HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, June 14, 2022

KIJIWE CHA KAHAWA CHAWAKUTANISHA TGNP, WANANCHI NA WADAU WA MAENDELEO

Mkurugenzi wa Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP,) Lilian Liundi akizungumza wakati wa mjadala wa bajeti ya fedha ya Taifa kwa mwaka 2022/2023 na kueleza kuwa jitihada zaidi zinahitajika katika sekta ya kilimo ambayo ushiriki wa wanawake ni mkubwa lakini ukuaji wake umekuwa mdogo, Leo jijini Dar es Salaam.




· Wanawake Kishapu walia na changamoto ya Maji

MTANDAO wa Jinsia Tanzania (TGNP,) umeendelea kuamini katika nguvu ya pamoja kwa kukutana na wadau na wanachama wa mtanda huo na kufuatilia mgawanyo wa rasilimali kwa kupitia bajeti kwa jicho la kijinsia.

Akizungumza wakati wa tafakari ya bajeti ya mwaka wa fedha 2022/2023 kupitia jukwaa la Kijiwe cha Kahawa Mkurugenzi wa Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP,) Lilian Liundi amesema kuwa jukwaa hilo litawasaidia wanajamii na wadau wa maendeleo kutambua fursa na vipaumbele vilivyoainishwa katika bajeti pamoja na mapungufu ya kijinsia yaliyopo katika bajeti ya mwaka husika na kutoa mapendekezo kwa watunga sera na wahusika kuboresha zaidi ili kuwa na bajeti yenye kujenga uchumi na maendeleo endelevu kwa taifa.

Lilian amesema kuwa, bado kuna changamoto katika sekta za maji na kilimo katika bajeti ya mrengo wa kijinsia na takwimu zimekuwa zikiangalia changamoto hizo kwa maeneo ya mjini pekee na kuishauri Serikali kuu kwa kushirikiana na Serikali  za mitaa kupitia Sensa ya watu na makazi inayokwenda kufanyika ilete takwimu sahihi ya wananchi, mahitaji yao pamoja na mgawanyo wa rasilimali kwa mrengo wa kijinsia.

Amesema katika sekta ya kilimo ambayo ina uhakika wa chakula na ushiriki wengi wa wanawake ukuaji wake ni kati ya asilimia 3 hadi 5 na bado uwekezaji wake hauna mkazo na kushauri maagizo na maelekezo yaliyotolewa na Rais Samia Suluhu Hassan katika hotuba yake ya kwanza Bungeni juu ya kutumia malighafi za viwandani kutoka kwa wakulima wazawa litiliwe mkazo ili kujenga uchumi shindani kwa maendeleo endelevu.

Mwanamtandao wa TGNP kutoka Kishapu, Shinyanga Bi. Fregina Said katika kueleza changamoto wanazokumbana nazo akina Mama kujenga uchumi wa taifa kwa mrengo wa kijinsia amesema, upatikanaji wa maji safi na salama bado imeendelea kuwa kikwazo kwa wanawake katika kushiriki katika shughuli za kiuchumi katika Wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga.

Amesema kuwa Kata nyingi wilayani humo nyingi zimepitiwa na mradi mkubwa wa maji kutoka Ziwa Viktoria ila bado hazijafikiwa na huduma hiyo kutokana na gharama ambazo wananchi hawawezi kuzimudu.

‘’Mimi natoka Kata ya Kiloleni kuna kata nyingi ambazo nyingine hazifanyi kazi na TGNP ila zina changamoto kubwa ya maji kuna Kata nyingi hazijapata huduma ya maji licha ya kupitiwa na mradi huo mkubwa…Gharama za kuunganishiwa maji zimefikia hadi shilingi laki mbili na themanini na unit moja inalipiwa shilingi elfu mbili kiasi ambacho mwanamke wa kijijini hawezi kukimudu.’’ Amesema.

Ameeleza kuwa katika harakati za kumtua Mama ndoo kichwani Serikali kupitia bajeti lazima iangalie namna bora ya kutatua changamoto za umbali na gharama ili wanawake ambao ndio wazalishaji wakubwa wajikite katika shughuli za uzalishaji mali.

‘’Baadhi ya Kata zinafuata maji kwa umbali wa Kilomita 15 na maji hayo sio salama na katika harakati hizo hukumbana na unyanyasaji wa kijinsia, mimba za mapema na hata kwa utoro kwa mabinti kutokana na hedhi na shuleni hakuna taulo wala maji ya kuwasitiri.’’ Amesema.

Raheli Misesi kutoka Kishapu, Shinyanga ameeleza katika sekta ya kilimo ambayo wanawake wanashiriki kwa asilimia 80 ni vyema Serikali ikaweka mkazo na juhudi mahususi katika kuboresha kilimo cha umwagiliaji hasa kwa wakulima wadogo vijijini.

‘’Kwa Wilaya ya Kishapu kwa mwaka huu kumekuwa na ukame hakuna mazao kwa sasa debe moja la mahindi linauzwa shilingi elfu kumi na nne hiki ni kiashiria kikubwa cha njaa ni vyema Serikali ikaweka juhudi kwa kuboresha kilimo cha umwagiliaji pamoja na teknolojia za kilimo ikiwemo matumizi ya trekta kwa wakulima wadogo na hiyo ni pamoja na kufanya tafiti kwa mbegu na mbolea za asili ambazo zinafanya vizuri katika ukuaji wa mazao.’’ Amesema.

Aidha amesema kuwa katika kuhakikisha bajeti inakuwa katika mrengo wa kijinsia wametembelea Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kuzungumza na wanawake na akina baba vinara kuhusu changamoto hizo na kushauri namna ya kuongeza bajeti kama TGNP wanavyofanya.

Kuhusiana na sekta ya afya ameishukuru Serikali kwa jitihada za ujenzi wa vituo vya afya na kuiomba kuelekeza nguvu zaidi kwa kupeleka wahudumu wa kutosha pamoja na vifaa tiba.

Jukwaa hilo lililoandaliwa na Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP,) umewakutanisha wananchi, wanajamii, wachambuzi, wanasiasa na wanachama wa mtandao huo na kusikiliza kwa pamoja uwasilishwaji wa bajeti ya Taifa na kutafakari na kujadili kwa mrengo wa kijinsia kwa namna ambavyo bajeti kuu imeakisi kupitia sauti za wanajamii.

 

Afisa Kiongozi wa Programu kutoka TGNP Bi. Joyce Mkina akiwasilisha mada katika jukwaa hilo.

 

Mtafiti wa masuala ya bajeti na mwanachama ya TGNP Edward Mhina akiwasilisha mada katika jukwaa hilo.
 

Mhandisi Wilhelma Malima kutoka shirika la Sanitation and Water Action (SAWA,) akichangia mada katika jukwaa la Kijiwe cha Kahawa maalumu kwa bajeti ya fedha ya mwaka 2022/2023.





















 

Matukio mbalimbali wakati wa mjadala huo.


 

 

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad