamiria kuwa taasisi ya elimu ya juu inayoheshimika duniani ambayo inaakisi mahitaji ya maendeleo ya kimataifa kupitia utoaji wa elimu na weledi katika fani za usimamizi wa fedha na zinazoshabihiana na hizo.

"Dhima ya Chuo inaelekeza kuwa Chuo cha Usimamizi wa Fedha kina wajibu wa kutoa mafunzo bora ya kitaaluma na kitaalamu ambayo yatatoa msukumo wa ubunifu na uvumbuzi kwa njia jumuishi za mafunzo, utafiti na ushauri kupitia mafunzo ya fani za fedha na zinazoshabihiana na hizo”. Amesema Dkt. Mzava.

Amesema malengo na shughuli za Chuo hazina budi kuonekana kimkakati kabisa zinatekeleza Dira na Dhima hiyo. "Nizidi kusisitiza kuwa Baraza la Uongozi la Chuo linahakikisha mitaala inayoandaliwa inawawezesha vijana wa kitanzania kuwa wabunifu, kujiajiri na kushindana katika soko la ajira duniani.

Pia tafiti zinazofanywa na wahadhiri wetu na machapisho ya kitaaluma yafanywe kwa viwango vya kimataifa na kuchapishwa ndani na nje ya mipaka ya nchi yetu katika majarida yanayoheshimika duniani ili kukipa Chuo hadhi inayostahili." Amesema Dkt. Mzava.
Naibu Katibu Mkuu Wa Wizara ya Fedha na Mipango, Amina Khamis Shaaban akiwa katika picha ya pamoja wakati wa Maadhimisho ya miaka 50 yaliyofanyika leo Julai 29, 2022 Katika Ukumbi wa Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere.


Naibu Katibu Mkuu Wa Wizara ya Fedha na Mipango, Amina Khamis Shaaban akizungumza wakati wa Maadhimisho ya miaka 50 yaliyofanyika leo Julai 29, 2022 Katika Ukumbi wa Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere.



No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad