HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Saturday, April 23, 2022

Absa yaahidi kuimarisha ubora wa huduma huhakikisha ukuaji endelevu

 
Na Mwandishi Wetu

Benki ya Absa Tanzania imeahidi kumarisha ubora wa huduma zake kwa wateja ili kuhakikisha kuwa ukuaji wa shughuli zake unakuwa endelevu, imeelezwa mjini Zanzibar Jana.

Akizungumza katika hafla ya mlo wa futari iliyoandaliwa na benki hiyo kwa ajili ya wateja wake walio kwenye Mfungo wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhan, Mkuu wa Kitengo cha Biashara wa Absa Tanzania, Melvin Saprapsen, alisema : “ Tuna uhakika na uimara wa shughuli zetu kwa siku zijazo, kwa kuwa tunaendelea kubuni na kuzindua bidhaa nyingi na ufumbuzi ambazo zipo kidijitali zaidi na hivyo kuwezesha wateja wetu kufikia huduma zetu kwa urahisi.”

Alisema mwaka wa fedha wa 2021 ulikuwa mzuri kibishara kwa benki hiyo, kwa kuangalia utendaji wa shughuli zake, ambapo benki iliweza kuibuka kutoka kwenye hasara ya Tsh 532 mwaka 2020 na kujipatia faida Kabla ya Makato ya Kodi ya Tsh 9.4 bilioni kwa mwaka 2021.

“ Katika mwaka huo benki ilizindua bidhaa mpya ya huduma ya utoaji mikopo kwa biashara ndogo na za kati, na vilevile kuboresha mfumo mzima wa miamala kwa biashara ndogo na za kati ikiwa ni sehemu ya mkakati wetu wa kupanua bidhaa na huduma na kuongeza huduma za kidijitali ”alisema Saprapsen.

“ Ushiriki wa benki katika kuchangia shughuli za umma ulikua kwa kiasi kikubwa kwa mwaka 2021, ikiashiria kushika kasi kwa mkakati wa benki wa kupanua nafasi yake katika sekta ya umma ili kuchangia maendeleo ya kijamii na kiuchumi.”

Mkuu wa Kitengo cha Wateja Binafsi, Bi. Ndabu Lilian Swere, akitoa maoni kuhusiana na mwelekeo chanya wa shughuli za benki hiyo, alisema : “ Katika mwaka 2021, benki ilizindua bidhaa kadhaa za kidijitali na kupanua wigo wa aina za bidhaa zake, ikiwa ni pamoja na kuzindua bidhaa ya utoaji wa mikopo kwa wateja binafsi kupitia simu ikishirikiana na kampuni ya mawasiliano ya Tigo Tanzania ambayo imefikia maelfu ya wateja na wasio wateja wao kuwasaidia kufikia huduma za kifedha kwa urahisi zaidi na kuboresha maisha yao.”

Ndabu alisema kuwa Benki ya Absa ina utamaduni wa muda mrefu wa kuandaa hafla za futari ikiwa ni hatua ya kuwashukuru wateja wake , na akaongeza kuwa benki hiyo imejikita katika kutoa huduma kwa wateja wadogo, wa kati na wakubwa, ikiwa ni pamoja na kufanya kazi na serikali na mashirika makubwa ya ndani na nje ya nchi

Akimwakilisha Mufti Mkuu wa Zanzibar katika hafla hiyo, Sheikh Khalid Ali Mfaume alitoa pongezi kwa Absa huku akinukuu moja ya hadithi za Mtume Muhammad inayosema ‘mwenye kumfuturisha aliyefunga anapata malipo ya thawabu zote za aliowafuturisha.”

Benki ya Absa imeendeela kuwa na mtaji wa kutosha kuendesha shughuli zake, ikiwa ni juu ya kiwango kinachohitajika kibishara na kima cha chini kilichowekwa kisheria. Uwezo wa benki wa kidijitali umekuwa ukiimarika zaidi na kuongeza wateja wapya na vilevile kuongeza matumizi ya huduma na bidhaa kwa wateja waliopo.

Kwa mwaka wa fedha wa 2021, Benki ya Absa ilishinda Tuzo Mbalimbali za ubora, ikiwa ni pamoja na Benki Bora ya Matumizi ya Kadi Tanzania ( inayotolewa na Global Brand Magazine ) , Benki Yenye Ubunifu Bora wa Huduma za Wateja Binafsi ( Inayotolewa na Global Business Outlook), na Benki Iliyotia Fora Kwenye Matumizi ya TEHAMA mwaka 2021 inayotolewa na Tume ya TEHAMA Tanzania.


Mwakilishi wa Mufti Mkuu wa Zanzibar, Shehe Khalid Ali Mfaume akihutubia katika hafla ya futari iliyoandaliwa na Benki ya Absa kwa wateja wake wa visiwani humo jana.



Mkuu wa Kitengo cha Biashara wa Benki ya Absa Tanzania, Melvin Saprapasen (kulia), akisaidia kuweka mlo wa futari kwenye sahani ya mmoja wa wateja wao katika hafla waliyoiandaa kwa wateja wao wa Zanzibar, visiwani humo jana.




Meneja wa Tawi la Benki ya Absa Mjini Zanzibar, Rabia Abood (kushoto), akisaidia kuweka mlo wa futari kwenye sahani ya mmoja wa wateja wao katika hafla waliyoiandaa kwa wateja wao wa Zanzibar, visiwani humo jana.



Meneja Huduma za Jamii wa Benki ya Absa Tanzania, Bi.Hellen Siria (kushoto), akisaidia kuweka mlo wa futari kwenye sahani ya mmoja wa wateja wao katika hafla waliyoiandaa kwa wateja wao wa Zanzibar, visiwani humo jana.




Meneja wa Tawi la Benki ya Absa Mjini Zanzibar, Rabia Abood (kulia), akiwakaribisha baadhi ya wateja na wadau wa benki hiyo visiwani humo katika hafla ya futari waliyowaandalia mjini Unguja jana.




Mwakilishi wa Mufti Mkuu wa Zanzibar, Shehe Khalid Ali Mfaume (wa pili kushoto), akiagana na Mkuu wa Kitengo cha Biashara wa Absa Tanzania, Melvin Saprapasen (kulia),mara baada ya hafla ya futari iliyoandaliwa na benki huyo kwa wateja wake wa Zanzibar jana. Kushoto ni Shehe Salum Maridhia kutoka ofisi ya Mufti Mkuu wa Zanzibar na Mkurugenzi wa Makampuni Mkubwa na Uwekezaji wa Absa, Hugo Chilufya.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad