HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, June 3, 2022

TANZANIA, IRELAND KUONGEZA MAENEO YA USHIRIKIANO

 Na Mwandishi wetu, Dar

TANZANIA na Ireland zimeahidi kuongeza maeneo mapya ya ushirikiano ambayo ni biashara na uwekezaji, kilimo, viwanda vya nguo pamoja na ujenzi.

Ahadi hiyo imetolewa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula (Mb) alipokutana kwa mazungumzo na Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje wa Ireland, Bw. Joe Hackett katika Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam

“Ireland imekuwa mdau mkubwa wa maendeleo kwa Tanzania katika masuala ya kijamii ikiwemo elimu, kusaidia kaya masikini na kuwajengea uwezo wanawake, kupitia kikao chetu cha leo tumekubaliana kuangalia namna ya kuongeza wigo wa ushirikiano katika sekta ya biashara na uwekezaji, kilimo hasa parachichi, viwanda vya nguo pamoja na ujenzi ili kuweza kuinua zaidi uchumi wetu kwa maslahi ya pande zote mbili,” amesema Balozi Mulamula

Balozi Mulamula ameongeza kuwa kupitia biashara na uwekezaji wafanyabiashara wa Kitanzania watapata fursa ya kuchangamkia biashara zinazopatikana nchini Ireland lakini pia wafanyabiashara wa Ireland watapata fursa ya kuwekeza nchini Tanzania.

Kwa upande wake Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje wa Ireland, Bw. Joe Hackett amesema Ireland wamefurahishwa na hatua ambazo Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan imekuwa ikizichukua katika kuimarisha na kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji pamoja na kuinganisha Tanzania na mataifa mengine ulimwenguni.

“Ireland tunaiona Tanzania ikiwa tulivu na mazingira mazuri ya kuwavutia wafanyabiashara, tutaongea na wafanyabiashara na kuwaeleza kuwa Tanzania ni sehemu salama kuwekeza,” amesema Bw. Hackett

Pamoja na mambo mengine, viongozi hao walijadili masuala mbalimbali ya uhusiano baina ya Tanzania na Ireland katika maeneo yenye maslahi kwa pande zote mbili.

Katika tukio jingine, Balozi Mulamula ameongoza majadiliano ya mpango wa kuimarisha diplomasia ya uchumi ya Tanzania. Wengine walioshiriki katik majadiliano hayo ni Balozi wa Uswisi nchini mhe. Didier Chassot, Mwakilishi Mkazi wa Umoja wa Mataifa (UN), Bw. Zlatan Milišić na Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Maendeleo (UNDP) Christine Musisi, Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Swahiba Mndeme pamoja na wadau wengine wa maendeleo.

Maongezi ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula na Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje wa Ireland, Bw. Joe Hackett yakiendelea katika Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula akizungumza na Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje wa Ireland, Bw. Joe Hackett katika Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi wa Idara ya Amerika na Ulaya kutoka Wizara ya mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Swahiba Mndeme (Mwenye Koti Jekundu) akifuatiwa na Afisa Dawati Bw. Laurian Ntwale, Mkurugenzi wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mindi Kasiga pamoja na Katibu wa Mhe. Waziri, Bw. Seif Kamtunda wakifuatilia kikao cha Balozi Liberata Mulamula na Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje wa Ireland, Bw. Joe Hackett katika Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula na Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje wa Ireland, Bw. Joe Hackett katika picha ya pamoja na Balozi Mindim Kasiga, Balozi Swahiba Mndeme na Bw. Laurian Ntwale kutoka wizarani pamoja na Balozi wa Ireland nchini, Mhe. Mary O’Neil na maafisa waandamizi kutoka ubalozi wa Ireland nchini.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula akiongoza kikao cha majadiliano ya Mpango wa kuimarisha diplomasia ya uchumi ya Tanzania katika Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam.
Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Maendeleo (UNDP) Christine Musisi akieleza jambo katika kikao cha majadiliano ya Mpango wa kuimarisha diplomasia ya uchumi ya Tanzania katika Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam.
Mtaalam akiwasilisha mada katika kikao cha majadiliano ya Mpango wa kuimarisha diplomasia ya uchumi ya Tanzania katika Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam..
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula katika picha ya pamoja na washiriki wa majadiliano ya Mpango wa kuimarisha diplomasia ya uchumi ya Tanzania katika Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad